Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Kwa Nini Watoto Hawana Nidhamu?

Kwa Nini Watoto Hawana Nidhamu?

Katika miaka ya hivi karibuni, maisha ya familia katika nchi za Magharibi yamebadilika sana. Zamani watoto walitii mwongozo wa wazazi wao. Leo, katika familia nyingi inaonekana kwamba watoto wanawaongoza wazazi wao. Kwa mfano, fikiria hali zifuatazo zinazoonyesha jinsi hali ilivyo.

  • Mvulana wa miaka minne yuko dukani pamoja na mama yake, na anachukua kigari cha kuchezea. Mama yake anamkataza kwa kusema: “Si una vifaa vya kutosha vya kuchezea?” Hata hivyo, anatambua kwamba hakupaswa kumwuliza swali hilo. Mvulana anajibu huku akilia “ninataka hiki!” Akijua kwamba mwana wake ana kawaida ya kulipuka kwa hasira, mama huyo anamruhusu achukue.

  • Msichana mwenye umri wa miaka mitano anakatiza mazungumzo kati ya baba yake na mtu fulani. Anamwambia hivi: “Nimechoka kusubiri, nataka kwenda nyumbani!” Hata kabla baba yake hajamaliza alichokuwa akisema, anainama na kumweleza binti yake hivi kwa sauti ya upole: “Binti yangu mpendwa, subiri tu kwa dakika chache, sawa?”

  • James mwenye umri wa miaka 12 ameshtakiwa tena kuwa amemfokea mwalimu wake. Baba ya James amemkasirikia sana mwalimu wa James. “Mwalimu huyo amezoea kukusumbua,” anamwambia James. “Nitamshtaki kwenye kamati ya shule!”

Hali hizo ni za kuwaziwa tu, ingawa kwa kweli zinaweza kutokea kihalisi. Zinaonyesha tatizo kubwa katika familia ambazo wazazi huruhusu watoto wajiendeshe bila adabu, hukubaliana na chochote wanachotaka, na hata huwatetea wanapojiendesha kwa njia isiyofaa. Kitabu The Narcissism Epidemic, kinasema hivi: “Limekuwa jambo la kawaida kuona wazazi wakikosa kutumia mamlaka yao kuelekea watoto wao. Miaka michache iliyopita, watoto walijua ni nani alikuwa mwenye mamlaka, nao walitii.”

Ni kweli kwamba wazazi wengi hujitahidi kufundisha watoto wao maadili yanayofaa kwa kuwawekea mfano mzuri na kwa kuwarekebisha kwa njia ya upendo wanapokosea. Hata hivyo, kulingana na kitabu kilichonukuliwa hapo mwanzoni, wazazi wanaotambua faida za kufanya hivyo, wanaonwa “kana kwamba wanapinga tamaduni za kwao.”

Kwa nini mambo yamebadilika hivyo? Kwa nini watoto wamekosa adabu?

Wazazi Walegeza Mamlaka Yao

Inasemekana kwamba wazazi walianza kulegeza mamlaka yao katika miaka ya 1960, wakati watu waliodai kuwa wataalamu walipopendekeza kwamba wazazi hawapaswi kuwawekea watoto wao sheria. Walisema hivi: ‘Mnapaswa kuwa marafiki, wala si wenye mamlaka. Kusifu ni bora kuliko kutia nidhamu. Badala ya kurekebisha makosa yao, tambua wanapofanya mambo mazuri.’ Hivyo, badala ya kuwa na usawaziko kati ya kupongeza na kurekebisha, inaonekana wataalamu walihisi kwamba hisia za watoto zingeumizwa baada ya kutiwa nidhamu na kuwafanya wawachukie wazazi wao watakapokuwa watu wazima.

Baada ya muda, wataalamu walianza kukazia sana umuhimu wa kujiamini. Ni kana kwamba waligundua siri hii mpya ya kuwa mzazi bora: Wasaidie watoto wako wajione kuwa wa maana. Ni kweli kwamba ni muhimu kusaidia watoto wajiamini. Hata hivyo, kampeni hiyo ilipita mipaka kwa kuwa wataalamu waliwaambia wazazi hivi: ‘Msitumie maneno kama vile hapana na vibaya. Endeleeni kuwaambia watoto wenu kwamba wao ni wa pekee na wanaweza kufanya lolote watakalo.’ Ni kana kwamba jambo muhimu zaidi lilikuwa kuwafanya wahisi vizuri badala ya kuwasaidia wawe na tabia nzuri.

Kampeni ya kuwafanya watoto wajihisi kuwa wa maana imewafanya wahisi kwamba watu wengine wanapaswa kuwatumikia

Matokeo ni kwamba, watu fulani wanasema kampeni hiyo iliwafanya watoto wahisi kwamba watu wote wanapaswa kuwatumikia. Kwa sababu ya mtazamo huo, kitabu Generation Me, kinasema kwamba vijana wengi “hawako tayari kukabiliana na matatizo halisi maishani kama vile uchambuzi watakaopata na pindi za kutofanikiwa maishani.” Baba mmoja ananukuliwa katika kitabu hicho akisema hivi: “Ukiwa kazini, hakuna mtu atakayejali ikiwa unajihisi kuwa mtu wa maana. . . . Ikiwa utaandika ripoti mbaya, mwajiri wako hatasema, ‘Ninapendezwa sana na rangi ya karatasi uliyotumia kuandika ripoti hii.’ Kulea watoto kwa njia hii kutawaletea madhara makubwa baadaye.”

Maoni Yanayobadilika-Badilika

Kwa miaka mingi, watu wamekuwa wakibadili maoni yao kuhusu mbinu za kulea watoto. Mwalimu Ronald G. Morrish, aliandika hivi: “Nidhamu hubadilika kila mara kutokana na mabadiliko katika jamii.” * Ni rahisi sana kwa wazazi ‘kurushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho,’ kama vile Biblia inavyosema.—Waefeso 4:14.

Ni wazi kwamba mtazamo uliopo wa kutotia nidhamu watoto umekuwa na matokeo mabaya. Hali hiyo imewafanya wazazi kulegeza mamlaka yao na pia kuwaacha watoto bila mwongozo wanaohitaji ili wafanye maamuzi mazuri na kujiamini kikweli maishani.

Je, kuna njia bora zaidi?

^ fu. 15 Italiki ni zetu; kutoka katika kitabu Secrets of Discipline: 12 Keys for Raising Responsible Children.