Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Isaya 42:8​—“Mimi Ni BWANA”

Isaya 42:8​—“Mimi Ni BWANA”

 “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu; simpi yeyote utukufu wangu, wala kuzipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isaya 42:8, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Mimi ni BWANA; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.”—Isaya 42:8, Union Version.

Maana ya Isaya 42:8

 Mungu anatuambia jina lake na pia anasema kwamba hakubali sifa au utukufu wake upewe sanamu.

  Mungu alijipatia jina lake binafsi ambalo mara nyingi hutafsiriwa “Yehova” katika Kiswahili. a (Kutoka 3:14, 15) Ingawa jina la Mungu linapatikana mara 7,000 katika Agano la Kale (Maandiko ya Kiebrania na Kiaramu), tafsiri nyingi hulibadili kwa jina la cheo “BWANA” (kwa herufi kubwa). Mfano mmoja ni Zaburi 110:1, inayotoa unabii kuhusu Yehova na Yesu. Tunasoma hivi katika Union Version: “Neno la BWANA [Yehova] kwa Bwana wangu [Yesu].” (Matendo 2:34-36) Ili kuondoa utata wowote unaweza kutokea katika kutofautisha hao “Mabwana” wawili, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia jina la Mungu mahali panapofaa. Inasema hivi: “Yehova alimwambia Bwana wangu: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka nitakapowaweka maadui wako kuwa kiti cha miguu yako.’”

 Wasomi wengi wanaamini kwamba jina la Mungu linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Ni Mungu wa kweli tu anayestahili jina hilo, kwa kuwa ni yeye tu anayeweza kuwa chochote au kuwezesha uumbaji wake kuwa chochote kile ili kutimiza kusudi lake.

  Akiwa Muumba na Mungu wetu wa kweli, Yehova anastahili ujitoaji wetu kamili. Hakuna yeyote au chochote kutia ndani sanamu na picha, kinachostahili ibada yetu.—Kutoka 20:2-6; 34:14; 1 Yohana 5:21.

Muktadha wa Isaya 42:8

 Katika mistari ya mwanzoni ya Isaya sura ya 42, Yehova anatabiri kuhusu utendaji wa ‘mchaguliwa wake.’ Mungu anasema mtumishi huyo aliyemkubali, “atayaletea mataifa haki.” (Isaya 42:1) Mungu alisema hivi kuhusu ahadi hiyo: “Sasa ninatangaza mambo mapya. Kabla hayajatokea, ninawaambia kuyahusu.” (Isaya 42:9) Unabii kuhusu ‘mchaguliwa wake’ ulitimizwa karne nyingi baadaye Masihi, au Kristo, alipofika na kutimiza huduma yake duniani.—Mathayo 3:16, 17; 12:15-21.

Isaya 42:8 Kulingana na Tafsiri Nyingine

 “Mimi ni Yehova, hilo ni jina langu; na utukufu wangu sitampa yeyote, wala sifa zangu kwa sanamu za kuchongwa.”— ‘Holy Scriptures,’ ya J. N. Darby.

 “Mimi ni Yehova; hilo ndilo jina Langu; nami sitampa utukufu Wangu mtu yeyote, wala sifa Zangu sanamu zilizochongwa.”—A Literal Translation of the Bible.

a Jina la Mungu katika Kiebrania lina konsonanti nne ambazo mara nyingi huandikwa katika Kiswahili YHWH. Katika baadhi ya tafsiri za Kiswahili, jina la Mungu limetafsiriwa kuwa “Yahweh.” Ili kupata habari zaidi, ona “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania” kwenye Nyongeza A4 ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.