Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 WASOMAJI WETU WANAULIZA . . .

Ni Nani Aliyemuumba Mungu?

Ni Nani Aliyemuumba Mungu?

Mfikirie baba akizungumza na mwanawe mwenye umri wa miaka saba. Anamwambia, “Hapo zamani za kale, Mungu aliumba dunia na kila kitu kilicho ndani yake, aliumba pia jua, mwezi na nyota.” Mvulana huyo anafikiria jambo hilo kwa dakika chache kisha anamuuliza, “Baba, ni nani aliyemuumba Mungu?”

Baba yake anamjibu, “Hakuna mtu aliyemuumba Mungu. Amekuwapo sikuzote.” Jibu hilo rahisi linamridhisha mtoto huyo kwa sasa. Hata hivyo, anapoendelea kukua bado anafikiria swali hilo. Anashindwa kuelewa kwa nini Mungu hana mwanzo. Hata ulimwengu ulikuwa na mwanzo. ‘Mungu alitoka wapi?’ anajiuliza.

Biblia inajibuje? Kwa kweli, inajibu tu kama vile yule baba katika mfano wetu alivyojibu. Musa aliandika: “Ee Yehova, . . . kabla ya kuzaliwa kwa milima, au kutokezwa kwa dunia na nchi yenye kuzaa, tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo wewe ni Mungu.” (Zaburi 90:1, 2) Vilevile, nabii Isaya alisema: “Je, hujajua au, je, hujasikia? Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, ni Mungu mpaka wakati usio na kipimo”! (Isaya 40:28) Vivyo hivyo, barua ya Yuda inasema kwamba Mungu ameishi “kwa umilele wote uliopita.”—Yuda 25.

Maandiko hayo yanatuonyesha kwamba Mungu ni “Mfalme wa umilele,” kama mtume Paulo anavyoeleza. (1 Timotheo 1:17) Hilo linamaanisha kwamba Mungu amekuwapo sikuzote. Na ataendelea kuwapo wakati ujao. (Ufunuo 1:8) Kwa hiyo, kwa vile amekuwepo sikuzote hilo linathibitisha kwamba yeye ni Mweza-Yote.

Kwa nini ni vigumu kwetu kuelewa jambo hilo? Kwa kuwa maisha yetu ni mafupi, maoni yetu kuhusu wakati yanatofautiana sana na ya Yehova. Kwa sababu Yehova ni wa milele, miaka elfu moja ni kama siku moja kwake. (2 Petro 3:8) Kwa mfano: Je, panzi aliyekomaa ambaye huishi siku 50 tu, anaweza kuelewa maisha yetu ya miaka 70 au 80? La hasha! Biblia inaeleza kwamba sisi ni kama panzi tukilinganishwa na Muumba wetu Mkuu. Hata uwezo wetu wa kufikiri ni mdogo sana ukilinganishwa na wake. (Isaya 40:22; 55:8, 9) Hivyo, haishangazi kwamba kuna mambo mengi kumhusu Yehova ambayo wanadamu hawawezi kuelewa kikamili.

Ingawa ni vigumu kwetu kuelewa kwamba Mungu amekuwepo sikuzote, jambo hilo linapatana na akili. Ikiwa mtu fulani angemuumba Mungu, basi mtu huyo angekuwa ndiye Muumba. Hata hivyo, Biblia inaeleza kwamba, Yehova ndiye “[aliye]umba vitu vyote.” (Ufunuo 4:11) Isitoshe, tunajua ulimwengu haukuwepo wakati fulani. (Mwanzo 1:1, 2) Ulitoka wapi? Lazima Muumba alikuwepo. Alikuwepo pia kabla ya viumbe wengine wenye akili, kama vile Mwana wake mzaliwa-pekee na malaika. (Ayubu 38:4, 7; Wakolosai 1:15) Ni wazi kwamba kabla ya kuumba vitu vingine vyote alikuwa peke yake. Hakuumbwa kwa sababu hakukuwa na mtu wa kumuumba.

Kuwepo kwetu na ulimwengu mzima pia kunathibitisha kwamba kuna Mungu anayeishi milele. Yule aliyeuumba ulimwengu na kuweka sheria zinazoudhibiti, lazima amekuwapo sikuzote. Hivyo basi, yeye ndiye aliyeumba vitu vyote.—Ayubu 33:4.