Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Makao Yetu

Yehova Ni Makao Yetu

“Ee Yehova, wewe mwenyewe umekuwa makao yetu halisi kwa kizazi baada ya kizazi.”—ZAB. 90:1.

1, 2. Watumishi wa Mungu wamehisije kuhusu mfumo huu wa mambo, na wana makao katika maana gani?

 JE, UNAJIHISI ukiwa salama katika ulimwengu wa leo? Ikiwa sivyo, kumbuka kwamba watumishi wengine wa Yehova wamekuwa na hisia kama hizo. Katika historia yote, watu wote wanaompenda kikweli Yehova wamekuwa kama wageni, au wakaaji wa muda katika mfumo huu wa mambo. Kwa mfano, walipohama kutoka kambi moja hadi nyingine katika nchi ya Kanaani, waabudu waaminifu wa Mungu ‘walitangaza hadharani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda.’—Ebr. 11:13.

2 Vivyo hivyo, wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta, ambao ‘uraia wao uko mbinguni,’ wanajiona kuwa “wageni na wakaaji wa muda” katika mfumo huu wa mambo. (Flp. 3:20; 1 Pet. 2:11) “Kondoo wengine” wa Kristo pia ‘si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo Yesu hakuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yoh. 10:16; 17:16) Hata hivyo, watu wa Mungu wana “makao.” Isitoshe, tuna makao yenye upendo na yaliyo salama zaidi, ambayo huonekana tu kwa macho ya imani. Musa aliandika hivi: “Ee Yehova, wewe mwenyewe umekuwa makao yetu halisi kwa kizazi baada ya kizazi.” * (Zab. 90:1) Yehova alithibitikaje kuwa ‘makao halisi’ kwa watumishi wake washikamanifu katika nyakati za kale? Yeye ni ‘makao halisi’ jinsi gani kwa watu wanaoitwa kwa jina lake leo? Na atathibitikaje kuwa makao pekee salama wakati ujao?

YEHOVA—“MAKAO HALISI” KWA WATUMISHI WAKE WA KALE

3. Ni jambo gani kuu, mfano, na ulinganifu gani unaokaziwa katika Zaburi 90:1?

3 Kama tu ilivyo na maneno mengine ya mfano yanayotumiwa katika Biblia, andiko la Zaburi 90:1  lina jambo kuu, mfano, na ulinganifu. Jambo kuu linalozungumziwa ni Yehova. Mfano unaotumiwa ni makao, au mahali pa kuishi. Yehova anaweza kufananishwa na makao. Kwa mfano, Yehova huwalinda watu wake. Hilo linapatana na uhakika wa kwamba yeye ni mfano bora zaidi katika kuonyesha upendo. (1 Yoh. 4:8) Yeye pia ni Mungu wa amani, anayewafanya washikamanifu wake ‘wakae kwa usalama.’ (Zab. 4:8) Kwa mfano, fikiria jinsi alivyoshughulika na wazee wa ukoo waaminifu, kuanzia Abrahamu.

4, 5. Mungu alithibitikaje kuwa “makao halisi” kwa Abrahamu?

4 Tunaweza tu kuwazia jinsi Abrahamu, aliyeitwa Abramu wakati huo, alivyohisi Yehova alipomwambia hivi: “Nenda zako kutoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako . . . mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.” Ikiwa Abrahamu alikuwa na wasiwasi, bila shaka wasiwasi huo ulitoweka alipoambiwa hivi na Yehova: “Nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki na kulifanya jina lako kuwa kuu . . . Nami nitawabariki wale wanaokubariki, na yule anayekulaani nitamlaani.”—Mwa. 12:1-3.

5 Kwa maneno hayo, Yehova aliahidi kwamba angekuwa makao salama kwa Abrahamu na uzao wake. (Mwa. 26:1-6) Yehova alitimiza ahadi yake. Kwa mfano, alimzuia Farao wa Misri na Mfalme Abimeleki wa Gerari wasimnajisi Sara na kumwangamiza Abrahamu. Alimlinda Isaka na Rebeka kwa njia hiyohiyo. (Mwa. 12:14-20; 20:1-14; 26:6-11) Tunasoma hivi: “[Yehova] hakumruhusu binadamu yeyote awapunje, bali aliwakaripia wafalme kwa sababu yao, akisema: ‘Msiwaguse watiwa-mafuta wangu, wala msiwatendee manabii wangu lolote lililo baya.’”—Zab. 105:14, 15.

“Sitakuacha”

6. Isaka alimwambia Yakobo afanye nini, na huenda Yakobo alihisije?

6 Yakobo, mjukuu wa Abrahamu alikuwa kati ya manabii hao. Wakati ulipofika wa Yakobo kuoa, Isaka baba yake alimwambia hivi: “Usichukue mke kutoka kwa binti za Kanaani. Ondoka, uende mpaka Padan-aramu kwa nyumba ya Bethueli baba ya mama yako na kutoka huko ujichukulie mke kati ya binti za Labani.” (Mwa. 28:1, 2) Yakobo alimtii mara moja Isaka. Yakobo aliacha maisha salama ya familia yake huko Kanaani akasafiri, huenda peke yake, maelfu ya kilomita hadi Harani. (Mwa. 28:10) Huenda alijiuliza hivi: ‘Nitakaa huko kwa muda gani? Je, mjomba atanikaribisha kwa uchangamfu na kunipa mke anayemwogopa Mungu?’ Ikiwa Yakobo alihangaishwa na mambo hayo, bila shaka wasiwasi huo uliisha alipofika Luzi, kilomita 100 hivi kutoka Beer-sheba. Ni nini kilichotokea huko Luzi?

7. Kupitia ndoto, Mungu alimhakikishia nini Yakobo?

 7 Huko Luzi, Yehova alimtokea Yakobo katika ndoto na kumwambia hivi: “Tazama, mimi nipo pamoja nawe, nami nitakutunza katika njia yote unayoenda, nami nitakurudisha kwenye nchi hii, kwa sababu sitakuacha mpaka niwe kwa kweli nimefanya hayo ambayo nimekuambia.” (Mwa. 28:15) Bila shaka maneno hayo ya fadhili yalimpa Yakobo uhakika na kumfariji sana! Je, unaweza kuwazia akiendelea na safari yake, akiwa na hamu ya kuona jinsi ambavyo Mungu angetimiza ahadi Yake? Ikiwa umeondoka nyumbani, labda ili kutumikia katika nchi ya kigeni, huenda unaelewa hisia alizokuwa nazo Yakobo. Hata hivyo, bila shaka umejionea jinsi Yehova anavyokujali.

8, 9. Yehova alithibitika jinsi gani kuwa “makao halisi” kwa Yakobo, na tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

8 Yakobo alipofika Harani, Labani, mjomba wake alimkaribisha kwa uchangamfu na baadaye akampa Lea na Raheli wawe wake zake. Hata hivyo, baadaye Labani alijaribu kumnyanyasa Yakobo kwa kubadili mshahara wake mara kumi! (Mwa. 31:41, 42) Ingawa hivyo, Yakobo alivumilia ukosefu huo wa haki, akiwa na hakika kwamba Yehova angeendelea kumtunza, na kwa kweli alimtunza! Mungu alipomwambia Yakobo arudi Kanaani, mzee huyo wa ukoo alikuwa na “makundi makubwa na wajakazi na watumishi wanaume na ngamia na punda.” (Mwa. 30:43) Yakobo alisali hivi akimshukuru sana Mungu: “Mimi sistahili fadhili zote zenye upendo na uaminifu wote ambao umemwonyesha mtumishi wako, kwa maana nilivuka huu mto Yordani nikiwa na fimbo yangu tu na sasa nimekuwa kambi mbili.”—Mwa. 32:10.

9 Naam, sala hii ya Musa ya kutafakari ilikuwa ya kweli: “Ee Yehova, wewe mwenyewe umekuwa makao yetu halisi kwa kizazi baada ya kizazi”! (Zab. 90:1) Maneno hayo yanatimia leo pia, kwa kuwa Yehova, ambaye “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli,” anaendelea kuwa makao mazuri na salama kwa washikamanifu wake. (Yak. 1:17) Acheni tuchunguze jinsi anavyofanya hivyo.

YEHOVA NI ‘MAKAO YETU HALISI’ LEO

10. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anaendelea kuwa makao salama kwa watumishi wake?

10 Wazia jambo hili: Unatoa ushahidi kortini kuhusu kundi fulani kubwa la wahalifu duniani. Kiongozi wa kundi hilo ni mjanja, ana nguvu, ni muuaji na mwongo kupindukia. Utahisije baada ya kutoka kortini? Je, utahisi ukiwa salama? Bila shaka la! Kwa kweli, utakuwa na sababu nzuri ya kuomba ulindwe. Mfano huo unaonyesha hali ya watumishi wa Yehova, wanaomtetea Yehova kwa ujasiri na kufunua bila woga uwongo wa adui mkuu wa Mungu, Shetani ambaye ni mkatili! (Soma Ufunuo 12:17.) Lakini je, Shetani amefaulu kuwanyamazisha watu wa Mungu? Hapana! Kwa kweli, tunaendelea kusitawi kiroho, na uhakika huo unadhihirisha jambo moja tu: Yehova bado ni ngome yetu, ‘makao yetu halisi,’ hasa katika siku hizi za mwisho. (Soma Isaya 54:14, 17.) Ingawa jambo hilo ni kweli, Yehova hawezi kuwa makao yetu halisi ikiwa tutamruhusu Shetani atushawishi kuondoka katika makao yetu.

Malaika wa Mungu huwategemeza na kuwalinda watumishi wake

11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na wazee wa ukoo?

11 Acheni tujifunze jambo lingine kutokana na wazee wa ukoo. Ingawa waliishi katika nchi ya Kanaani, walijitenga na watu wa nchi hiyo kwa sababu walichukia maadili yao mapotovu na maovu. (Mwa. 27:46) Wanaume hao waliongozwa na kanuni na hawakuhitaji orodha ndefu ya mambo waliyopaswa kufanya au kutofanya. Mambo waliyojua kumhusu Yehova na utu wake yaliwatosha. Kwa sababu alikuwa makao yao, hawakutaka kuukaribia sana  ulimwengu. Badala yake, walikaa mbali kabisa iwezekanavyo na ulimwengu. Walituwekea mfano mzuri kama nini! Je, unajitahidi kuwaiga wazee hao wa ukoo waaminifu unapochagua marafiki au vitumbuizo? Inasikitisha kwamba watu fulani katika kutaniko la Kikristo wanaonyesha kwamba wanafurahia mambo fulani katika ulimwengu wa Shetani. Ikiwa unayafurahia, hata kama ni kwa kadiri ndogo tu, sali kuhusu jambo hilo. Kumbuka kwamba ulimwengu huu ni wa Shetani. Ulimwengu unadhihirisha roho yake ya ubinafsi na hauna huruma.—2 Kor. 4:4; Efe. 2:1, 2.

12. (a) Yehova huwaandaliaje watu wa nyumba yake ya kiroho? (b) Unahisije kuhusu maandalizi hayo?

12 Ili tupinge mbinu za Shetani, ni lazima tutumie kikamili maandalizi ya kiroho ambayo Yehova huwapa watu wa nyumba yake ya imani, wale wanaomfanya awe makao yao. Maandalizi hayo yanatia ndani mikutano ya Kikristo, ibada ya familia, na “zawadi katika wanadamu,” yaani, wachungaji waliowekwa rasmi na Mungu ili kutufariji na kututegemeza tunapokabiliana na matatizo maishani. (Efe. 4:8-12) Ndugu George Gangas, aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza kwa miaka mingi aliandika hivi: “Ninapokuwa miongoni mwa [watu wa Mungu] ninajihisi nikiwa nimestarehe na familia yangu katika paradiso ya kiroho.” Je unahisi vivyo hivyo?

13. Tunajifunza jambo gani muhimu kwenye Waebrania 11:13?

13 Sifa nyingine ya wazee wa ukoo tunayoweza kuiga ni utayari wao wa kuwa tofauti na majirani zao. Kama ilivyotajwa katika  fungu la kwanza, ‘walitangaza hadharani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika nchi.’ (Ebr. 11:13) Je, umeazimia kuwa tofauti na ulimwengu unaokuzunguka? Kwa kweli, si rahisi sikuzote kuwa tofauti na ulimwengu. Lakini, Mungu na Wakristo wenzako wanaweza kukusaidia kuwa tofauti. Kumbuka kwamba huhitaji kukabiliana na hali hiyo ukiwa peke yako. Wote wanaotaka kumtumikia Yehova ni lazima wapigane vita! (Efe. 6:12) Lakini, tunaweza kushinda vita hivyo tukimtegemea Yehova na kumfanya kuwa makao yetu salama.

14. Watumishi wa Yehova walingojea “jiji” gani?

14 Jambo lingine muhimu ni hili: Mwige Abrahamu kwa kukazia macho tuzo. (2 Kor. 4:18) Mtume Paulo aliandika kwamba Abrahamu “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Ebr. 11:10) “Jiji” hilo ni Ufalme wa Kimasihi. Bila shaka, Abrahamu alihitaji kungojea “jiji” hilo. Kwa njia fulani, sisi hatulingojei.  Ufalme huo unatawala sasa mbinguni. Isitoshe, kuna mambo mengi yanayothibitisha kwamba hivi karibuni utaitawala dunia. Je, Ufalme huo ni halisi kwako? Je, Ufalme unaongoza mtazamo wako kuelekea maisha, maoni yako kuhusu ulimwengu huu, na mambo unayotanguliza maishani?—Soma 2 Petro 3:11, 12.

‘MAKAO YETU HALISI’ KADIRI MWISHO UNAVYOKARIBIA

15. Itakuwaje kwa wale wanaotegemea ulimwengu huu?

15 Ulimwengu wa Shetani unapokaribia mwisho wake, “maumivu ya taabu” yatakuwa mabaya zaidi. (Mt. 24:7, 8) Bila shaka mambo yatazidi kuwa mabaya wakati wa dhiki kuu. Majengo yataporomoka na watu watahofia uhai wao. (Hab. 3:16, 17) Kwa sababu ya kukata tamaa, watakimbilia kwa njia ya mfano “katika mapango na katika miamba ya milima.” (Ufu. 6:15-17) Hata hivyo, hawatalindwa kamwe na mapango halisi au matengenezo ya kisiasa na ya kibiashara yaliyo kama milima.

16. Tunapaswa kulionaje kutaniko la Kikristo, na kwa nini?

16 Hata hivyo, watu wa Yehova wataendelea kufurahia usalama katika ‘makao yao halisi,’ Yehova Mungu. Kama nabii Habakuki, ‘watafurahi katika Yehova mwenyewe. Watakuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wao.’ (Hab. 3:18) Ni katika njia zipi Yehova atakuwa “makao halisi” wakati huo wa msukosuko? Tutahitaji kungojea ili tuone jambo hilo. Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika huu: Kama tu Waisraeli waliokuwa wakitoka Misri, “umati mkubwa” utaendelea kufuata utaratibu na kuwa macho kutii mwongozo kutoka kwa Mungu. (Ufu. 7:9; soma Kutoka 13:18.) Mwongozo huo utatolewa kwa njia ya kitheokrasi, labda kupitia kutaniko. Kwa kweli, inaonekana kwamba maelfu ya makutaniko ulimwenguni pote ni kama ‘vyumba vya ndani’ vinavyoandaa ulinzi ambavyo vilitabiriwa katika Isaya 26:20. (Soma.) Je, unathamini mikutano ya kutaniko? Je, unatii haraka mwongozo ambao Yehova anatoa kupitia kutaniko?—Ebr. 13:17.

17. Ni katika maana gani Yehova ni “makao halisi” hata kwa watumishi wake washikamanifu waliokufa?

17 Hata wale ambao huenda wakafa wakiwa waaminifu kabla ya dhiki kuu kuanza, wataendelea kuwa salama katika ‘makao yao halisi,’ yaani, Yehova. Jinsi gani? Muda mrefu baada ya wazee wa ukoo kufa, Yehova alimwambia Musa hivi: “Mimi ni Mungu wa . . . Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.” (Kut. 3:6) Baada ya kunukuu maneno hayo, Yesu aliongezea hivi: “Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:38) Naam, watumishi washikamanifu wa Yehova waliokufa wakiwa waaminifu wangali hai machoni pake; kwa hakika watafufuliwa.—Mhu. 7:1.

18. Katika ulimwengu mpya, Yehova atakuwaje “makao halisi” kwa watu wake katika njia ya pekee?

18 Katika ulimwengu mpya ulio karibu sana, Yehova atakuwa “makao halisi” kwa watu wake katika njia nyingine. Andiko la Ufunuo 21:3 linasema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao.” Mwanzoni, Yehova atakaa na raia wake walio duniani kupitia mwakilishi wake Kristo Yesu. Mwishoni mwa ile miaka elfu, Yesu atamrudishia Baba yake Ufalme, baada ya kutimiza kikamili kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. (1 Kor. 15:28) Baadaye, wanadamu wakamilifu hawatahitaji tena kusali kupitia Yesu; Yehova atakuwa pamoja nao. Tuna tumaini zuri ajabu la wakati ujao! Kwa sasa, acheni tujitahidi kuwaiga watu waaminifu wa kale kwa kumfanya Yehova kuwa ‘makao yetu halisi.’

^ fu. 2 Biblia ya Contemporary English Version inasema hivi katika Zaburi 90:1: “Bwana wetu, katika vizazi vyote umekuwa nyumba yetu.”