Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfano wa Maria Unatufundisha Nini?

Mfano wa Maria Unatufundisha Nini?

Mfano wa Maria Unatufundisha Nini?

Je, umewahi kulemewa na kipingamizi au jukumu lisilotarajiwa? Je, unahisi umechoka sana kwa sababu ya shughuli za kila siku za kutafuta riziki? Huenda ukawa mmoja kati ya mamilioni ambao wanahisi wamechanganyikiwa na wanaogopa kwa sababu wametoroka nchi zao na wanaishi kama wakimbizi. Na ni nani kati yetu ambaye hajawahi kuhisi uchungu mwingi na upweke baada ya mpendwa wake kufa?

JE, ULIJUA kwamba Maria, mama ya Yesu alikabili matatizo kama hayo? Isitoshe, alikabiliana na matatizo hayo kwa njia inayofaa! Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa mfano wake?

Bila shaka, Maria anajulikana ulimwenguni pote. Na hilo halishangazi kwa sababu alikuwa na sehemu ya pekee katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Zaidi ya hayo, Maria anaabudiwa na mamilioni ya watu. Kanisa Katoliki linamwabudu na kumwona kuwa Mama mpendwa na kama kielelezo cha imani, tumaini, na matendo mema. Wengi wamefundishwa kwamba Maria ni mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu.

Una maoni gani kumhusu mama ya Yesu? Na swali muhimu zaidi ni, Mungu ana maoni gani kumhusu?

Mgawo wa Pekee

Maria, binti ya Heli, alitoka katika kabila la Yuda la Israeli. Anatajwa katika Biblia kuhusiana na tukio lisilo la kawaida. Malaika alimtembelea na kumwambia: “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” Mwanzoni, Maria alishtuka na “kuanza kuwaza hiyo ingeweza kuwa ni salamu ya namna gani.” Kwa hiyo, malaika akamwambia kwamba alikuwa amechaguliwa kwa ajili ya mgawo wa ajabu lakini muhimu sana wa kuchukua mimba, kuzaa, na kumlea Mwana wa Mungu.—Luka 1:26-33.

Hilo lilikuwa jukumu zito kama nini ambalo mwanamke huyo kijana ambaye hakuwa ameolewa alipewa! Alitenda jinsi gani? Huenda Maria alijiuliza ni nani angeamini maneno hayo. Je, mimba hiyo ingeharibu uhusiano wake na Yosefu mchumba wake au ingemfanya aaibishwe hadharani? (Kumbukumbu la Torati 22:20-24) Hakusitasita kukubali mgawo huo muhimu.

Imani yenye nguvu ya Maria ilimwezesha afanye mapenzi ya Mungu wake Yehova. Aliamini kabisa kwamba angemtegemeza. Kwa hiyo alisema hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” Maria alikuwa tayari kukabiliana hali ngumu zilizokuwa mbele yake kwa sababu kwa kufanya hivyo angemletea Mungu heshima.—Luka 1:38.

Maria alipomwambia Yosefu kwamba alikuwa na mimba, Yosefu alitaka kuvunja uchumba wao. Huenda hicho kilikuwa ni kipindi chenye kufadhaisha sana kwa wote wawili. Biblia haielezi urefu wa kipindi hiki kigumu. Hata hivyo, huenda Maria na Yosefu walifarijiwa sana wakati malaika wa Yehova alipomtokea Yosefu. Mjumbe huyo kutoka kwa Mungu alieleza kuhusu mimba ya Maria isiyo ya kawaida na akamwambia Yosefu ampeleke nyumbani awe mke wake.—Mathayo 1:19-24.

Nyakati Ngumu

Leo, wanawake wengi wajawazito wanatumia miezi mingi wakijitayarisha kwa ajili ya mtoto atakayezaliwa, na huenda Maria alifanya hivyo pia. Huyo angekuwa mtoto wake wa kwanza. Hata hivyo, mambo yasiyotazamiwa yalitatiza mipango yake. Kaisari Augusto aliagiza watu wahesabiwe, na kwamba kila mtu aandikishwe katika mji ambao alizaliwa. Kwa hiyo, Yosefu akamchukua Maria, ambaye sasa alikuwa na mimba ya miezi tisa, na kusafiri umbali wa kilomita 150 hivi, huenda akitumia punda! Mji wa Bethlehemu ulikuwa umejaa watu na Maria alihitaji mahali pa faragha ili azae, lakini mahali pekee alipopata palikuwa ni hori. Ni lazima liwe lilikuwa jambo gumu sana kwa Maria kumzaa mtoto katika hori. Huenda aliaibika na kuogopa.

Katika nyakati hizo ngumu maishani mwake, bila shaka Maria alimmiminia Yehova moyo wake, akiamini kwamba angemlinda pamoja na mtoto wake mchanga. Baadaye wachungaji waliwasili, wakitamani kumwona mtoto huyo. Walisema kwamba malaika walikuwa wamemwita mtoto huyo “Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana.” Kisha tunasoma hivi: “Maria akaanza kuyahifadhi maneno hayo yote, akikata kauli moyoni mwake.” Alitafakari kuhusu maneno hayo nayo yakamtia nguvu.—Luka 2:11, 16-19.

Namna gani sisi? Huenda tukapatwa na matatizo maishani. Kwa kuongezea, Biblia inaonyesha kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” linaweza kumpata yeyote kati yetu na kutokeza matatizo na vipingamizi vya aina mbalimbali katika maisha yetu. (Mhubiri 9:11) Jambo kama hilo likitokea, je, tutakasirika na kumlaumu Mungu? Je, haingekuwa afadhali kuiga mtazamo wa Maria kwa kumkaribia Yehova Mungu kwa kujifunza Neno lake, Biblia, kisha kutafakari kuhusu mambo tunayojifunza? Bila shaka, kufanya hivyo kutatusaidia kuvumilia majaribu.

Maskini na Mkimbizi

Maria alikabili matatizo mengine pia kutia ndani umaskini na kulazimika kutoroka nchi yake. Je, umekabili matatizo kama hayo? Kulingana na ripoti moja, “nusu ya watu ulimwenguni, yaani, watu karibu bilioni tatu, wanajiruzuku kwa dola mbili hivi kila siku,” na mamilioni ya watu wengine wanajitahidi sana kutafuta riziki ingawa wanaishi katika nchi zinazoonwa kuwa tajiri. Namna gani wewe? Je, shughuli za kila siku za kuiandalia familia yako chakula, mavazi, na nyumba zinakuchosha au hata kukulemea nyakati nyingine?

Biblia inaonyesha kwamba Yosefu na Maria walikuwa maskini. Tunajua namna gani? Kati ya mambo machache ambayo vitabu vya Injili—Mathayo, Marko, Luka, na Yohana—vinatuambia kuhusu wenzi hawa wa ndoa ni kwamba siku 40 baada ya Maria kuzaa, yeye na Yosefu walienda katika hekalu ili kutoa dhabihu iliyohitajiwa, yaani, “njiwa-tetere wawili au hua wachanga wawili.” * (Luka 2:22-24) Walioruhusiwa kutoa dhabihu hiyo ni wale tu waliokuwa maskini sana hivi kwamba hawangeweza kutoa kondoo-dume mchanga. Kwa hiyo, yaelekea kwamba, Yosefu na Maria walijitahidi ili kujiruzuku. Hata hivyo, walifaulu sana kuandaa mazingira ya familia yenye upendo. Bila shaka, walitanguliza mambo ya kiroho maishani.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Muda mfupi baada ya Yesu kuzaliwa, mambo yalianza kumwendea Maria kombo tena. Malaika alimwambia Yosefu aichukue familia yake na kutorokea Misri. (Mathayo 2:13-15) Hiyo ilikuwa mara ya pili kwa Maria kuondoka katika eneo alilozoea, lakini wakati huu ilimbidi kuhamia nchi nyingine. Nchi ya Misri ilikuwa na Wayahudi wengi, kwa hiyo huenda Maria na Yosefu waliishi kati ya watu wa jamii yao. Hata hivyo, si rahisi kuishi katika nchi ya kigeni na ni jambo linaloweza kumfanya mtu achanganyikiwe. Je, wewe na familia yako ni kati ya mamilioni ya watu ambao wamehama kutoka nchi yao, huenda ili wawalinde watoto wao au kuepuka hatari? Ikiwa ni hivyo, huenda unaelewa baadhi ya matatizo ambayo labda Maria alikabili nchini Misri.

Mke na Mama Mwenye Bidii

Mbali na masimulizi ya kuzaliwa na maisha ya utotoni ya Yesu, Maria hatajwi sana katika vitabu vya Injili. Hata hivyo, tunajua kwamba Maria na Yosefu walikuwa na angalau watoto wengine sita. Huenda ukashangazwa na hilo. Lakini fikiria yale ambayo vitabu vya Injili vinasema.

Yosefu aliheshimu sana pendeleo la Maria la kubeba mimba ya Mwana wa Mungu. Kwa hiyo, aliepuka kufanya ngono naye kabla Yesu hajazaliwa. Mathayo 1:25 inasema kwamba Yosefu “hakufanya ngono naye mpaka alipozaa mwana.” Neno “mpaka” katika mstari huo linaonyesha kwamba baada ya Yesu kuzaliwa, Yosefu na Maria walifanya ngono kama mke na mume. Vitabu vya Injili vinasema kwamba kwa sababu hiyo Maria na Yosefu walipata watoto, wana na mabinti. Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yudasi walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu. Alikuwa na angalau mabinti wawili. (Mathayo 13:55, 56) Hata hivyo, mimba za watoto hao zilitungwa kwa njia ya kawaida. *

Maria alikuwa mtu aliyethamini mambo ya kiroho. Ingawa sheria haikuwaamuru wanawake wahudhurie sherehe ya Pasaka, kwa kawaida Maria aliandamana na Yosefu kwenye safari ya kila mwaka hadi Yerusalemu kwa ajili ya sherehe hiyo. (Luka 2:41) Hilo lilimaanisha kwamba wangesafiri umbali wa kilomita 300 hivi kwenda na kurudi kila mwaka pamoja na familia iliyokuwa ikiongezeka! Lakini bila shaka safari hizo ziliandaa nafasi za familia kufurahia pamoja.

Wanawake wengi leo wanaiga mfano mzuri wa Maria. Wao wanafanya kazi kwa bidii na bila ubinafsi ili kutimiza majukumu yao ya Kimaandiko. Mara nyingi wake hao wanaonyesha subira, uvumilivu, na unyenyekevu mwingi! Kutafakari juu ya mtazamo wa Maria kunawasaidia kutanguliza mambo ya kiroho badala ya starehe na anasa. Kama Maria, wanajua kwamba kumwabudu Mungu pamoja na mume na watoto wao kunaimarisha na kuifanya familia iwe na umoja zaidi.

Siku moja, Maria na Yosefu walipokuwa wakitoka kwenye sherehe huko Yerusalemu, huenda wakiwa na watoto kadhaa sasa, waligundua kwamba Yesu aliyekuwa na umri wa miaka 12 hakuwa pamoja nao. Je, unaweza kuwazia wasiwasi ambao Maria alihisi alipomtafuta kwa bidii mwana wake kwa siku tatu? Yeye na Yosefu walipompata hekaluni, Yesu aliwaambia: “Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Kwa mara nyingine, simulizi hilo linasema, Maria “akaweka kwa uangalifu maneno yote hayo moyoni mwake.” Hilo ni jambo lingine linaloonyesha hali nzuri ya kiroho ya Maria. Alitafakari kwa uangalifu kuhusu mambo yote yaliyompata Yesu. Miaka mingi baadaye, huenda aliwasimulia waandikaji wa vitabu vya Injili mambo aliyokumbuka kuhusu tukio hilo na matukio mengine ya maisha ya mapema ya Yesu.—Luka 2:41-52.

Kuvumilia Mateso na Msiba

Ni nini kilichompata Yosefu, baba wa kambo wa Yesu? Baada ya kutajwa kifupi katika tukio hilo Yesu alipokuwa kijana, Yosefu hatajwi tena katika vitabu vya Injili. Watu fulani wanafikiri kwamba hilo linaonyesha Yosefu alikufa muda fulani kabla ya huduma ya Yesu kuanza. * Vyovyote vile, inaonekana kwamba kufikia mwisho wa huduma ya Yesu, Maria alikuwa mjane. Alipokuwa akielekea kufa, Yesu alimkabidhi mtume Yohana jukumu la kumtunza mama yake. (Yohana 19:26, 27) Ikiwa Yosefu angekuwa bado hai, huenda Yesu hangefanya hivyo.

Maria na Yosefu walikuwa wamepitia mambo mengi sana pamoja! Walikuwa wametembelewa na malaika, wakahepa mtawala mkatili, wakahama mara kadhaa, na wakazaa watoto wengi. Ni mara ngapi walipoketi pamoja jioni na kuzungumza kuhusu Yesu, wakijiuliza atakabili mambo gani wakati ujao, na kujiuliza ikiwa walikuwa wakimzoeza na kumtayarisha kwa njia inayofaa? Kisha ghafula Maria alijikuta peke yake.

Je, umempoteza mwenzi wako katika kifo? Je, bado unahisi uchungu na upweke unaoletwa na msiba huo, hata baada ya miaka mingi? Bila shaka Maria alifarijiwa na imani yake na ujuzi wa kwamba kutakuwa na ufufuo. * (Yohana 5:28, 29) Hata hivyo, mawazo hayo yenye kufariji hayakumwondolea Maria matatizo yake. Kama ilivyo na akina mama wengi wasio na wenzi wa ndoa, Maria alikuwa na daraka gumu la kutunza watoto wake bila msaada wa mume.

Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba Yesu alichukua daraka la kuiandalia familia mahitaji Yosefu alipokufa. Ndugu za Yesu walipoendelea kukua wangekubali daraka la kuiandalia familia mahitaji. Yesu “alikuwa na umri wa karibu miaka 30” alipoondoka nyumbani na kuanza huduma yake. (Luka 3:23) Wazazi wengi wanafurahi na wakati uleule wanahuzunika sana mwana au binti yao anapoondoka nyumbani. Wazazi wanatumia wakati, jitihada, na kuwaonyesha watoto hisia nyingi hivi kwamba wanakuwa wapweke sana watoto wanapoondoka. Je, wana au mabinti wako wameondoka nyumbani ili wafuatilie miradi yao? Je, unafurahi kwamba wanafuatilia miradi hiyo lakini unatamani kwamba wangekuwa karibu zaidi? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kuwazia jinsi Maria alivyohisi Yesu alipoondoka nyumbani.

Majaribu Yasiyotarajiwa

Huenda Maria hakuwa ametarajia jaribu lingine ambalo alikabili. Yesu alipohubiri, watu wengi walimfuata—lakini ndugu zake hawakumfuata. Maandiko yanasema: “Kwa kweli, ndugu zake walikuwa hawamwamini.” (Yohana 7:5) Bila shaka, Maria aliwaambia yale ambayo malaika alikuwa amemwambia, yaani, Yesu alikuwa “Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Lakini Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yudasi, walimwona Yesu kuwa kaka yao tu. Hivyo, Maria alijikuta katika familia ya watu wa dini zinazotofautiana.

Je, Maria alivunjika moyo na kukata tamaa kuhusiana na hali hiyo? La hasha! Wakati mmoja, Yesu alipokuwa akihubiri huko Galilaya, alienda kula katika nyumba fulani na umati ukakusanyika ili kumsikiliza. Ni nani waliokuwa nje wakimtafuta? Maria na ndugu za Yesu. Hivyo, Yesu alipokuwa karibu na nyumba ya familia yao, Maria alimfuata pamoja na watoto wake wengine, huenda akitumaini kwamba watabadili mtazamo wao kumwelekea.—Mathayo 12:46, 47.

Huenda wewe pia unakabili tatizo la kumfuata Yesu huku washiriki wengine wa familia yenu wakiwa hawataki kufanya hivyo. Usivunjike moyo wala usikate tamaa! Watu wengi, kama tu Maria, wamewatia moyo kwa subira washiriki wa familia kwa miaka mingi kabla ya kuona mabadiliko yoyote. Uvumilivu huo una thamani machoni pa Mungu, iwe wanadamu wengine wanaitikia au la.—1 Petro 3:1, 2.

Jaribu Gumu Zaidi

Jaribu la mwisho la Maria lililorekodiwa katika Maandiko, bila shaka lilikuwa lenye kuumiza sana. Alimwona mwana wake mpendwa akifa kifo cha maumivu sana baada ya kukatiliwa na watu wake. Kifo cha mtoto kimesemwa kuwa “msiba mkuu zaidi,” “kifo kinachoumiza zaidi,” iwe mtoto huyo ni mchanga au ni mtu mzima. Kama ilivyotabiriwa miaka mingi mapema, Maria alihisi kana kwamba upanga umemchoma!—Luka 2:34, 35.

Je, Maria aliruhusu jaribu hilo la mwisho limlemee kihisia au lidhoofishe imani yake katika Yehova? Hapana. Mara nyingine ambapo Maria anatajwa katika Biblia, ni wakati alipokuwa na wanafunzi wa Yesu ‘akidumu katika sala’ pamoja nao. Na hakuwa peke yake. Wana wake ambao wakati huo walikuwa wameanza kuwa na imani katika kaka yao, walikuwa pamoja naye. Jambo hilo lilimfariji Maria kama nini! *Matendo 1:14.

Maria alifurahia maisha yenye kuridhisha akiwa mwanamke, mke, na mama mwaminifu. Alijionea mambo mengi yenye kufurahisha katika kumtumikia Mungu. Alishinda majaribu mengi sana. Tunapopatwa na matatizo tusiyotazamia au tunapokuwa na wasiwasi kwa sababu ya matatizo katika familia, bila shaka tunaweza kujifunza kutokana na mfano wake wa kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu ingawa alipatwa na magumu mengi.—Waebrania 10:36.

Hata hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu kuabudiwa kwa Maria? Je, simulizi la Biblia kuhusu jukumu muhimu la Maria linaonyesha kwamba anapaswa kuabudiwa?

[Maelezo ya chini]

^ fu. 17 Ndege mmoja alitolewa kuwa toleo la dhambi. (Mambo ya Walawi 12:6, 8) Kwa kuitoa, Maria alionyesha kwamba yeye kama wanadamu wengine wote wasio wakamilifu alikuwa amerithi matokeo ya dhambi ya Adamu, mwanadamu wa kwanza.—Waroma 5:12.

^ fu. 26 Imeonekana kwamba kutotajwa tena kwa Yosefu katika masimulizi ya huduma ya Yesu ni jambo lenye kutokeza kwa sababu washiriki wengine wa familia ya Yesu, yaani, mama, ndugu na dada zake wanatajwa. Kwa mfano, katika karamu ya arusi huko Kana, Maria anatajwa na hata inaonekana alikuwa na daraka fulani, lakini Yosefu hatajwi. (Yohana 2:1-11) Katika kisa kingine, tunaona watu katika mji wa nyumbani wa Kristo wakimtaja Yesu kuwa “mwana wa Maria” wala si mwana wa Yosefu.—Marko 6:3.

^ fu. 28 Kwa habari zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 36 Ona sanduku  “Alikuwa na Ujasiri wa Kubadili Dini,” katika ukurasa wa 7.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

 Je, Yesu Alikuwa na Ndugu na Dada?

Ndiyo, alikuwa nao. Wanatheolojia fulani wamejaribu kuupinga ukweli huo hata ingawa vitabu vya Injili vinathibitisha jambo hilo mara kadhaa. (Mathayo 12:46, 47; 13:54-56; Marko 6:3) Hata hivyo, wasomi wa Biblia wametoa hoja mbili kuhusu nadharia za kwamba Maria hakupata watoto wengine. Kwanza, nadharia hizo zinachochewa na fundisho la kanisa lililotokea baadaye, yaani, Maria alibaki bikira maisha yake yote. Pili, nadharia hizo haziwezi kuthibitishwa.

Kwa mfano, nadharia moja inadokeza kwamba “ndugu” wanaotajwa walikuwa ndugu wa kambo, yaani, wana ambao Yosefu alipata katika ndoa ya mapema. Wazo hilo halina msingi kwa sababu lingemfanya Yesu asiwe na haki ya kisheria ya mzaliwa wa kwanza ya kurithi kiti cha ufalme cha Daudi.—2 Samweli 7:12, 13.

Nadharia nyingine inasema kwamba ndugu hao walikuwa binamu za Yesu, ingawa Maandiko ya Kigiriki yanatumia maneno tofauti kwa ajili ya “ndugu,” “binamu,” na “mtu wa ukoo.” Kwa hiyo, msomi Frank E. Gaebelein anasema kuwa nadharia hizo za kidini ni mawazo ya kubuniwa. Anamalizia kwa kusema: “Njia ya kawaida ya kuelewa neno ‘ndugu’ . . . ni kwamba neno hilo linarejelea wana wa Maria na Yosefu na hivyo wao ni ndugu za Yesu wa mama mmoja.”

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

 Alikuwa na Ujasiri wa Kubadili Dini

Maria alizaliwa katika familia ya Kiyahudi na alifuata dini ya Wayahudi. Alihudhuria ibada katika sinagogi, jina la mahali pa ibada pa Wayahudi, na alienda hekaluni huko Yerusalemu. Hata hivyo, kadiri ujuzi wa Maria kuhusu makusudi ya Mungu ulivyoendelea kukua, alitambua kwamba desturi za mababu wake hazikukubaliwa na Mungu. Viongozi wa kidini Wayahudi walimwua Mwana wake, Masihi. Kabla ya tukio hilo, Yesu aliwaambia: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38) Mungu aliondoa baraka zake kutoka kwa mfumo wa kidini ambao Maria alikuwa akifuata tangu utotoni.—Wagalatia 2:15, 16.

Kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, huenda Maria alikuwa na umri wa miaka 50 hivi. Angefanya nini? Je, alisema kwamba alikuwa amezaliwa katika mfumo wa kidini wa Kiyahudi na alitaka kuwa mshikamanifu kwa mababu zake? Je, alisema kwamba alikuwa mzee sana asiweze kubadili dini? Hapana! Maria alielewa kwamba sasa Yehova alibariki kutaniko la Kikristo hivyo akawa na imani na ujasiri wa kubadili dini.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kukimbilia Misri wakiwa wakimbizi

[Picha katika ukurasa wa 8]

Jambo gumu zaidi ambalo mama anaweza kukabili