Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maandishi ya Kale Yenye Thamani

Maandishi ya Kale Yenye Thamani

Msomi huyo hakuamini macho yake! Alichunguza kwa makini tena na tena vipande vya maandishi ya kale. Mwandiko na lugha iliyotumiwa ilimsadikisha kwamba alikuwa amepata tafsiri ya kale zaidi ya Biblia ya Kigeorgia!

MAANDISHI hayo yalipatikana mwishoni mwa Desemba 1922, msomi kutoka Georgia anayeitwa Ivané Javakhishvili alipokuwa akifanya utafiti kuhusu jinsi alfabeti za Kigeorgia zilivyotungwa. Alipata nakala ya Talmud ya Yerusalemu. Alipokuwa akiichunguza, aliona chini ya maandishi ya Kiebrania maandishi ya Kigeorgia yaliyofutwa kidogo. *

Maandishi yaliyofutwa kwenye Talmud hiyo yalikuwa kisehemu cha kitabu cha Biblia cha Yeremia kilichoandikwa karne ya tano W.K. Kabla ya kupatikana, maandishi ya kale zaidi ya Biblia ya Kigeorgia yalikuwa ya karne ya tisa W.K. Baadaye, visehemu vya vitabu vingine vya Biblia vilipatikana ambavyo viliandikwa karne ya tano W.K. au mapema zaidi. Wazia kupata maandishi ya Biblia yaliyoandikwa karne chache tu baada ya kifo cha Yesu na mitume wake!

Ni nani aliyeandika tafsiri hiyo? Je, ni mtu mmoja au ni kikundi cha watafsiri wenye bidii? Kufikia sasa, hakuna rekodi ya kihistoria inayoweza kutoa jibu. Vyovyote vile, ni wazi kwamba Biblia nzima, au visehemu vyake, vilikuwa vimetafsiriwa katika Kigeorgia kufikia karne ya nne na pia watu wanaozungumza Kigeorgia wamekuwa na Neno la Mungu tangu wakati huo.

Kitabu The Martyrdom of St. Shushanik the Queen, (Malkia Shushanik Aliyefia Imani) ambacho huenda kiliandikwa mwishoni mwa karne ya tano, kinaonyesha jinsi watu wa Georgia walivyoelewa Maandiko. Anaposimulia msiba uliompata malkia, mwandishi anatia ndani manukuu au marejeo ya Zaburi, Vitabu vya Injili, na sehemu nyingine za Biblia. Pia, anasimulia kwamba Varsken mume wa Shushanik, aliyekuwa gavana wa Ufalme wa Kartili wa Georgia, aliasi “Ukristo,” akawa mfuasi wa dini ya Zoro-aster ya Kiajemi, na akamwamuru mkewe afanye hivyo pia. Kulingana na kitabu hicho,  malkia alikataa kuasi Ukristo na akapata faraja kwa kusoma Maandiko kabla ya kuuawa.

Kazi ya kutafsiri na kunakili Biblia ya Kigeorgia imeendelea kufanywa tangu karne ya tano. Idadi kubwa ya maandishi ya Biblia katika Kigeorgia inathibitisha kazi ngumu ya wanakili na watafsiri wenye bidii. Acheni tuchunguze mambo mawili kuhusu hadithi hii ya kutafsiri na kuchapishwa kwa Biblia.

IDADI KUBWA YA TAFSIRI ZA BIBLIA

“Mimi, Giorgi, kasisi mnyenyekevu, nimetafsiri kitabu cha Zaburi katika Kigeorgia kutoka Kigiriki cha kisasa, kwa jitihada na bidii nyingi.” Hayo ni maneno ya kasisi wa karne ya 11 Giorgi Mtatsmindeli, wa Georgia. Kwa nini kulikuwa na uhitaji wa kutafsiri Biblia ingawa tafsiri ya Kigeorgia ilikuwepo kwa karne nyingi?

Kufikia karne ya 11, ni nakala chache sana za maandishi ya Biblia ya Kigeorgia zilizopatikana. Vitabu fulani vilikuwa vimepotea kabisa. Pia, lugha ilikuwa imebadilika kwa kadiri fulani, hivyo, ilikuwa vigumu kwa wasomaji wengi kuelewa nakala za zamani. Ingawa watafsiri fulani walijitahidi kutokeza tena Biblia ya Kigeorgia, Giorgi ndiye aliyekuwa maarufu zaidi. Alilinganisha tafsiri za Kigeorgia na maandishi ya Kigiriki na akatafsiri sehemu zilizokosekana, na hata vitabu vizima. Mchana, alitimiza majukumu yake akiwa kiongozi wa makao ya watawa. Usiku, alitafsiri Biblia.

Ephrem Mtsire, aliyeishi wakati mmoja na Giorgi, aliongezea kwenye maandishi ya Giorgi maagizo ya kutafsiri. Yalitia ndani kanuni muhimu za kutafsiri, kama vile kutafsiri kutoka lugha ya awali inapowezekana na kufuata maandishi ya awali bila kupoteza maana. Pia, alianzisha zoea la kuongeza maelezo ya chini na marejezo ya pambizoni katika tafsiri za Kigeorgia. Ephrem alitokeza tafsiri mpya kabisa ya vitabu fulani vya Biblia. Kazi ya Giorgi na Ephrem iliweka msingi thabiti wa tafsiri zilizofuata.

Karne zilizofuata, vitabu vingi viliandikwa katika Kigeorgia. Vyuo vilianzishwa katika miji ya Gelati na Ikalto. Wasomi wengi wanatumia sana tafsiri inayoitwa Gelati Bible, iliyo katika Kituo cha Kitaifa cha Maandishi ya Georgia, ambayo ni tafsiri mpya kabisa iliyotafsiriwa na msomi fulani wa Gelati au Ikalto.

Kazi hiyo ya kutafsiri Biblia imekuwa na matokeo gani kwa Wageorgia? Katika karne ya 12, mshairi kutoka Georgia aliyeitwa Shota Rustaveli aliandika shairi Vepkhis-tqaosani (Mwanajeshi Aliyevalia Ngozi ya Chui), ambalo limekuwa maarufu kwa karne nyingi hivi kwamba linaitwa Biblia ya pili ya Kigeorgia. K. Kekelidze,  msomi wa kisasa kutoka Georgia anasema kwamba iwe mshairi huyo alinukuu Biblia moja kwa moja au la, “baadhi ya maneno yake yanafanana kabisa na masimulizi fulani ya Biblia.” Ingawa shairi hilo liliongezwa habari nyingi za kimahaba, linazungumzia hasa urafiki wa kweli, ukarimu, kuwaheshimu wanawake, na kuwapenda wageni. Viwango hivyo vinavyotajwa katika Biblia vilifuatwa na Wageorgia kwa miaka mingi na bado vinaonwa kuwa viwango vinavyofaa vya maadili.

KUCHAPISHA BIBLIA—KAZI YA KIFALME

Mwishoni mwa karne ya 17, familia ya kifalme huko Georgia ilitaka sana Biblia ichapishwe. Ili kutimiza jambo hilo Mfalme Vakh-tang wa Sita alijenga kiwanda cha kuchapisha katika jiji kuu la Tbilisi. Hata hivyo, maandishi ya Biblia hayakuwa yametayarishwa. Kwa njia fulani, Biblia ya Kigeorgia ilikuwa imepotea tena. Ni visehemu tu vya maandishi fulani vilivyopatikana, na lugha iliyotumiwa ilikuwa ya kale. Mtaalamu wa lugha Sulkhan-Saba Orbeliani, ndiye aliyepewa kazi ya kutayarisha maandishi ya Biblia.

Orbeliani alianza kufanya kazi hiyo kwa makini. Kwa vile alijua lugha kadhaa, kutia ndani Kigiriki na Kilatini, alichunguza pia maandishi mengine mbali na maandishi ya Kigeorgia. Hata hivyo, mtazamo wake wa kukubali maoni ya wengine haukupendwa na Kanisa Othodoksi la Georgia. Makasisi walidai kwamba amesaliti kanisa na wakamsadikisha mfalme asimamishe kazi yake ya kutafsiri Biblia. Kulingana na kitabu fulani nchini Georgia, katika kongamano fulani la kanisa, makasisi walimlazimisha Orbeliani achome Biblia aliyokuwa ameitafsiri kwa miaka mingi!

Inapendeza kwamba Maandishi ya Mtskheta (Mcxeta), yanayoitwa pia Saba’s Bible, bado yanapatikana na yana maelezo yaliyoandikwa na Orbeliani. Hata hivyo, watu fulani wanashuku kama hii ndiyo Biblia ambayo makasisi waliipinga. Wanasema kwamba sehemu ya nyongeza ndiyo tu iliyoandikwa naye.

Licha ya matatizo hayo, bado kazi ya kuchapisha Biblia ilikuwa muhimu kwa familia ya kifalme. Sehemu fulani za Biblia hiyo zilichapishwa kati ya 1705 na 1711. Jitihada za wana wawili wa mfalme, Bakari na Vakhshti, zilisaidia sana kukamilisha kazi ya kuchapisha Biblia mwaka wa 1743. Biblia hiyo haingefichwa tena.

^ fu. 3 Zamani, vifaa vya kuandikia havikupatikana kwa urahisi na vilikuwa vya bei ghali. Hivyo, ilikuwa kawaida kufuta maandishi ya kale kisha kutumia mafunjo hayo kuandika maandishi mengine.