Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUFAIDIKA ZAIDI UNAPOSOMA BIBLIA

Ni Nini Kitakachofanya Nifurahie Kusoma Biblia?

Ni Nini Kitakachofanya Nifurahie Kusoma Biblia?

Je, kusoma Biblia kunakuchosha au kunakufurahisha? Yote hayo yanategemea njia unayotumia katika usomaji wako. Acheni tuchunguze mambo unayoweza kufanya ili uongeze hamu ya kusoma na ufurahie zaidi.

Chagua tafsiri sahihi na yenye lugha inayoeleweka. Ikiwa unasoma habari fulani yenye maneno magumu au yasiyoeleweka, ni wazi kwamba hutafurahia usomaji huo. Kwa hiyo, chagua Biblia yenye lugha rahisi kueleweka ambayo itagusa moyo wako. Wakati huohuo, Biblia hiyo inapaswa kuwa tafsiri sahihi na inayotegemeka. *

Tumia teknolojia ya kisasa. Leo, Biblia inapatikana katika nakala zilizochapishwa, na pia katika mfumo wa vifaa vya elektroniki. Baadhi ya Biblia zinaweza kusomwa mtandaoni au kupakuliwa na kusomwa kupitia kompyuta, tablet, au simu. Baadhi ya programu za elektroniki zina mfumo unaoweza kukusaidia kulinganisha mistari ya Biblia inayohusu jambo unalosoma au hata kulinganisha tafsiri kadhaa. Ikiwa unapenda kusikiliza badala ya kusoma, Biblia pia inapatikana katika rekodi za kusikiliza kwa baadhi ya lugha. Wengi hupenda kusikiliza wanapotumia usafiri wa umma, wanapofua nguo, au wanapofanya kazi nyingine yoyote inayowaruhusu kusikiliza. Kwa nini usijaribu njia inayokufaa?

Tumia vifaa vya kujifunzia Biblia. Vifaa vya kujifunzia Biblia vinaweza kukusaidia ufaidike zaidi na usomaji wako. Kuna ramani za nchi zinazotajwa katika Biblia, ambazo zitakusaidia kujua mahali ambapo jambo unalosoma lilitukia na hivyo kukuwezesha kuwazia matukio. Makala mbalimbali, kama zile zinazopatikana kwenye gazeti hili au sehemu yenye kichwa “Mafundisho ya Biblia” iliyo kwenye tovuti ya jw.org/sw, zinaweza kukusaidia kuelewa maana ya mistari mbalimbali ya Biblia.

Tumia njia mbalimbali kusoma Biblia. Ikiwa kusoma Biblia kuanzia mwanzo hadi mwisho kunaoneka kuwa kunachosha, jaribu kusoma sehemu fulani za Biblia ambazo zinakuvutia. Pia, unaweza kutumia njia ya kusoma habari zinazohusu mtu mmoja-mmoja kati ya wale wanaotajwa katika Biblia. Mfano mmoja wa jinsi ya kufanya hivyo umeonyeshwa katika sanduku lenye kichwa, “ Chimba Katika Biblia kwa Kuwajua Watu Wanaotajwa Humo.” Njia nyingine ni kusoma habari fulani hususa, moja baada ya nyingine, au kusoma kulingana na mfuatano wa matukio. Unaonaje ukitumia njia moja kati ya hizo?

^ fu. 4 Wengi wameona kwamba Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni sahihi, inategemeka, na ni rahisi kusoma. Biblia hiyo inachapishwa na Mashahidi wa Yehova, na inapatikana katika lugha zaidi ya 130. Unaweza kupakua nakala yako katika tovuti ya jw.org/sw au kupakua programu ya JW Library. Au wasiliana na Mashahidi wa Yehova wakuletee nakala ya Biblia.