Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Biblia

Je, Ni Sawa Kusali kwa “Watakatifu”?

Je, Ni Sawa Kusali kwa “Watakatifu”?

Marie na Theresa waliamini kwamba wao ni “Wakatoliki wazuri.” Wote waliamini kwamba kuna “watakatifu.” Marie aliamini kwamba anaweza kusali na kuwaomba msaada. Theresa alisali kwa ukawaida kwa “mtakatifu” mkuu wa kijiji chao. Pia alisali kwa “mtakatifu” aliyekuwa na jina kama lake.

KAMA tu Marie na Theresa, mamilioni ya watu ulimwenguni husali kwa “watakatifu” wakiomba baraka. Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia, “watakatifu husali kwa niaba ya wanadamu,” na “‘inafaa na ni vizuri’ kuwasihi watuombee . . . baraka za Mungu.”

Hata hivyo, Mungu ana maoni gani kuhusu jambo hilo? Je, ni sawa kwake kwamba tusali kwa “watakatifu” ili wao wamsihi kwa niaba yetu? Ona maoni ya Biblia.

Je, Tuwaombe “Watakatifu” Msaada?

Hakuna mahali katika Biblia ambapo mtumishi mwaminifu wa Mungu alisali kwa “mtakatifu.” Kwa nini? Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema kwamba katika “karne ya tatu ndipo maoni yalipotolewa kwamba watu wanapaswa kuwaomba watakatifu wasali kwa niaba yao.” Hiyo ilikuwa miaka 200 hivi baada ya Kristo kufa. Kwa hiyo, fundisho hilo halikuanzishwa na Yesu wala na waandikaji wa Biblia walioongozwa kwa roho ya Mungu ambao waliandika habari kuhusu huduma yake. Kwa nini?

Biblia yote inafundisha kwamba tunapaswa kusali kwa Mungu peke yake, kupitia kwa jina la Yesu Kristo. Yesu alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6, Union Version) Maneno hayo ya wazi yanapatana na fundisho la Yesu lililo katika Mathayo 6:9-13. Akieleza kuhusu sala, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Basi, ninyi msali hivi: Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. . . .” (Mathayo 6:9) Kwa wazi basi, Baba yetu wa mbinguni ndiye tu tunayepaswa kusali kwake. Hiyo ni kweli inayotegemea kanuni fulani ya msingi ya Biblia.

Sala—Tendo la Ibada

Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema: “Sala, ni maneno na mawazo yenye heshima yanayoelekezwa kwa Mungu, miungu, miungu ya kike, au kwa mifano inayotumiwa katika ibada. . . . Sala ni sehemu muhimu ya ibada katika karibu dini zote ulimwenguni.” (Italiki ni zetu.) Jiulize, ‘Je, ni sawa kupiga magoti na kusali kumwelekea mtu mwingine yeyote isipokuwa Muumba na Mpaji-Uhai wetu?’ (Zaburi 36:9) Yesu alisema hivi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Biblia pia inasema kwamba Muumba wetu anataka ‘tujitoe kikamili’ kwake.—Kumbukumbu la Torati 4:24; 6:15.

Fikiria mfano wa mtume Yohana Mkristo. Baada ya kupokea maono yenye kuvutia yaliyoandikwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, mtume huyo aliyejawa na hofu ‘alianguka chini kuabudu mbele ya miguu ya malaika’ aliyekuwa amemwonyesha mambo hayo. Lakini malaika huyo alifanya nini? “Uwe mwangalifu!” malaika huyo akasema. “Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu na wa ndugu zako . . . Mwabudu Mungu.” (Ufunuo 22:8, 9) Ndiyo, Biblia inakazia kwamba tunapaswa kumwabudu Yehova Mungu peke yake.

Kupatana na mambo yaliyotajwa hapo juu, Mungu peke yake ndiye anayeitwa “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Isitoshe, akiwa Mweza-Yote, yeye peke yake ndiye aliye na mamlaka, ujuzi, na uwezo wa kujibu sala yoyote. (Ayubu 33:4) Hata Yesu Kristo mwenyewe alikiri kwamba uwezo wake una mipaka. (Mathayo 20:23; 24:36) Licha ya hayo, Yesu Kristo amepewa mamlaka kubwa, kutia ndani daraka la kutumika akiwa Mwombezi wa wanadamu.

Mwombezi Mwenye Huruma

Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Yeye anaweza pia kuwaokoa kwa ukamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.” (Waebrania 7:25) Kwa maneno mengine, Yesu anaweza kuwa Mwombezi mwenye huruma kwa niaba ya wale “wanaomkaribia Mungu kupitia yeye.” Hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kusali kwa Yesu na eti yeye atampitishia Mungu sala yetu. Badala yake, linamaanisha kwamba tunasali kwa Mungu katika jina la Yesu, hivyo tukionyesha kwamba tunatambua mamlaka yake. Kwa nini Yesu ndiye anayestahili zaidi kuwa Mwombezi wetu?

Sababu moja ni kwamba Yesu aliwahi kuwa mwanadamu, na hilo lilimfanya aweze kuelewa vizuri zaidi kuteseka kwa watu wengine. (Yohana 11:32-35) Isitoshe, aliwaonyesha watu upendo kwa kuwaponya wagonjwa, kufufua wafu, na kuwaandalia maandalizi ya kiroho wote waliomwendea. (Mathayo 15:29, 30; Luka 9:11-17) Hata alisamehe dhambi. (Luka 5:24) Hilo linatusaidia tuwe na uhakika, kwa kuwa tukitenda dhambi, “tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu.”—1 Yohana 2:1.

Yesu alionyesha upendo na rehema, sifa tunazopaswa kujitahidi kuiga. Ni kweli kwamba hatujapewa mamlaka ya kuwa waombezi. Lakini tunaweza kusali kwa ajili ya wengine. Kwa kweli, upendo unapaswa kutuchochea kufanya hivyo. Yakobo aliandika hivi: ‘Salini kwa ajili ya mtu na mwenzake. Dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi.’—Yakobo 5:16.

Marie na Theresa walijifunza kweli hizo muhimu kwa kujichunguzia Biblia. Mashahidi wa Yehova wanakutia moyo ufanye hivyo pia. Kama Yesu alivyosema, “wale wanaomwabudu [Mungu] lazima wamwabudu kwa roho na kweli.”—Yohana 4:24.