Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe “Huwa Karamu Siku Zote”?

Je, Wewe “Huwa Karamu Siku Zote”?

“Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.”Methali 15:15.

MANENO hayo yanamaanisha nini? Yanarejelea hali ya akili na kihisia ya mtu. “Mwenye kuteseka” hufikiria sana kuhusu mambo mabaya—mtazamo unaofanya siku zake ziwe “mbaya” au zenye kuhuzunisha. Tofauti na hilo, mtu “aliye mchangamfu moyoni” hujaribu kukazia fikira mambo mazuri—mtazamo unaochochea shangwe ya moyoni, ukimfanya awe na “karamu sikuzote.”

Sisi sote tuna matatizo yanayoweza kutunyang’anya furaha yetu kwa kadiri fulani. Hata hivyo, tunaweza kufanya mambo fulani yatakayotusaidia kudumisha shangwe yetu tunapokumbwa na matatizo. Ona Biblia inasema nini.

  • Usiruhusu mahangaiko ya kesho yakulemee leo. Yesu Kristo alisema hivi: “Msiwe na wasiwasi juu ya kesho; kesho inayo yake. Matatizo ya siku moja yanawatosheni kwa siku hiyo.”Mathayo 6:34, Biblia Habari Njema.

  • Jaribu kukazia fikira mambo mazuri yanayokupata. Unaposhuka moyo, kwa nini usijikumbushe mambo hayo mazuri na kutafakari kuyahusu? Pia, usikazie fikira makosa au mambo mabaya uliyofanya zamani. Jifunze kutokana nayo, na usonge mbele. Uwe kama dereva ambaye mara kwa mara hutumia kioo cha kuangalia nyuma lakini hakazii fikira kioo hicho. Pia, kumbuka kwamba kwa “[Mungu] kuna msamaha wa kweli.”Zaburi 130:4.

  • Unapolemewa na mahangaiko, mweleze mtu anayeweza kukutia moyo. “Hangaiko” huufanya moyo wetu “uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie,” inasema Methali 12:25. “Neno [hilo] jema” linaweza kutoka kwa mtu wa familia au rafiki anayetumainiwa—mtu ambaye hachambui-chambui au hana mtazamo mbaya bali “anapenda nyakati zote.”Methali 17:17.

Maneno yenye hekima yanayopatikana katika Biblia yamewasaidia wengi kupata shangwe zaidi maishani mwao, hata wanapokabili magumu. Maneno hayo yenye thamani na yakusaidie wewe pia.