Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tutakula nini?”

“Tutakula nini?”

“Tutakula nini?”

WAKATI wa huduma ya Yesu, mara nyingi watu walizungumza kuhusu vyakula na vinywaji. Muujiza wake wa kwanza ulikuwa kugeuza maji kuwa divai, na katika pindi mbili alilisha umati mkubwa wa watu kwa mikate michache na samaki. (Mathayo 16:7-10; Yohana 2:3-11) Watu wengi walijua kwamba Yesu alikula pamoja na maskini na pamoja na matajiri katika karamu. Kwa kweli, maadui wa Yesu walimshtaki kwamba alikuwa mlafi na mlevi. (Mathayo 11:18, 19) Bila shaka, Yesu hakuwa mlafi wala mlevi. Hata hivyo, alijua kwamba chakula na kinywaji vilikuwa vitu vya maana sana kwa wanadamu, na alitumia vitu hivyo kwa ustadi katika mifano alipofundisha mambo mazito ya kiroho.—Luka 22:14-20; Yohana 6:35-40.

Ni vyakula na vinywaji gani vilivyokuwapo kwa kawaida katika siku za Yesu? Chakula kilitayarishwa jinsi gani? Na kazi ya kukitayarisha ilikuwa nyingi kadiri gani? Majibu ya maswali hayo yatakusaidia kuelewa vizuri matukio na mambo fulani yanayotajwa katika Injili.

Utupe “Mkate Wetu kwa Ajili ya Siku Hii”

Yesu alipowafundisha wanafunzi wake jinsi ya kusali, alifunua kwamba ni jambo linalofaa kumwomba Mungu atutimizie mahitaji ya lazima ya maisha, yaani, ‘mkate kwa ajili ya siku hii.’ (Mathayo 6:11) Mkate ulikuwa chakula cha maana sana hivi kwamba katika Kiebrania na Kigiriki, maneno “kula mlo” yalimaanisha kihalisi “kula mkate.” Nafaka zilizotumiwa kuoka mikate, kama vile ngano na shayiri, na nafaka nyinginezo, kama vile ulezi na mtama, zilitumiwa sana katika vyakula vya Wayahudi wa karne ya kwanza. Watafiti wanakadiria kwamba mtu mmoja angeweza kula karibu kilo 200 za nafaka kwa mwaka, na hivyo kupata nusu ya kalori alizohitaji.

Mkate ungeweza kununuliwa sokoni. Lakini familia nyingi zilioka mikate yao wenyewe, na kazi ya kuoka ilikuwa ngumu sana. Kitabu kimoja (Bread, Wine, Walls and Scrolls) kinaeleza hivi: “Kwa kuwa ni vigumu kuhifadhi unga kwa muda mrefu, mke alisaga unga kila siku.” Kazi hiyo ilichukua muda mrefu kadiri gani? Mwandishi wa kitabu hicho anasema hivi: “Baada ya kufanya kazi ngumu ya kusaga unga kwa mkono kwa saa nzima, mtu alipata unga usiozidi kilo 0.8 [karibu pauni mbili] kutokana na kilo 1 ya ngano [zaidi ya pauni mbili].” Kwa kuwa kila mtu alihitaji karibu nusu kilo [pauni moja] ya ngano kila siku, basi ili kulisha familia ya watu watano au sita, mke wa nyumbani alihitaji kusaga ngano kwa muda wa saa tatu.”

Sasa mfikirie Maria, mama ya Yesu. Kwa kuongezea kazi zake nyingine za nyumbani, alihitaji kuoka mikate kwa ajili ya mume, watoto watano wa kiume, na mabinti wawili hivi. (Mathayo 13:55, 56) Bila shaka, Maria, kama wanawake wengine Wayahudi, alijitahidi sana kutayarisha ‘mkate kwa ajili ya siku hii.’

“Njooni, Mpate Kiamsha-Kinywa Chenu”

Baada ya Yesu kufufuliwa, aliwatokea baadhi ya wanafunzi wake asubuhi moja mapema. Wanafunzi hao walikuwa wamejaribu kuvua samaki usiku wote, bila mafanikio. “Njooni, mpate kiamsha-kinywa chenu,” Yesu akawaita marafiki wake waliokuwa wamechoka. Kisha akawaandalia samaki na mkate. (Yohana 21:9-13) Hata ingawa hiyo ndiyo pindi pekee ambayo kiamsha-kinywa kinatajwa katika Injili, kwa kawaida watu walianza siku yao kwa kula mkate, njugu, na zabibu kavu au zeituni.

Namna gani chakula cha mchana? Watu waliofanya kazi walikula nini? Kitabu kimoja (Life in Biblical Israel) kinasema hivi: “Chakula cha mchana kilikuwa chepesi, na kilitia ndani mkate, nafaka, zeituni, na tini.” Inaelekea wanafunzi walikuwa wamebeba vitu hivyo walipotoka Sikari na kumkuta Yesu akizungumza na mwanamke Msamaria kwenye kisima. Ilikuwa “karibu saa sita” au adhuhuri, na wanafunzi “walikuwa wameenda katika jiji kununua chakula.”—Yohana 4:5-8.

Wakati wa jioni, familia zilikusanyika ili kula mlo mkuu wa siku. Kitabu kimoja (Poverty and Charity in Roman Palestine, First Three Centuries C.E.) kinaeleza hivi kuhusu mlo huo: “Watu wengi walikula mkate au kunywa uji wa shayiri, uji wa nafaka na wa mbegu mbalimbali za kunde, na mara chache walikunywa uji wa ngano. Kwa kawaida, waliweka ndani chumvi na mafuta au zeituni, na nyakati nyingine mchuzi mzito wenye vikolezo, asali, au maji matamu ya matunda.” Huenda nyakati nyingine waliandaa maziwa, jibini, mboga, na matunda yaliyokaushwa au yasiyokaushwa. Wakati huo, kulikuwa na karibu aina 30 za mboga, kama vile vitunguu, vitunguu-saumu, figili, karoti, na kabeji, na zaidi ya aina 25 za matunda zilipandwa katika eneo hilo, kama vile (1) tini, (2) tende, na (3) komamanga.

Je, unaweza kuwazia baadhi ya vitu hivyo vikiwa mezani wakati Yesu alipokula chakula cha jioni pamoja na Lazaro na dada zake, Martha na Maria? Sasa wazia harufu nzuri iliyoenea chumbani wakati Maria alipoipaka miguu ya Yesu mafuta ya “nardo halisi.” Wazia harufu nzuri ya chakula ikiwa imechanganyika na harufu yenye kuvutia ya mafuta hayo ya bei ghali.—Yohana 12:1-3.

“Unapoandaa Karamu”

Pindi nyingine, alipokuwa akila chakula “ndani ya nyumba ya mtu fulani, mmoja kati ya watawala wa Mafarisayo,” Yesu aliwafundisha wale waliokuwapo somo la maana sana. Alisema hivi: “Unapoandaa karamu, alika maskini, viwete, vilema, vipofu; nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hao hawana kitu cha kukulipa. Kwa maana utalipwa katika ufufuo wa walio waadilifu.” (Luka 14:1-14) Ikiwa Farisayo huyo alifuata shauri la Yesu, aliandaa chakula cha aina gani katika karamu hiyo?

Huenda mtu tajiri aliandaa mikate ya pekee, yenye maumbo tofauti-tofauti na iliyotiwa ndani divai, asali, maziwa, na viungo mbalimbali. Inaelekea kwamba siagi na jibini ngumu iliwekwa mezani. Zeituni zilizokaushwa na zile ambazo hazijakaushwa, au mafuta ya zeituni bila shaka yaliwekwa mezani. Kulingana na kitabu fulani (Food in Antiquity), “kila mtu alikula kilo 20 [pauni 40] za mafuta ya zeituni kila mwaka katika chakula, na kwa kuongezea, alitumia mafuta hayo katika vipodozi na katika taa.”

Ikiwa Farisayo aliishi karibu na bahari, inaelekea kwamba yeye na wageni wake wangekula samaki waliotoka tu kuvuliwa. Kwa kawaida, wale walioishi mashambani walikula samaki waliohifadhiwa kwa kutiwa chumvi au achari. Huenda mwenye nyumba aliandaa pia nyama, na kwa kawaida mgeni aliye maskini hakupikiwa nyama. Watu wengi waliandaa pia chakula cha mayai. (Luka 11:12) Huenda vyakula hivyo viliongezwa ladha kwa kutiwa viungo na vikolezo, kama vile mnanaa, dili, bizari, na haradali. (Mathayo 13:31; 23:23; Luka 11:42) Baada ya kula chakula kizito, huenda wageni walifurahia kula ngano iliyokaangwa na kuchanganywa na lozi, asali, na vikolezo vingine.

Inaelekea kwamba wale waliohudhuria karamu walipewa zabibu zilizokaushwa na zisizokaushwa, au divai ya zabibu. Maelfu ya mashinikizo ya divai yamepatikana huko Palestina, na hilo linathibitisha kwamba divai ilipendwa sana. Katika eneo moja huko Gibeoni, wataalamu wa vitu vya kale wamegundua maghala 63 yaliyo ndani ya miamba ambayo yangeweza kuhifadhi lita 100,000 hivi za divai.

“Msihangaike Kamwe”

Unaposoma vitabu vya Injili, angalia ni mara ngapi Yesu anataja chakula au kinywaji katika mifano yake au angalia jinsi anavyofundisha masomo fulani ya maana wakati wa kula. Bila shaka, Yesu na wanafunzi wake walifurahia kula na kunywa, hasa walipokuwa pamoja na marafiki wa karibu, lakini hawakufanya mambo hayo yawe ya maana zaidi katika maisha yao.

Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kuwa na mtazamo wenye usawaziko kuhusu vyakula na vinywaji aliposema hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” (Mathayo 6:31, 32) Wanafunzi wa Yesu walifuata shauri hilo, na Mungu aliwatimizia mahitaji yao. (2 Wakorintho 9:8) Huenda vyakula unavyokula leo ni tofauti na vile vilivyokuwapo katika karne ya kwanza. Lakini unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atakutunza ikiwa utatanguliza utumishi wake katika maisha yako.—Mathayo 6:33, 34.