Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya Furaha ya Familia

Kupanga Matumizi ya Pesa

Kupanga Matumizi ya Pesa

Mume anasema: “Ninafikiri mke wangu, Laura, * anatumia pesa kununua vitu visivyo vya lazima—ananunua vitu ambavyo sifikiri tunahitaji. Inaonekana hajui jinsi ya kuweka akiba! Hilo linakuwa tatizo kubwa tunapopata gharama za ghafula. Mara nyingi nimesema kwamba mke wangu akiwa na pesa mfukoni, atazitumia.”

Mke anasema: “Huenda sijui kuweka akiba lakini mume wangu hajui hata kidogo bei ya vitu kama vile chakula, vifaa vya nyumbani, na gharama za nyumbani, na mara nyingi mimi ndiye ninayekaa nyumbani. Ninajua vitu tunavyohitaji, na ninavinunua hata ikiwa hilo litasababisha tena mabishano kuhusu pesa.”

PESA zinaweza kuwa moja kati ya mambo magumu zaidi ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kuzungumzia kwa utulivu. Haishangazi kwamba mara nyingi mambo ya pesa yanaonwa kuwa chanzo kikubwa zaidi cha ugomvi katika ndoa.

Wenzi wa ndoa ambao hawana maoni yenye usawaziko kuhusu pesa wanaweza kufadhaika, kukosana, kupata madhara ya kihisia na hata ya kiroho. (1 Timotheo 6:9, 10) Wazazi ambao hawawezi kusuluhisha matatizo ya pesa huenda wakalazimika kufanya kazi zaidi, na hivyo kukosa kutegemezana na kuwategemeza watoto wao kihisia na kiroho. Pia, hilo linafanya watoto wao wakose usawaziko kuhusiana na pesa.

Biblia inakubali kwamba “pesa ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Lakini pesa zitailinda ndoa na familia yako ikiwa tu utajifunza jinsi ya kuzitumia vizuri na pia jinsi ya kuzungumza na mwenzi wako wa ndoa kuhusu pesa. * Kwa hakika, badala ya kusababisha ugomvi, mazungumzo kuhusu pesa yanaweza kwa kweli kutia nguvu kifungo cha ndoa.

Lakini kwa nini pesa zinasababisha matatizo mengi sana katika ndoa? Na unaweza kuchukua hatua gani zinazofaa ili mazungumzo kuhusu pesa yawe yenye kujenga badala ya kuwa ugomvi?

Pesa Zinasababisha Matatizo Gani?

Mara nyingi, ugomvi kuhusu pesa unasababishwa na kutoaminiana au woga wala si kwa sababu ya pesa au mkopo. Kwa mfano, mume anayedai kwamba mke wake aeleze jinsi anavyotumia kila senti ni kana kwamba anasema haamini kuwa mke wake ana uwezo wa kupanga matumizi ya pesa za familia. Na mke anayelalamika kwamba mume wake haweki pesa za kutosha akibani huenda anaonyesha kwamba anaogopa jambo fulani litatukia wakati ujao na kusababisha matatizo ya kifedha katika familia.

Pia, wenzi wa ndoa wanakabili tatizo lingine, yaani, malezi yao. Matthew, ambaye sasa ameoa kwa muda wa miaka minane anasema: “Mke wangu ametoka katika familia ambayo ilitumia pesa kwa uangalifu. Hana woga kama mimi. Baba yangu alikuwa mlevi na alivuta sigareti mfululizo naye hakupata kazi kwa muda mrefu. Mara nyingi, hatukuwa na vitu vya msingi, hivyo niliogopa sana kuwa na deni. Nyakati nyingine, woga unanifanya nikose usawaziko ninapozungumza na mke wangu kuhusu pesa.” Hata iwe ugomvi wenu unasababishwa na nini, mnaweza kufanya nini ili pesa zenu zinufaishe ndoa yenu badala ya kuiharibu?

Mambo Manne Yatakayowasaidia Kufanikiwa

Biblia haikukusudiwa kuwa kitabu cha kuwasaidia watu kutatua matatizo ya pesa. Lakini ina mashauri yenye hekima ambayo yanaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kuepuka matatizo ya pesa. Kwa nini usisome mashauri hayo na kujaribu kufuata mapendekezo yaliyoorodheshwa hapo chini?

1. Jifunze kuzungumza kwa utulivu kuhusu pesa.

“Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Ikitegemea malezi yako, huenda isiwe rahisi kwako kushauriana na wengine kuhusu pesa, hasa mwenzi wako wa ndoa. Hata hivyo, ni jambo la hekima ujifunze kuzungumzia jambo hilo la maana. Kwa mfano, kwa nini usimweleze mwenzi wako wa ndoa jinsi ambavyo mtazamo wa wazazi wako kuhusu pesa umekuwa na uvutano juu yako? Pia, jitahidi kuelewa jinsi malezi ya mwenzi wako yamekuwa na uvutano juu yake.

Si lazima mngoje mpaka tatizo litokee ndipo mzungumze kuhusu pesa. Mwandikaji mmoja wa Biblia aliuliza hivi: “Je, watu wawili watatembea pamoja isipokuwa wawe wamekutana kwa mapatano?” (Amosi 3:3) Kanuni hiyo inatumika jinsi gani? Mkipanga wakati hususa wa kuzungumza kuhusu masuala ya pesa, mnapunguza uwezekano wa kukosana kwa sababu ya kutoelewana.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Chagueni wakati wa kuzungumzia kwa ukawaida mambo yanayohusu pesa katika familia. Mnaweza kuwa na mazungumzo hayo siku ya kwanza kila mwezi au siku fulani hususa kila juma. Zungumzeni kwa muda mfupi tu, labda kwa dakika 15 hivi au dakika chache zaidi. Chagueni wakati ambao inaelekea nyote wawili mtakuwa mmestarehe. Mkubaliane kwamba hamtazungumza kuhusu pesa pindi nyingine, kama vile wakati wa chakula au mnapopumzika pamoja na watoto.

2. Mkubaliane juu ya maoni ambayo mnapaswa kuwa nayo kuhusu mshahara.

“Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10) Ikiwa wewe tu ndiye unayepata mshahara, unaweza kumheshimu mwenzi wako kwa kuona mshahara wako kuwa pesa za familia bali si pesa zako binafsi.—1 Timotheo 5:8.

Ikiwa wewe na mwenzi wako mnapata mshahara, mnaweza kuonyeshana heshima kwa kuambiana kiasi mnachopata na gharama za kila mmoja wenu. Usipomwambia mwenzi wako jambo moja kati ya mambo hayo, huenda ukamfanya asikuamini na hilo litaharibu uhusiano wenu. Si lazima uwasiliane na mwenzi wako kabla ya kutumia kila senti. Lakini ukimweleza kuhusu vitu vitakavyogharimu pesa nyingi ambavyo unakusudia kununua, unaonyesha kwamba unathamini maoni ya mwenzi wako.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Mkubaliane kuhusu kiasi ambacho kila mmoja wenu anaweza kutumia bila kumweleza mwenzake, iwe ni dola 20, 200, au kiasi kingine. Sikuzote zungumza na mwenzi wako unapotaka kutumia kiasi kikubwa zaidi cha pesa.

3. Andikeni mipango yenu.

“Ukipanga na kufanya kazi kwa bidii, utakuwa na vitu vingi.” (Methali 21:5, Contemporary English Version) Njia moja ya kupanga kwa ajili ya wakati ujao na kuepuka kufanya kazi yako ngumu iwe ya bure ni kupanga bajeti au matumizi ya pesa za familia. Nina, ambaye ameolewa kwa miaka mitano, anasema: “Mtajifunza mengi mkiandika mshahara na matumizi yenu kwenye karatasi. Hamtakuwa na mabishano ikiwa mtaandika jinsi mtakavyotumia pesa zenu.”

Si lazima mpange bajeti yenu kwa njia ya pekee sana. Darren, baba ya wavulana wawili ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 26, anasema: “Mwanzoni, tulitumia bahasha. Tuliweka pesa za kila juma katika bahasha tofauti. Kwa mfano, tulikuwa na bahasha ya pesa za chakula, bahasha ya pesa za burudani, na hata bahasha ya pesa za kinyozi. Pesa za bahasha fulani zilipopungua, tulikopa pesa kutoka katika bahasha nyingine lakini sikuzote tulihakikisha kwamba tumerudisha pesa hizo katika bahasha hiyo haraka iwezekanavyo.” Ikiwa kwa kawaida mnatumia kadi ya mkopo au mfumo wa benki ili kulipia gharama zenu badala ya kulipa kwa pesa taslimu, ni jambo la maana sana kupanga na kuweka rekodi ya gharama zenu.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Andikeni gharama zenu zote ambazo hazibadiliki. Mkubaliane ni kiasi gani cha mshahara wenu mnachopaswa kuweka akiba. Kisha mworodheshe gharama zenu zinazobadilika, kama vile gharama za chakula, umeme, na malipo ya simu. Halafu, muwe na rekodi ya pesa zote ambazo mmetumia kwa miezi fulani. Badilisheni mtindo wenu wa maisha ikiwa ni lazima ili msitumbukie katika madeni.

4. Mkubaliane kuhusu madaraka ya kila mmoja wenu.

“Watu wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa sababu wanatimiza mengi kwa kufanya kazi pamoja.” (Mhubiri 4:9, 10, New Century Version) Katika familia fulani, mume anashughulikia mambo ya pesa. Katika familia nyingine, mke ndiye anayetimiza vizuri daraka hilo. (Methali 31:10-28) Hata hivyo, wenzi wengi wanaamua kusaidiana daraka hilo. Mario, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 21 anasema hivi: “Mke wangu anashughulikia malipo mbalimbali na gharama ndogo-ndogo. Mimi ninashughulikia kodi, mikataba, na malipo ya nyumba. Tunazungumza kuhusu mambo hayo na kufanya kazi pamoja.” Hata iwe mnatumia njia gani kupanga bajeti, siri ni kushirikiana.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Zungumzeni kuhusu ni nani atakayeshughulikia madaraka fulani, huku mkitilia maanani uwezo na udhaifu wa kila mmoja wenu. Chunguzeni tena mpango huo baada ya miezi fulani kupita. Muwe tayari kufanya mabadiliko. Ili kukusaidia uthamini kazi ambayo mwenzi wako anafanya, kama vile kushughulikia malipo mbalimbali au kununua vitu, mnaweza kubadilishana madaraka hayo mara kwa mara.

Mazungumzo Kuhusu Pesa Yanafunua Nini Hasa?

Si lazima mazungumzo yenu kuhusu pesa yaharibu upendo wenu. Leah, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka mitano, aliona ukweli wa jambo hilo. Anasema hivi: “Mimi na mume wangu tumejifunza kuzungumza waziwazi na kwa unyoofu kuhusu pesa. Matokeo ni kwamba sasa tunashirikiana, na upendo wetu umekua.”

Wenzi wa ndoa wanapozungumzia jinsi wanavyotaka kutumia pesa zao, wanakuwa na miradi ileile na wanaonyesha kwamba wameazimia kufanikisha ndoa yao. Wanapozungumza kabla ya kununua vitu vinavyogharimu pesa nyingi, wanaonyesha kwamba wanaheshimu maoni na hisia za wenzi wao. Kila mmoja anapomruhusu mwenzi wake atumie kiasi fulani cha pesa bila kuwasiliana, hilo linaonyesha kwamba wanaaminiana. Hayo ndiyo mambo yanayowasaidia wenzi wa ndoa kuwa na uhusiano wenye upendo wa kweli. Uhusiano wa aina hiyo ni wenye thamani kuliko pesa, kwa hiyo, kwa nini basi mbishane kuhusu pesa?

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 7 Biblia inasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake,” kwa hiyo, ana daraka kuu la kuangalia jinsi pesa za familia zitakavyotumiwa na pia ana wajibu wa kumtendea mke wake kwa upendo na bila uchoyo.—Waefeso 5:23, 25.

JIULIZE . . .

  • Ni wakati gani nilipozungumza mara ya mwisho na mwenzi wangu wa ndoa kuhusu pesa kwa utulivu?

  • Ninaweza kusema na kufanya nini ili kuonyesha kwamba ninathamini msaada wa kifedha ambao mwenzi wangu anatoa kwa familia?