Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MKARIBIE MUNGU

Yehova “Hana Ubaguzi”

Yehova “Hana Ubaguzi”

Je, umewahi kubaguliwa? Je, umewahi kunyimwa ombi au huduma fulani, au kutendewa vibaya kwa sababu ya rangi, kabila, malezi, au hali yako ya kifedha? Ikiwa ndivyo, si wewe peke yako. Hata hivyo, kuna habari njema: Ingawa ubaguzi umeenea sana ulimwenguni, mbinguni hakuna ubaguzi. “Mungu hana ubaguzi,” akasema mtume Mkristo Petro akiwa na uhakika kabisa.Soma Matendo 10:34, 35.

Petro alitamka maneno hayo alipokuwa nyumbani kwa mtu asiye Myahudi aliyeitwa Kornelio. Petro aliyekuwa Myahudi, aliishi kipindi ambacho Wayahudi waliona watu wa mataifa mengine kuwa wasio safi na hivyo hawakupaswa kushirikiana nao. Basi, kwa nini Petro alikuwa nyumbani kwa Kornelio? Ni kwa sababu Yehova Mungu ndiye aliyepanga mkutano huo. Petro alikuwa amepokea maono kutoka kwa Mungu, ambapo aliambiwa: “Wewe acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu ametakasa.” Petro hakujua kwamba siku iliyotangulia Kornelio pia alikuwa amepata maono, ambapo malaika alimwambia amwite Petro. (Matendo 10:1-15) Petro alipogundua kwamba Mungu alihusika katika mpango huo hakujizuia kuzungumza.

“Kwa hakika,” Petro akasema, “ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi.” (Matendo 10:34) Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ubaguzi” kihalisi linamaanisha “kuangalia nyuso.” (The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures) Kuhusu neno hilo, msomi mmoja anafafanua hivi: “Linarejelea hakimu ambaye anamhukumu mtu si kulingana na sheria, bali kwa kutegemea sura yake.” Mungu hapendelei uso wa mtu kwa sababu ya rangi, taifa, hali ya kiuchumi, au sababu nyingine za nje.

Badala yake, Yehova huangalia moyo. (1 Samweli 16:7; Methali 21:2) Kisha, Petro akasema: “Katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:35) Kumwogopa Mungu humaanisha kumstahi, kumheshimu, kumtegemea, na kuepuka kufanya jambo lolote ambalo halimpendezi. Kutenda uadilifu hutia ndani kufanya kwa hiari mambo yanayofaa machoni pa Mungu. Yehova hupendezwa na mtu ambaye moyo wake unachochewa kumwogopa Mungu na anayetamani kufanya yaliyo sawa.Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.

Yehova anapotazama wanadamu akiwa mbinguni, anaona jamii moja tu, yaani, jamii ya wanadamu

Ikiwa umewahi kubaguliwa, kuna sababu nzuri ya kuzingatia maneno ya Petro kuhusu Mungu. Yehova anawavuta watu wa mataifa yote kwenye ibada ya kweli. (Yohana 6:44; Matendo 17:26, 27) Yeye husikiliza na kujibu sala za waabudu wake iwe ni wa rangi, taifa, au hali yoyote ya kiuchumi. (1 Wafalme 8:41-43) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anapotazama wanadamu akiwa mbinguni, anaona jamii moja tu, yaani, jamii ya wanadamu. Je, huchochewi kujifunza mengi kuhusu Mungu huyo asiye na ubaguzi?

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Juni

Yohana 17-21Matendo 1-10