Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Wanyama

Wanyama

Kwa njia moja au nyingine, wanyama wanahusika katika maisha yetu. Je, tunawajibika kutokana na jinsi tunavyowatendea?

Wanadamu wanapaswa kuwatendea wanyama jinsi gani?

WATU HUSEMA NINI?

Baadhi ya watu wanaamini kwamba wanadamu wanaweza kuwatumia wanyama kwa njia yoyote wapendayo. Wengine wanahisi kwamba wanyama wanapaswa kutendewa kama wanadamu wanavyotendewa.

  • Mtetezi maarufu wa haki za wanyama alisema kwamba wanyama wana “haki ya msingi ya kutoonwa kuwa chanzo cha uchumi au biashara. Tunapaswa kuacha kuwaona wanyama kuwa mali.”

  • Katika kisa ambacho wengi walidai kwamba ni kupita kiasi, bilionea Leona Helmsley, alimwachia mbwa wake urithi wa dola za Marekani milioni 12, na kuagiza kwamba mbwa huyo akifa, azikwe kando ya kaburi lake.

Jambo la kufikiria: Unahisi wanyama wanapaswa kutendewa jinsi gani?

BIBLIA INASEMA NINI?

Muumba wa uhai, Yehova Mungu, aliwaagiza wanadamu ‘watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.’ (Mwanzo 1:28) Hivyo, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba, Mungu huona wanadamu kuwa bora kuliko wanyama.

Mkataa huo unathibitishwa na maneno ya pekee yaliyo katika mstari unaotangulia andiko lililonukuliwa hapo juu. Biblia inasema hivi: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.”—Mwanzo 1:27.

Kwa kuwa tuliumbwa “kwa mfano wa Mungu,” tuna uwezo wa kuonyesha sifa zake kama vile hekima, haki, na upendo. Wanadamu wana uwezo wa asili wa kufuata kanuni na kutaka kumjua Mungu. Wanyama hawana uwezo huo kwa sababu hawakuumbwa kwa “mfano wa Mungu.” Wao si sawa na wanadamu nao hawakuumbwa watendewe kama wanadamu.

Je, hilo linamaanisha kwamba wanadamu wana haki ya kuwatendea wanyama isivyofaa? Hapana.

“Siku sita utafanya kazi yako; lakini siku ya saba utaacha, ili ng’ombe-dume wako na punda wako wapate kupumzika.” Kutoka 23:12.

Je, ni kosa kuua wanyama?

WATU HUSEMA NINI?

Wawindaji na wavuvi fulani huua wanyama ili kujifurahisha na kusisimuka kutokana na hilo. Huenda wengine wakakubaliana na mwandishi Mrusi, Leo Tolstoy, aliyeandika kwamba ni “upotovu wa maadili,” kuua na kula wanyama.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu ameruhusu wanadamu kuua wanyama ili kujilinda au kupata mavazi. (Kutoka 21:28; Marko 1:6) Biblia inasema pia kwamba wanadamu wanaweza kuua wanyama ili kupata chakula. Andiko la Mwanzo 9:3 linasema hivi: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu.” Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kuvua samaki waliotumia baadaye kama chakula.—Yohana 21:4-13.

Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Mungu ‘humchukia mtu yeyote anayependa jeuri.’ (Zaburi 11:5) Hilo linamaanisha kwamba Mungu hataki tuwadhuru au kuwaua wanyama kwa ajili ya mchezo au kujifurahisha tu.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu anathamini sana uhai wa wanyama.

  • Biblia inasema kwamba wakati wa uumbaji, “Mungu akafanya mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake na mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake na kila mnyama anayetembea wa nchi kulingana na aina yake. Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema.”Mwanzo 1:25.

  • Biblia inasema kwamba Yehova, “anawapa wanyama chakula chao.” (Zaburi 147:9) Mungu ameumba mifumo ya ekolojia inayotoa chakula cha kutosha na malazi kwa ajili ya wanyama.

  • Mfalme Daudi wa Israeli alisali hivi: “Wewe huokoa mwanadamu na mnyama, Ee Yehova.” (Zaburi 36:6) Kwa mfano, kabla ya kuangamiza watu waovu wakati wa Gharika, Yehova alihifadhi hai watu wanane na wanyama wa kila aina.—Mwanzo 6:19.

Ni wazi kwamba Yehova anapendezwa na wanyama na anatazamia wanadamu wawatendee wanyama kulingana na maoni yake.

“Mwadilifu anatunza nafsi ya mnyama wake wa kufugwa.” Methali 12:10.