Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Umedumisha Mtazamo Mzuri”

“Umedumisha Mtazamo Mzuri”

“Umedumisha Mtazamo Mzuri”

● Camila anaugua ugonjwa wa kupungukiwa na damu, ana matatizo ya neva, na ya ukuzi. Kwa hiyo, alipokuwa na umri wa miaka minane, alikuwa na kimo cha sentimita 75 tu. Wazazi wa Camila, ambao ni Mashahidi wa Yehova, waliamua kumpeleka kwenye kongamano la kitiba lililokuwa kwenye ukumbi wa maonyesho katika eneo la nyumbani kwao huko Argentina. Waliketi kwenye viti vya mbele, na watu 500 walihudhuria.

Katika hotuba yake, msemaji mmoja ambaye pia ni daktari, alimwelekezea Camila kidole na kusema kwamba yeye ni mtoto aliyeonekana kuwa na afya nzuri. Bila kujua umri wa Camila na matatizo yake ya afya, aliuliza: “Mtoto huyu ana umri wa miaka mingapi?”

“Miaka minane,” akajibu Marisa, mama ya Camila.

“Eti umesema miezi minane?” akauliza daktari.

“Hapana, miaka minane,” Marisa akajibu.

Akiwa ameshangaa mno, daktari alimwomba Marisa pamoja na binti yake waje jukwaani ili awahoji zaidi. Baada ya Marisa kueleza uchunguzi na matibabu ambayo madaktari wamempa Camila, daktari yule alisema: “Kuna akina mama ambao hulalamika sana mtoto wao anaposhikwa na mafua tu. Lakini baada ya kujaribu matibabu mbalimbali kwa miaka saba ili kumsaidia Camila, bado umedumisha mtazamo mzuri. Ni nini kimekusaidia?”

Marisa aliwaeleza wasikilizaji kuhusu tumaini lake la Biblia la ulimwengu mpya wenye uadilifu, wakati ambapo hakutakuwa na magonjwa yoyote, kuteseka, wala kifo. (Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4) Mwishowe, Marisa alieleza kuhusu undugu wa ulimwenguni pote ambao Mashahidi wa Yehova wanafurahia na akaeleza jinsi upendo kati yao unavyowasaidia Mashahidi kukabiliana na matatizo mbalimbali yanayotokea maishani.—Yohana 13:35.

Baada ya kongamano hilo kwisha, mwanamke mmoja alimwomba Marisa amweleze zaidi kuhusu mambo aliyosema. Mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia nyumbani bila malipo pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa sababu wao huwasaidia watu ulimwenguni pote ambao kwa kweli wangependa kujifunza Biblia na kuelewa kuhusu kusudi zuri la Mungu kwa wanadamu.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Camila mwenye umri wa miaka minane pamoja na mama yake, Marisa