Matendo ya Mitume 17:1-34

  • Paulo na Sila huko Thesalonike (1-9)

  • Paulo na Sila huko Beroya (10-15)

  • Paulo huko Athene (16-22a)

  • Hotuba ya Paulo katika Areopago (22b-34)

17  Sasa wakasafiri kupitia Amfipoli na Apolonia wakaenda hadi Thesalonike,+ ambako kulikuwa na sinagogi la Wayahudi.  Basi kulingana na desturi ya Paulo+ akaingia ndani ya sinagogi, na kwa sabato tatu akajadiliana nao akitumia Maandiko,+  akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke+ na kufufuliwa kutoka kwa wafu,+ akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.”  Kwa hiyo, baadhi yao wakaamini na kujiunga na Paulo na Sila,+ pia umati mkubwa wa Wagiriki waliomwabudu Mungu, vilevile wanawake wengi mashuhuri.  Lakini Wayahudi wakawa na wivu,+ wakakusanya wanaume fulani waovu waliokuwa wakizurura sokoni, wakafanyiza kikundi chenye ghasia kisha wakazusha fujo jijini. Wakaishambulia nyumba ya Yasoni wakitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi.  Walipowakosa wakamkokota Yasoni na baadhi ya akina ndugu mpaka kwa watawala wa jiji, wakisema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ambao wameipindua* dunia inayokaliwa wako hapa pia,+  naye Yasoni amewakaribisha. Watu hao wote wanapinga maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.”+  Ule umati na watawala wa jiji waliposikia mambo hayo, wakashtuka;  baada ya kuchukua dhamana ya kutosha kutoka kwa Yasoni na wale wengine, wakawaacha waende zao. 10  Mara tu ilipofika usiku, akina ndugu wakawatuma Paulo na Sila waende Beroya. Walipofika huko, wakaingia ndani ya sinagogi la Wayahudi. 11  Sasa watu hawa walikuwa wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo. 12  Kwa hiyo wengi wao wakawa waamini, vilevile wanawake wengi Wagiriki walioheshimiwa na pia baadhi ya wanaume. 13  Lakini Wayahudi kutoka Thesalonike waliposikia kwamba Paulo alikuwa akitangaza pia neno la Mungu huko Beroya, wakaja huko ili kuchochea na kuuvuruga umati.+ 14  Mara moja akina ndugu wakamsindikiza Paulo mpaka baharini,+ lakini Sila na Timotheo wakabaki huko. 15  Hata hivyo, wale waliomsindikiza Paulo wakaenda naye mpaka Athene, kisha wakarudi baada ya kupokea maagizo kwamba Sila na Timotheo+ wamfuate Paulo haraka iwezekanavyo. 16  Paulo alipokuwa akiwasubiri huko Athene, roho yake ikaudhika sana alipoona kwamba jiji hilo lilikuwa limejaa sanamu. 17  Basi akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi na watu wengine waliomwabudu Mungu na kila siku pamoja na watu aliowakuta sokoni. 18  Lakini baadhi ya Waepikurea na wanafalsafa Wastoa wakaanza kubishana naye, wengine wao wakisema: “Mpigadomo huyu anataka kusema nini?” Nao wengine: “Inaonekana anatangaza miungu ya kigeni.” Kwa sababu alikuwa akihubiri habari njema ya Yesu na ufufuo.+ 19  Kwa hiyo wakamshika na kumpeleka Areopago, wakisema: “Je, tunaweza kujua ni fundisho gani hili jipya unalozungumzia? 20  Kwa maana unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu, na tunataka kujua yanamaanisha nini.” 21  Kwa kweli, Waathene wote na wageni waliokaa* huko walitumia muda wao wa starehe bila kufanya kitu kingine isipokuwa kuambiana au kusikiliza jambo jipya. 22  Basi Paulo akasimama katikati ya Areopago+ na kusema: “Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa mnaogopa sana miungu* kuliko watu wengine.+ 23  Kwa mfano, nilipokuwa nikipita na kutazama kwa uangalifu vitu vyenu vya ibada, niliona pia madhabahu iliyoandikwa, ‘Kwa Mungu Asiyejulikana.’ Kwa hiyo, kile mnachoabudu bila kujua, hicho ndicho ninachowatangazia. 24  Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama alivyo, Bwana wa mbingu na dunia,+ hakai katika mahekalu yaliyotengenezwa kwa mikono;+ 25  wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote,+ kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi+ na vitu vyote. 26  Naye alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja+ ili wakae juu ya uso wa dunia nzima,+ na akaamuru nyakati na kuweka mipaka ya makao ya watu,+ 27  ili wamtafute Mungu, ikiwa watapapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate,+ ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu. 28  Kwa maana kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi, hata kama vile ambavyo baadhi ya washairi wenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni watoto* wake.’ 29  “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni watoto* wa Mungu,+ hatupaswi kufikiri kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na ubunifu wa wanadamu.+ 30  Ni kweli, Mungu ameachilia nyakati hizo za kutojua;+ lakini sasa anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu. 31  Kwa sababu ameweka siku ambayo anakusudia kuihukumu+ kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.”+ 32  Sasa waliposikia kuhusu ufufuo wa wafu, baadhi yao wakaanza kumdhihaki,+ huku wengine wakisema: “Tutakusikiliza kuhusu jambo hili wakati mwingine.” 33  Basi Paulo akawaacha, 34  lakini wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini. Miongoni mwao kulikuwa na Dionisio, aliyekuwa mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke aliyeitwa Damari, na wengineo.

Maelezo ya Chini

Au “wameleta vurugu katika.”
Au “waliotembelea.”
Au “mnapenda sana dini.”
Au “uzao.”
Au “uzao.”