Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni muhimu kuzungumzia mambo mapema na waziwazi

Mpendwa Wako Anapokuwa na Ugonjwa Usiotibika

Mpendwa Wako Anapokuwa na Ugonjwa Usiotibika

DOREEN alishtuka sana baada ya mume wake, Wesley, aliyekuwa na umri wa miaka 54 tu, kugunduliwa kuwa na uvimbe hatari sana kwenye ubongo. * Madaktari walisema kwamba hakuwa na muda mrefu wa kuishi. Doreen anasema hivi: “Sikuamini nilichosikia. Mshtuko niliopata uliniathiri kwa majuma kadhaa. Nilihisi kana kwamba ni watu wengine waliokuwa wakipitia hali hiyo, na si sisi. Sikuwa tayari hata kidogo.”

Kwa kusikitisha, watu wengi huhisi kama Doreen mpendwa wao anapogunduliwa kuwa na ugonjwa usiotibika. Ugonjwa wa aina hiyo unaweza kumpata yeyote, wakati wowote. Inapendeza kwamba wengi huwa tayari kuwatunza wapendwa wao ambao wana ugonjwa usiotibika. Ingawa hivyo, kazi hiyo si rahisi. Washiriki wa familia wanaweza kufanya nini ili kumtunza na kumfariji mpendwa wao ambaye ana ugonjwa usiotibika? Wale wanaomtunza mgonjwa wanaweza kukabilianaje na hisia mbalimbali ambazo huenda wakawa nazo katika kipindi hicho chote? Wanapaswa kutarajia nini kadiri kifo cha mgonjwa kinavyokaribia? Kabla ya kujibu maswali hayo, acheni kwanza tuone kwa nini ni vigumu sana leo kumtunza mtu mwenye ugonjwa usiotibika.

MAENDELEO YANAYOLETA UTATA

Sayansi ya tiba imebadili mambo kadhaa kuhusiana na vifo vya watu. Miaka 100 hivi iliyopita, maisha ya watu yalikuwa mafupi ukilinganisha na sasa, hata katika nchi zilizoendelea. Watu walikufa haraka kutokana na magonjwa ya kuambukiza au aksidenti. Huduma za matibabu hazikupatikana kwa urahisi. Vilevile, wagonjwa wengi walihudumiwa na familia zao na kufia nyumbani.

Leo, kwa sababu ya maendeleo ya tiba, matabibu wanajitahidi sana kupambana na magonjwa ili kurefusha maisha ya watu. Siku hizi mtu anaweza kuishi muda mrefu na ugonjwa ambao kipindi cha nyuma huenda ungesababisha kifo cha mapema sana. Licha ya hilo, huenda bado ikashindikana kuutibu kabisa ugonjwa. Mara nyingi wagonjwa hufikia hatua ya kuwa dhaifu sana kiasi cha kushindwa kujihudumia. Kuwatunza wagonjwa wa aina hiyo ni kazi yenye changamoto na inahitaji kujitoa sana.

Pia, siku hizi watu wengi zaidi wanafia hospitalini na si nyumbani kama zamani. Watu wengi leo hawajui mambo yanayotokea mtu anapokaribia kufa, na ni wachache sana ambao wamewahi kushuhudia mtu akifa. Hivyo, huenda woga ukamfanya mtu ashindwe kabisa kumhudumia mshiriki wa familia yake ambaye ni mgonjwa. Ni nini kinachoweza kusaidia?

FANYA MIPANGO MAPEMA

Kama ilivyokuwa katika kisa cha Doreen, watu wengi huchanganyikiwa mpendwa wao anapogunduliwa kuwa na ugonjwa usiotibika. Licha ya wasiwasi mwingi, woga, na huzuni, unaweza kufanya nini ili ujiandae na mambo utakayokabili? Mtumishi fulani mwaminifu wa Mungu alisali hivi: “Utuonyeshe jinsi ya kuzihesabu siku zetu hivi kwamba tupate kuuingiza moyo wa hekima.” (Zaburi 90:12) Naam, sali kwa bidii kwa Yehova Mungu akuonyeshe jinsi ya ‘kuzihesabu siku zako’ kwa hekima ili utumie siku zilizobaki pamoja na mpendwa wako kwa njia bora zaidi.

Ili kutimiza hilo, unahitaji kufanya mipango mizuri. Ikiwa bado mpendwa wako anaweza kuwasiliana nanyi, na yupo tayari kuzungumzia kuhusu mtu atakayemfanyia maamuzi atakapokuwa hajiwezi, basi ni vizuri kufanya hivyo. Mazungumzo ya wazi kuhusu ikiwa angependa uhai wake uendelezwe kwa mashine au la, ahudumiwe hospitalini, au apewe aina fulani ya matibabu, yatasaidia kupunguza hali ya kutoelewana na kufanya wale wanaomtunza wasihisi hatia kwa maamuzi watakayohitaji kufanya kwa niaba yake. Kuzungumzia mambo waziwazi na mapema kutafanya washiriki wa familia wakazie fikira kazi ya kumtunza mgonjwa. Biblia inasema: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.”​—⁠Methali 15:⁠22.

JINSI YA KUMSAIDIA MGONJWA

Daraka kuu la yule anayemtunza mgonjwa ni kumfariji. Mtu anayekaribia kufa anapaswa kuhakikishiwa kwamba anapendwa na hayuko peke yake. Unaweza kufanyaje hivyo? Msomee vitabu au mwimbie nyimbo ambazo zitamjenga na kumfurahisha. Wagonjwa wengi huhisi faraja mshiriki wao wa familia anapowashika mkono na kuzungumza nao kwa wororo.

Ni vizuri kuwatambulisha wageni wanaokuja kumtembelea. Ripoti moja inaeleza hivi: “Inasemekana kwamba uwezo wa kusikia ndio huwa wa mwisho kupotea kati ya hisi zote tano. Inawezekana [mgonjwa] akawa bado anasikia vizuri sana ingawa anaonekana amelala, kwa hiyo usiseme jambo lolote ambalo hungesema ikiwa angekuwa macho.”

Ikiwezekana, sali pamoja naye. Biblia inasema kwamba wakati fulani mtume Paulo na wenzake walikabili hali ngumu na hata wakaanza kuhofia uhai wao. Waliomba msaada gani? Paulo aliwaambia hivi rafiki zake: “Ninyi pia mnaweza kushiriki kusaidia kwa dua yenu kwa ajili yetu.” (2 Wakorintho 1:​8-​11) Sala ya kutoka moyoni ni muhimu sana wakati wa mkazo au ugonjwa hatari.

KUBALI UKWELI WA MAMBO

Wazo tu la kufiwa na mpendwa huleta mkazo. Hiyo haishangazi kwa sababu kifo si kitu cha kawaida. Hatukuumbwa tukione kifo kuwa sehemu ya maisha. (Waroma 5:​12) Hiyo ndiyo sababu Neno la Mungu hukiita “adui.” (1 Wakorintho 15:26) Kwa hiyo, ni kawaida na inaeleweka kabisa ikiwa mtu hataki kufikiria kuhusu kifo cha mpendwa wake.

Ingawa hivyo, kufikiria mambo ambayo huenda yakatokea kutasaidia kupunguza woga wa washiriki wa familia na kuwasaidia wakazie fikira jinsi wanavyoweza kufanya mambo yawe shwari kadiri iwezekanavyo. Baadhi ya mambo ambayo huenda yakatokea yameorodheshwa kwenye sanduku “ Majuma ya Mwisho ya Mgonjwa.” Bila shaka, si lazima kila mgonjwa apitie mambo hayo yote au kwa mfuatano uleule. Hata hivyo, wagonjwa wengi hupitia hali kadhaa kati ya zile zilizoorodheshwa.

Baada ya kifo cha mpendwa, litakuwa jambo la hekima kuwasiliana na rafiki wa karibu ambaye alikuwa ameahidi kukusaidia. Ni muhimu wale waliokuwa wakimtunza mgonjwa pamoja na washiriki wa familia wahakikishiwe kwamba mateso ya mpendwa wao yameisha. Kwa upendo, Muumba wa wanadamu anatuhakikishia kwamba “wafu, hawajui lolote kamwe.”​—⁠Mhubiri 9:⁠5.

MTUNZAJI MKUU

Inafaa tujifunze kukubali msaada wowote tunaopata

Ni muhimu sana kumtegemea Mungu, si tu wakati mpendwa wetu anapokuwa mgonjwa, bali hata tunapokuwa na huzuni baada ya kifo chake. Anaweza kutufariji kupitia maneno na matendo ya watu wengine. Doreen alisema hivi: “Nilijifunza kwamba sipaswi kukataa msaada wa mtu yeyote. Kusema kweli, tulisaidiwa kwa kiasi kikubwa sana. Mimi na mume wangu hatukuwa na shaka kwamba Yehova alikuwa akituambia, ‘Nipo hapa ili kuwasaidia kukabiliana na hali hii.’ Kamwe sitasahau jambo hilo.”

Naam, Yehova Mungu ndiye Mtunzaji mkuu. Akiwa Muumba wetu, anaelewa kikamili maumivu na majonzi tuliyo nayo. Anaweza na ana hamu ya kutoa msaada na kitia moyo kinachohitajika. Jambo bora zaidi ni kwamba, ameahidi kuwa hivi karibuni atakiondoa kifo kabisa na kufufua mamilioni ya watu ambao wapo kwenye kumbukumbu yake. (Yohana 5:​28, 29; Ufunuo 21:​3, 4) Kisha, wote watasema maneno kama haya ya mtume Paulo: “Kifo, uko wapi ushindi wako? Kifo, uko wapi mchomo wako?”​—⁠1 Wakorintho 15:⁠55.

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa.