Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 8

Masihi Atokea

Masihi Atokea

MIAKA zaidi ya 500 baada ya Danieli kutoa unabii, malaika wa Mungu, Gabrieli alimtokea msichana bikira aitwaye Maria, mzao wa Mfalme Daudi. Gabrieli akamwambia, “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” (Luka 1:28) Hata hivyo, Maria aliogopa. Salamu ya Gabrieli ilikuwa na maana gani?

Gabrieli alimwambia Maria kwamba atamzaa Masihi

Gabrieli akaeleza: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu; na, tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na . . . ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:30-33) Hiyo ilikuwa habari njema kama nini! Maria angemzaa Masihi, “uzao” uliosubiriwa sana!

Mwaka uliofuata, Yesu alizaliwa Bethlehemu. Usiku huo, malaika aliwatangazia hivi wachungaji: “Tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa . . . kwa sababu leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” (Luka 2:10, 11) Baadaye, familia ya Yesu ilihamia Nazareti, ambako alikulia.

Mnamo mwaka wa 29 W.K.—mwaka hususa ambao Masihi alitazamiwa kutokea—Yesu alianza kutumikia akiwa nabii wa Mungu, akiwa “na umri wa karibu miaka 30.” (Luka 3:23) Watu wengi wakaja kutambua kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Wakasema: “Nabii mkuu ameinuliwa katikati yetu.” (Luka 7:16, 17) Hata hivyo, Yesu alifundisha nini?

Yesu aliwafundisha watu kumpenda na kumwabudu Mungu: Alisema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja, nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:29, 30) Pia, alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.

Yesu aliwahimiza watu wapendane: Alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31) Pia alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo; hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.”—Mathayo 7:12.

Yesu alikuwa na bidii ya kuwatangazia wengine Ufalme wa Mungu: Alisema, “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini Ufalme wa Mungu ni wa maana sana?

Maandiko yanafundisha kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia. Yesu, yule Masihi, ndiye ambaye Mungu amemteua kuwa Mfalme. Katika maono, nabii Danieli aliona mapema Mungu akimkabidhi Masihi “utawala na heshima na ufalme,” mbinguni. (Danieli 7:14) Ufalme huo utaifanya dunia yote kuwa Paradiso na kuwapa watumishi wa Mungu zawadi ya uzima wa milele. Je, hizo si habari njema?