Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Viwango vya Biblia Kuhusu Mema na Mabaya Bado Vinafaa?

Je, Viwango vya Biblia Kuhusu Mema na Mabaya Bado Vinafaa?

 Watu wengi, kutia ndani wengine wanaodai kuwa Wakristo, wanahisi kwamba viwango vya maadili vya Biblia kuhusu ngono na ndoa vimepitwa na wakati. Ili kwenda na wakati, baadhi ya makanisa wamebadili mafundisho yao kuhusu mwenendo unaofaa na usiofaa. Je, viwango vya Biblia kuhusu mema na mabaya bado vinafaa? Ndiyo. Tunajua hilo kwa sababu zifuatazo.

Wanadamu wanahitaji viwango vya Mungu kuhusu mema na mabaya

 Wanadamu waliumbwa wamtegemee Muumba wao ili kupata mwongozo. Biblia inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Ijapokuwa Yehova a Mungu alituumba tukiwa na uwezo wa kufanya maamuzi, hakutupa mamlaka au uwezo wa kujiamulia mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa. Kwa sababu hiyo, anataka tumtegemee yeye.—Methali 3:5.

 Katika Biblia tunapata mwongozo wa Mungu kuhusu maadili. Fikiria sababu mbili kwa nini viwango hivyo ni vyenye thamani sana.

  •   Tuliumbwa na Mungu. (Zaburi 100:3) Akiwa Muumba wetu, Yehova Mungu anajua kile tunachohitaji hasa ili tuwe na afya nzuri na furaha kimwili, kiakili, na kihisia. Anajua matokeo mabaya tutakayopata tukipuuza viwango vyake vya kimaadili. (Wagalatia 6:7) Zaidi ya hayo, Yehova anataka tuwe na maisha bora. Kwa sababu hiyo, Biblia inamfafanua Mungu kuwa yule ‘anayetufundisha ili tujifaidi wenyewe, anayetuongoza katika njia tunayopaswa kutembea.’—Isaya 48:17.

  •   Tunaweza kupotoshwa na tamaa zetu. Watu wengi wanahisi kwamba wanaweza kujiamulia mema na mabaya kwa kutegemea moyo wao, yaani, tamaa zao. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Ikiwa moyo wetu hauongozwi na hekima ya Mungu, unaweza kutuongoza kutenda katika njia ambayo baadaye tukajutia.—Methali 28:26; Mhubiri 10:2.

Je, viongozi wa kidini wanapaswa kupuuza kile ambacho Biblia inasema kuhusu mema na mabaya?

 Hapana! Biblia inafundisha kweli kumhusu Mungu na jinsi anavyotaka tutende. (1 Wakorintho 6:9-11; Wagalatia 5:19-23) Anatamani kwamba watu wajue ukweli huo. (1 Timotheo 2:3, 4) Hivyo, wahubiri Wakristo wanapaswa kufundisha kile ambacho Neno la Mungu linasema.—Tito 1:7-9.

 Watu wengi ambao hawataki kufuata viwango vya Biblia vya maadili, hutafuta walimu wa dini ambao ‘watawaambia mambo wanayotaka kusikia.’ (2 Timotheo 4:3, maelezo ya chini) Hata hivyo, Neno la Mungu lina onyo hili kali: “Ole wao wanaosema kwamba wema ni uovu na uovu ni wema.” (Isaya 5:20) Kwa kweli, Mungu atawaadhibu viongozi wa kidini ambao hawawafundishi watu ukweli kuhusu maoni ya Mungu ya mema na mabaya.

Je, viwango vya Biblia kuhusu maadili vinawachochea watu kuwahukumu wengine?

 Hapana. Wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanafuata mfano na mafundisho ya Yesu Kristo. Aliwafundisha wafuasi wake waepuke kuwahukumu wengine badala yake wawaonyeshe watu wote upendo na heshima.—Mathayo 5:43, 44; 7:1.

 Yesu aliwafundisha wafuasi wake kufuata viwango vya Mungu vya maadili katika maisha yao wenyewe. Hata hivyo, aliwafundisha wanapaswa kukubali kwamba watu wengine wataamua kufuata viwango tofauti na alivyofundisha. (Mathayo 10:14) Yesu hakuwaruhusu wafuasi wake watumie siasa au njia nyingine yoyote ili kuwalazimisha watu watii viwango vya Mungu.—Yohana 17:14, 16; 18:36.

Kuna manufaa gani kuishi kulingana na viwango vya maadili vya Biblia?

 Wale wanaojitahidi kufuata viwango vya Mungu vya mema na mabaya watanufaika sasa na wakati ujao. (Zaburi 19:8, 11) Yafuatayo ni baadhi ya manufaa hayo:

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.