Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Maadili Yanayoboresha Maisha

Maadili Yanayoboresha Maisha

Christina hakuamini macho yake! Alikuwa amepata mfuko mweusi wa plastiki uliokuwa na pesa nyingi sana—kiasi cha mshahara wake wa zaidi ya miaka 20! Na alijua ni nani aliyekuwa amepoteza mfuko huo. Angefanya nini? Wewe ungefanya nini? Jibu lako litaonyesha maoni yako kuhusu sifa ya unyoofu.

MAADILI ni nini? Ni kanuni zinazoonwa kuwa nzuri na muhimu. Zinaweza kutia ndani kusamehe, unyoofu, upendo, kuheshimu uhai, na kujizuia. Kwa hiyo, maadili yetu huathiri tabia zetu, mambo tunayotanguliza, mahusiano yetu na wengine, na pia maadili tunayowafundisha watoto wetu. Hata hivyo, ingawa maadili ni muhimu, yanazorota.

KUZOROTA KWA MAADILI

Katika mwaka wa 2008, watafiti nchini Marekani waliwaomba vijana wengi watoe maoni yao kuhusu maadili. David Brooks aliandika hivi katika gazeti The New York Times: “Jambo la kusikitisha ni kwamba vijana hao hawaoni kuwa ni muhimu kufikiria au kuzungumza kuhusu maadili.” Wengi wao walisema kwamba ni vibaya kubaka na kuua, lakini “mbali na mambo hayo, hawakufikiria kuhusu mambo yaliyo sawa na yaliyo mabaya, hata wakati walipokuwa wakizungumzia mambo kama vile kuendesha gari ukiwa mlevi, kuiba mtihani shuleni au kukosa kuwa mwaminifu kwa mwenzi wako.” Kijana mmoja alisema, “Ni nadra sana kwangu kufikiria kuhusu yaliyo sawa na yaliyo makosa.” Wengi wao walikuwa na maoni  haya: ‘Ikiwa unahisi ni sawa kufanya jambo fulani, lifanye. Fuata moyo wako.’ Lakini je, ni jambo la hekima kuwa na maoni hayo?

Ingawa moyo wa mwanadamu unaweza kuonyesha huruma na upendo mwingi, unaweza pia kuwa ‘wenye hila na hatari.’ (Yeremia 17:9) Ukweli huo wenye kusikitisha unaonekana katika tabia za watu ambazo zimebadilika kama Biblia ilivyotabiri zamani za kale. Ilisema hivi: “Katika siku za mwisho . . . watu watakuwa na ubinafsi, wenye tamaa ya fedha, wenye majivuno, wenye kujiona,” na pia watakuwa “watu wasio na upendo moyoni [na] wakali.” Pia, “watachukia chochote kilicho chema” na “watapenda anasa kuliko kumpenda Mungu.”2 Timotheo 3:1-5, Biblia Habari Njema.

Mambo hayo yanayoonekana wazi yanapaswa kutuchochea kuchunguza moyo wetu badala ya kuufuata bila kufikiri! Biblia inasema hivi waziwazi: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga.” (Methali 28:26) Andiko hilo linaonyesha kwamba moyo wetu unapaswa kurekebishwa kwa kutumia kanuni zinazofaa ili utuongoze vizuri. Tunaweza kupata wapi kanuni hizo? Watu wengi huiamini Biblia kwa sababu ni sahihi na inasema mambo waziwazi.

KANUNI ZENYE KUTEGEMEKA!

Kanuni za Biblia zinathibitisha kwamba ziliandikwa kwa ajili ya wanadamu. Fikiria mifano hii michache—sifa ya upendo, fadhili, ukarimu, na unyoofu.

Kuwapenda wengine.

“Ikiwa umejifunza kuwapenda wengine, bila shaka wewe pia utakuwa mwenye furaha,” kinasema kitabu Engineering Happiness—A New Approach for Building a Joyful Life (Kukuza UpendoMbinu Mpya ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha). Ni wazi kwamba sisi wanadamu tunahitaji upendo. Bila upendo, hatuwezi kuwa na furaha ya kweli.

Biblia inasema nini? “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Mwandikaji huyo wa Biblia pia alisema: “Ikiwa . . . sina upendo, mimi si kitu.”1 Wakorintho 13:2.

Upendo unaozungumziwa si wa kimahaba au unaochochewa na hisia; ni upendo unaoongozwa na kanuni. Upendo wa aina hiyo hutuchochea kumsaidia mtu tusiyemfahamu anapokuwa na matatizo bila kutarajia malipo yoyote. Tunasoma hivi kwenye 1 Wakorintho 13:4-7: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, . . . huvumilia mambo yote.”

Upendo huo unapokosekana katika familia, kila mtu huumia, hasa watoto. Mwanamke mmoja anayeitwa Monica aliandika kwamba alipokuwa mtoto alitendewa vibaya kimwili, kihisia, na kingono. Anasema: “Nilihisi sipendwi na sikuwa na tumaini.” Kisha alipokuwa na umri wa miaka 15, alienda kuishi na babu na nyanya yake ambao ni Mashahidi wa Yehova.

Monica anasema hivi: “Miaka hiyo miwili niliyoishi nao, walinifunza jinsi ya kushirikiana, kuwapenda, na kuwajali wengine  ingawa nilikuwa mwenye haya. Walinisaidia kuwa kijana mwenye kuheshimika.” Akiwa sasa anafurahia maisha ya ndoa, Monica pamoja na mume wake na watoto wao watatu huwaonyesha wengine upendo kwa kuwaeleza ujumbe wa Biblia.

Adui asiyeonekana wa upendo ni kufuatilia mali, yaani, wazo la kwamba kuwa na mali nyingi na anasa ndivyo vitu vyenye thamani zaidi. Hata hivyo, utafiti unaonyesha kwamba watu hawahitaji kuwa na pesa nyingi ili wawe na furaha. Kwa kweli, watu ambao hufuatilia mali huenda wakawa wanajinyima furaha na Biblia inaunga mkono wazo hilo. Mhubiri 5:10 inatuambia hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” Biblia pia inasema: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa.”Waebrania 13:5.

Fadhili na ukarimu.

“Je, haingependeza ikiwa ungeweza kwenda tu dukani na kununua furaha ya kudumu?” inasema makala moja iliyoandikwa huko Marekani na kituo cha utafiti kuhusu mahusiano mazuri na hali njema ya kihisia katika Chuo Kikuu cha California, Berkeley. Makala hiyo inaendelea kuonyesha kwamba njia pekee ya kujipatia furaha ni kuwa tayari kuwapa wengine zawadi. Kwa kweli, kutoa hutufanya tuwe wenye furaha kuliko kupokea.

Biblia inasema nini? “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”Matendo 20:35.

Mara nyingi, njia bora zaidi ya kutoa—na yenye kuthawabisha zaidi—ni kutoa wakati na nguvu zetu. Kwa mfano, mwanamke mmoja anayeitwa Karen alimwona mama na binti zake wawili wakiwa wameketi kwenye gari lao huku boneti la gari likiwa wazi. Mama huyo pamoja na binti yake mmoja walipaswa kusafiri kwa ndege; lakini gari lao lilikuwa limeharibika na walikuwa wakisubiri teksi ambayo ilikuwa imechelewa. Karen alijitolea kuwapeleka kwenye uwanja wa ndege ingawa ulikuwa umbali wa dakika 45, nao wakakubali. Aliporudi, Karen alimwona binti yule mwingine akiwa bado anasubiri tu ndani ya gari lake lililokuwa limeegeshwa.

Mwanamke huyo alimwambia Karen, “Mume wangu yuko njiani.”

Karen akamjibu: “Nafurahi kusikia hivyo. Naenda kutunza bustani ya Jumba la Ufalme, yaani, kanisa letu.”

“Kwani wewe ni Shahidi wa Yehova?” mwanamke huyo akamwuliza.

“Ndiyo,” akajibu Karen, na wakazungumza kifupi.

Majuma machache baadaye, Karen alipokea barua. Ilisema hivi kwa sehemu: “Mimi na mama yangu bado tunakumbuka fadhili ulizotuonyesha. Tulifaulu kupata ndege yetu na tunakushukuru sana! Dada yangu alitueleza kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova, na hilo linafanya tuelewe kwa nini ulitutendea kwa fadhili hivyo. Mama yangu ni Shahidi, na mimi ni Shahidi asiyetenda. Lakini nitarekebisha jambo hilo hivi karibuni!” Karen alifurahi sana kujua kwamba aliwasaidia waamini wenzake. Anasema: “Nilitokwa na machozi.”

Mwandishi Charles D. Warner aliandika hivi: “Mojawapo ya mambo yenye kupendeza  sana maishani ni kwamba . . . mtu anayejitolea kumsaidia mwingine hujisaidia mwenyewe pia.” Hiyo ni kwa sababu Mungu hakuwaumba wanadamu wawe wenye ubinafsi, bali aliwaumba wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa zake zenye thamani.Mwanzo 1:27.

Unyoofu.

Kanuni hiyo ni muhimu katika jamii. Ukosefu wa unyoofu hufanya watu wawe na woga, waache kuaminiana, na kuzorotesha jamii.

Biblia inasema nini? “Ni nani atakayekuwa mgeni katika hema [la Mungu]?” Jibu? “Yeye anayetembea bila kosa na . . . kusema kweli katika moyo wake.” (Zaburi 15:1, 2) Kama tu zile sifa nyingine ambazo tumezungumzia, unyoofu wa kutoka moyoni ni tabia ambayo mtu anakuza. Hauongozwi na hali au ubinafsi.

Unamkumbuka Christina ambaye aliokota mfuko uliojaa pesa? Yeye hakutaka kujitajirisha bali alitaka kumpendeza Mungu. Kwa hiyo, mwenye mfuko huo aliporudi kuutafuta akiwa na wasiwasi, Christina alimwambia kwamba pesa zake zimepatikana. Alishangazwa sana na unyoofu wake. Hata mwajiri wa Christina alipendezwa na unyoofu wake hivi kwamba alimpandisha cheo na kumweka kuwa msimamizi wa bidhaa zote katika kiwanda chake. Cheo hicho hupewa mtu anayeaminiwa sana. Kisa hicho kinaonyesha ukweli wa maneno ya 1 Petro 3:10: ‘Yeye ambaye anapenda uzima na kuona siku zilizo njema, na azuie midomo yake isiseme udanganyifu.’

‘TEMBEA KATIKA NJIA YA WATU WEMA’

Kanuni za maadili ambazo zinapatikana katika Biblia zinaonyesha kwamba Muumba wetu anatupenda sana kwa kuwa zinatuwezesha “kutembea katika njia ya watu wema.” (Methali 2:20; Isaya 48:17, 18) Tunapofuata mwongozo huo, sisi pia tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na tunapata faida nyingi. Kwa kweli, Biblia inaahidi hivi: ‘Ishike njia ya Mungu, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.’Zaburi 37:34.

Wale wanaofuata viwango vya Biblia wanatarajia wakati ujao mzuri, yaani, kuishi katika dunia yenye amani isiyo na uovu hata kidogo! Kwa kweli tunapaswa kuchunguza kanuni zilizo katika Biblia.