Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninapaswa Kutoa Kiasi Gani cha Pesa?

Ninapaswa Kutoa Kiasi Gani cha Pesa?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Ninapaswa Kutoa Kiasi Gani cha Pesa?

“Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanajua maneno hayo. Hata hivyo, huenda watu fulani wanaoenda kanisani wakahisi kwamba wanalazimika kutoa zaidi ya uwezo wao. Kwa kweli, dini fulani zinawataka washiriki wao watoe kiasi fulani cha pesa. Zoea hilo linaitwa kutoa zaka, yaani, mtu kutoa asilimia 10 ya mapato yake kwa kanisa.

Je, kweli Biblia inatuamuru tutoe kiasi fulani hususa cha pesa kama mchango? Mimi binafsi, ninapaswa kuchanga kiasi gani cha pesa?

Matakwa na Michango ya Hiari Zamani

Biblia ina maagizo ya wazi kwa taifa la Israeli kuhusu kiasi ambacho Mungu alitaka watoe. (Mambo ya Walawi 27:30-32; Hesabu 18:21, 24; Kumbukumbu la Torati 12:4-7, 11, 17, 18; 14:22-27) Matakwa hayo hayakuzidi uwezo wao. Yehova aliahidi kwamba ikiwa wangetii sheria zake, angefanya taifa hilo ‘lifurike kwa ufanisi.’—Kumbukumbu la Torati 28:1, 2, 11, 12.

Nyakati nyingine, Waisraeli walitoa michango mingi au michache ya hiari kadiri walivyotaka. Kwa mfano, Mfalme Daudi alipopanga kumjengea Yehova hekalu, raia wake walitoa “dhahabu yenye thamani ya talanta elfu tano.” * (1 Mambo ya Nyakati 29:7) Tofautisha hilo na yale ambayo Yesu aliona alipokuwa duniani. Alimwona “mjane fulani mwenye uhitaji akitumbukiza . . . sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana” ndani ya sanduku la hazina la hekalu. Mchango wake ulikuwa wa kiasi gani? Ulikuwa tu 1/64 ya mshahara wa siku moja. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba kiasi hicho kidogo kilikubalika.—Luka 21:1-4.

Je, Wakristo Wanapaswa Kutoa Kiasi Fulani cha Pesa?

Wakristo hawako chini ya agano la Sheria ambalo Waisraeli walipewa. Hivyo, hawalazimishwi kumtolea Mungu kiasi fulani cha pesa. Hata hivyo, katika kutaniko la kweli la Kikristo, kutoa kunaleta shangwe kubwa sana. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Mashahidi wa Yehova wanategemeza kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote kupitia michango ya hiari. Michango hiyo inatumiwa kuchapisha vichapo, kama vile gazeti hili unalosoma, na kujenga na kutunza majengo yao ya ibada ambayo yanaitwa Majumba ya Ufalme. Pesa zinazokusanywa hazitumiwi kamwe kulipa mishahara. Wengine wanaojitoa wakati wote katika kazi ya kufanya wanafunzi wanapewa msaada ili kulipia gharama zao za kusafiri na gharama nyingine za kibinafsi. Lakini hakuna mtu anayesisitiza apewe msaada huo. Kwa kweli, Mashahidi wengi wa Yehova hawapewi msaada wowote wa kifedha ili kutegemeza kazi yao ya kuhubiri. Badala yake, wengi wao wanafanya kazi za kimwili ili kujitegemeza wenyewe, kama tu Paulo alivyofanya kazi ya kutengeneza mahema.—2 Wakorintho 11:9; 1 Wathesalonike 2:9.

Ikiwa mtu anataka kutoa mchango kwa ajili ya kazi inayotimizwa na Mashahidi wa Yehova, anapaswa kutoa kiasi gani? Mtume Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 8:12; 9:7.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Katika mwaka wa 2008, bei ya wastani ya dhahabu ilikuwa dola 871 za Marekani kwa wakia au gramu 28.35, hivyo mchango huo ulikuwa na thamani ya dola 4,794,855,000 za Marekani.