Malaki 3:1-18

  • Bwana wa kweli aja kutakasa hekalu lake (1-5)

    • Mjumbe wa agano (1)

  • Washauriwa wamrudie Yehova (6-12)

    • Yehova habadiliki (6)

    • “Nirudieni, nami nitawarudia” (7)

    • ‘Leteni sehemu yote ya kumi, na Yehova atawamwagia baraka’ (10)

  • Mwadilifu na mwovu (13-18)

    • Majina yaandikwa katika kitabu cha kumbukumbu cha Mungu (16)

    • Tofauti kati ya mwadilifu na mwovu (18)

3  “Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu, naye atafungua* njia mbele yangu.+ Na ghafla Bwana wa kweli, mnayemtafuta, atakuja katika hekalu lake;+ na mjumbe wa agano atakuja, mnayependezwa naye. Tazama! Kwa hakika atakuja,” asema Yehova wa majeshi.  “Lakini ni nani atakayestahimili siku atakayokuja, na ni nani atakayeweza kusimama atakapotokea? Kwa maana atakuwa kama moto wa msafishaji wa madini na kama sabuni+ ya wafuaji wa nguo.  Naye ataketi kama msafishaji na mtakasaji wa fedha,+ naye atawatakasa wana wa Lawi; atawasafisha kama dhahabu na kama fedha, nao hakika watakuwa watu wanaomtolea Yehova zawadi kwa uadilifu.  Na kwa kweli zawadi ya Yuda na Yerusalemu itampendeza* Yehova, kama ilivyokuwa katika siku za kale na kama ilivyokuwa katika miaka ya zamani za kale.+  “Nitawakaribia ili niwahukumu, nami nitakuwa shahidi asiyesita* dhidi ya walozi,+ dhidi ya wazinzi, dhidi ya watu wanaotoa viapo vya uwongo,+ dhidi ya wale wanaomlaghai kibarua,+ mjane, na yatima,*+ na dhidi ya wale wanaokataa kumsaidia* mgeni.+ Watu hao hawaniogopi,” asema Yehova wa majeshi.  “Kwa maana mimi ni Yehova; sibadiliki.*+ Nanyi ni wana wa Yakobo; bado hamjaangamia.  Tangu siku za mababu zenu mmegeuka na kuacha masharti yangu nanyi hamjayashika.+ Nirudieni, nami nitawarudia,”+ asema Yehova wa majeshi. Lakini mnauliza: “Tukurudie jinsi gani?”  “Je, mwanadamu anaweza kumwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia.” Nanyi mnauliza: “Tumekuibia jinsi gani?” “Katika sehemu za kumi na michango.  Kwa hakika mmelaaniwa,* kwa maana mnaniibia—naam, taifa zima linafanya hivyo. 10  Leteni ghalani sehemu yote ya* kumi,+ ili kuwe na chakula nyumbani mwangu;+ tafadhali, nijaribuni kwa njia hii,” asema Yehova wa majeshi, “mwone kama sitawafungulia malango ya mbinguni ya mafuriko+ na kuwamwagia baraka hivi kwamba hamtakosa chochote.”+ 11  “Na kwa ajili yenu nitamkemea yule anayenyafua,* naye hataharibu mazao ya nchi yenu, wala mzabibu wa shamba lenu hautakosa matunda,”+ asema Yehova wa majeshi. 12  “Mataifa yote yatalazimika kuwatangaza ninyi kuwa wenye furaha,+ kwa maana mtakuwa nchi ya kupendeza,” asema Yehova wa majeshi. 13  “Maneno yenu dhidi yangu yamekuwa makali,” asema Yehova. Nanyi mnauliza: “Ni katika njia gani tumesema maneno makali dhidi yako miongoni mwetu?”+ 14  “Mnasema, ‘Hakuna faida yoyote ya kumtumikia Mungu.+ Tumefaidikaje kwa kutimiza wajibu wetu kwake na kutembea kwa huzuni mbele za Yehova wa majeshi? 15  Sasa tunawaona watu wenye kimbelembele kuwa wenye furaha. Pia, watu wanaotenda maovu wanafanikiwa.+ Wanathubutu kumjaribu Mungu, nao hawaadhibiwi.’” 16  Wakati huo wale wanaomwogopa Yehova walizungumza kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kuwakazia uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaandikwa mbele zake+ kwa ajili ya wale wanaomwogopa Yehova na wale wanaolitafakari* jina lake.+ 17  “Nao watakuwa wangu,”+ asema Yehova wa majeshi, “siku nitakayotokeza mali ya pekee.*+ Nitawahurumia, kama mwanamume anavyomhurumia mwana wake anayemtumikia.+ 18  Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu,+ kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”

Maelezo ya Chini

Au “atatayarisha.”
Au “itamridhisha.”
Au “wanaomnyima haki.”
Tnn., “mtoto asiye na baba.”
Tnn., “mwepesi.”
Au “sijabadilika.”
Au labda, “Kwa laana mnanilaani.”
Au “sehemu zote za.”
Inaonekana ni pigo la wadudu.
Au “wanaolifikiria.” Au labda, “wanaolithamini.”
Au “mali ninayothamini sana.”