Hamia kwenye habari

Mungu Ana Majina Mangapi?

Mungu Ana Majina Mangapi?

Jibu la Biblia

 Mungu ana jina moja tu la kibinafsi. Katika Kiebrania jina hilo linaandikwa יהוה na kwa kawaida linaandikwa “Yehova” katika Kiswahili. a Mungu alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” (Isaya 42:8) Jina hilo linapatikana karibu mara 7,000 katika hati za kale za Biblia​—hizo ni mara nyingi zaidi kuliko neno lolote linalotumiwa kumrejelea Mungu, au hata kuliko jina la mtu mwingine yeyote. b

Je, Mungu ana majina mengine?

 Ingawa Biblia inamtaja Mungu kwa jina moja tu la kibinafsi, inatumia majina mengi ya cheo na ya kumfafanua. Orodha ifuatayo ya baadhi ya majina hayo ya cheo na ya kumfafanua inaonyesha jinsi kila moja linavyofunua sehemu ya utu wa Yehova.

Jina la Cheo

Rejeo

Maana

Allah

(Hakuna)

Neno hili la Kiarabu “Allah,” si jina la kibinafsi bali ni jina la cheo linalomaanisha “Mungu.” Tafsiri za Biblia katika Kiarabu na lugha nyingine zinatumia jina la cheo “Allah” kurejelea neno “Mungu.”

Mweza-Yote

Mwanzo 17:1

Ana nguvu zisizo na kifani. Neno la Kiebrania ʼEl Shad·daiʹ, “Mungu Mweza-Yote,” linapatikana mara saba katika Biblia.

Alfa na Omega

Ufunuo 1:8; 21:6; 22:13

“Wa Kwanza na wa mwisho,” au “mwanzo na mwisho,” kumaanisha kwamba hakukuwa na Mungu Mweza-Yote kabla ya Yehova na hakutakuwa na yeyote baada yake. (Isaya 43:10) Alfa na omega ni herufi ya kwanza na ya mwisho katika alfabeti ya Kigiriki.

Mzee wa Siku

Danieli 7:​9, 13, 22

Hakuwa na mwanzo; alikuwepo milele kabla ya mtu yeyote au kitu chochote kingine kuwepo.​—Zaburi 90:2.

Muumba

Isaya 40:28

Alitokeza kila kitu.

Baba

Mathayo 6:9

Ndiye mpaji-uhai.

Mungu

Mwanzo 1:1

Ndiye wa kuabudiwa; ana nguvu. Neno la Kiebrania ʼElo·himʹ linaandikwa kwa wingi, kuonyesha ukuu, heshima, na utukufu wa Yehova.

Mungu wa miungu

Kumbukumbu la Torati 10:17

Mungu mkuu zaidi, akitofautishwa na “miungu isiyo na thamani” ambayo watu fulani huabudu.​—Isaya 2:8.

Mfundishaji Mkuu

Isaya 30:20, 21

Anafundisha na kuongoza kwa njia inayofaa.​—Isaya 48:17, 18.

Mtengenezaji Mkuu

Zaburi 149:2

Alitokeza vitu vyote.​—Ufunuo 4:​11.

Mungu mwenye furaha

1 Timotheo 1:​11

Ana shangwe na furaha nyakati zote.​—Zaburi 104:31.

Msikiaji wa sala

Zaburi 65:2

Yeye binafsi husikiliza kila sala inayotolewa kwake kwa imani.

Mimi Niko Ambaye Niko

Kutoka 3:​14, Union Version

Anakuwa chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. Maneno hayo yametafsiriwa pia “Mimi Ndimi Niliye” au “Nitakuwa Kile Nitakachokuwa.” (Biblia Habari Njema; Tafsiri ya Ulimwengu Mpya) Ufafanuzi huo unasaidia kueleza maana ya jina la Mungu, Yehova, linalotajwa katika mstari unaofuata.​—Kutoka 3:​15.

Mwenye Wivu

Kutoka 34:14, Biblia Habari Njema

Havumilii ushindani wowote katika ibada.

Mfalme wa umilele

Ufunuo 15:3

Utawala wake hauna mwanzo wala mwisho.

Bwana

Zaburi 135:5

Mmiliki; Kiebrania ʼA·dhohnʹ na ʼAdho·nimʹ.

Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Bwana wa majeshi

Isaya 1:9, Biblia Habari Njema; Waroma 9:​29, Biblia Habari Njema

Amiri-jeshi wa jeshi kubwa la malaika. Jina hilo la cheo “Bwana wa majeshi” linatafsiriwa pia “Yehova wa majeshi.”​—Waroma 9:​29, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Aliye Juu Zaidi

Zaburi 47:2

Ana cheo cha juu zaidi.

Mtakatifu Zaidi

Methali 9:​10

Ni mtakatifu (safi kabisa kiadili) kuliko kiumbe yeyote.

Mfinyanzi

Isaya 64:8

Ana mamlaka juu ya watu mmojammoja na mataifa, kama vile mfinyanzi alivyo na mamlaka juu ya udongo.​—Waroma 9:​20, 21.

Mkombozi

Isaya 41:14

Anakomboa au kuwanunua wanadamu kutoka katika dhambi na kifo kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.​—Yohana 3:​16.

Mwamba

Zaburi 18:​2, 46

Kimbilio salama na chanzo cha wokovu.

Mwokozi

Isaya 45:21

Anaokoa kunapokuwa na hatari au maangamizi.

Mchungaji

Zaburi 23:1

Anawatunza waabudu wake.

Bwana Mwenye Enzi Kuu

Mwanzo 15:2

Ana mamlaka ya juu zaidi; Kiebrania ʼAdho·naiʹ.

Aliye Mkuu Zaidi

Danieli 7:​18, 27

Mwenye mamlaka ya juu zaidi.

Majina ya mahali katika Maandiko ya Kiebrania

 Majina ya mahali fulani katika Biblia yanatia ndani jina la Mungu la kibinafsi, lakini hayo si majina yanayotumika badala ya jina la Mungu.

Jina la mahali

Rejeo

Maana

Yehova-yire

Mwanzo 22:13, 14

“Yehova Ataandaa.”

Yehova-nisi

Kutoka 17:15

“Mwenyezi-Mungu ni Bendera Yangu.” (Biblia Habari Njema) Yehova ni Mungu ambaye watu wake wanaweza kumwendea ili kupata ulinzi na msaada.​—Kutoka 17:13-​16.

Yehova-shalomu

Waamuzi 6:​23, 24

“Mwenyezi-Mungu ni Amani.” (Biblia Habari Njema)

Yehova-shama

Ezekieli 48:35

“Yehova Mwenyewe Yupo Hapo.”

Sababu za kujua na kutumia jina la Mungu

  •   Lazima Mungu anahisi kwamba jina lake la kibinafsi Yehova ni muhimu, ndiyo sababu alilitaja mara nyingi sana katika Biblia.​—Malaki 1:​11.

  •   Mwana wa Mungu, Yesu, alikazia mara nyingi umuhimu wa jina la Mungu. Kwa mfano, alisali hivi kwa Yehova: “Jina lako na litakaswe.”​—Mathayo 6:9; Yohana 17:6.

  •   Wale ambao wanajifunza jina la Mungu na kulitumia wanachukua hatua za kwanza za kujenga urafiki pamoja na Yehova. (Zaburi 9:​10; Malaki 3:​16) Uhusiano kama huo unawawezesha kunufaika kutokana na ahadi hii ya Mungu: “Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu, mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.”​—Zaburi 91:14.

  •   Biblia inasema hivi: “Kuna wale wanaoitwa ‘miungu,’ iwe wako mbinguni au duniani, kama vile kulivyo na ‘miungu’ mingi na ‘mabwana’ wengi.” (1 Wakorintho 8:5, 6) Hata hivyo, inamtambulisha Mungu wa pekee wa kweli kwa jina lake, Yehova.​—Zaburi 83:18.

a Wasomi fulani wa Kiebrania wanapendelea kutumia “Yahweh” kama jina la Mungu.

b Ufupisho wa jina la Mungu, “Yah,” unaonekana mara 50 katika Biblia, kutia ndani neno “Haleluya,” linalomaanisha “Msifuni Yah.”​—Ufunuo 19:1.