Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 6

Umuhimu wa Kuwa na Maadili

Umuhimu wa Kuwa na Maadili

MAADILI NI NINI?

Watu wenye maadili wana uwezo mzuri wa kutambua mambo sahihi na yasiyo sahihi. Maoni yao kuhusu maadili hayabadiliki kwa kutegemea hisia walizo nazo wakati huo. Badala yake, yanategemea kanuni ambazo huongoza jinsi wanavyojiendesha hata ikiwa hakuna mtu anayewatazama.

KWA NINI NI MUHIMU KUWA NA MAADILI?

Watoto hupokea habari nyingi zilizopotoka kuhusu maadili, iwe ni kutoka kwa watu wanaoshirikiana nao shuleni, kwenye muziki wanaosikiliza, au sinema na vipindi vya televisheni wanavyotazama. Mambo ya namna hiyo yanaweza kuyumbisha maoni yao kuhusu kile ambacho ni sahihi na kisicho sahihi.

Hali hii inawaathiri zaidi vijana walio katika umri wa kubalehe. Kitabu Beyond the Big Talk kinasema kwamba, vijana wanapofikia umri huo, “wanapaswa kuelewa kuwa marafiki na vyombo vya habari huwachochea watu wajiendeshe kwa njia fulani ili tu wakubalike, na wanapaswa kujifunza kufanya maamuzi kwa hiari na kupatana na kanuni walizojiwekea, hata kama hayawafurahishi marafiki zao.” Basi ni wazi kwamba, kazi ya kuwazoeza inapaswa kuanza kabla hawajafikia umri wa kubalehe.

JINSI YA KUMZOEZA MTOTO KUWA NA MAADILI

Mfundishe kanuni za maadili.

KANUNI YA BIBLIA: “Watu wakomavu . . . wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.”​—Waebrania 5:14.

  • Mwonyeshe tofauti ya mema na mabaya. Katika maisha ya kila siku, uwe ukimwonyesha tofauti kati ya jema na baya labda kwa kusema: “Huu ni unyoofu; huu si unyoofu.” “Huu ni ushikamanifu; huu si ushikamanifu.” “Tendo hili ni la fadhili; tendo hili si la fadhili.” Baada ya muda, mtoto wako ataweza kuhusianisha maneno na matendo yanayowakilishwa na maneno hayo.

  • Fafanua umuhimu wa kanuni za maadili unazofundisha. Kwa mfano, unaweza kumwuliza maswali kama vile: Kwa nini ni vizuri kuwa mnyoofu? Uwongo unaweza kuathirije urafiki? Kwa nini wizi ni mbaya? Zoeza dhamiri ya mtoto wako na uwezo wake wa kufikiri.

  • Mwonyeshe faida za kufuata kanuni za maadili. Unaweza kumwambia: “Ikiwa wewe ni mnyoofu, watu watakuamini,” au “Ikiwa wewe ni mwenye fadhili, watu watafurahia kushirikiana na wewe.”

Hakikisha familia yenu inatambulika kwa kufuata kanuni za maadili mlizojiwekea.

KANUNI YA BIBLIA: “Endeleeni kuthibitisha jinsi ninyi wenyewe mlivyo.”​—2 Wakorintho 13:5.

  • Familia yenu inapaswa kuishi kulingana na kanuni za maadili mlizojiwekea ili muweze kusema kwa uhuru kwamba:

    • “Katika familia yetu hatusemi uwongo.”

    • “Huwa hatupigani na watu wala hatuwafokei.”

    • “Huwa hatuongei kwa ukali wala kutukana.”

Mtoto wako ataona kwamba kanuni za maadili si sheria zilizowekwa tu, bali zinatambulisha njia ya maisha ya familia.

  • Mara kwa mara, zungumza na mtoto wako kuhusu kanuni zenu za maadili. Tumia hali zinazojitokeza kila siku kumfundisha mtoto wako. Unaweza kulinganisha maadili yenu na yale anayoona shuleni au kwenye vyombo vya habari. Muulize mtoto wako maswali kama: “Wewe ungefanyaje?” “Familia yetu ingeshughulikiaje hali hiyo?”

Msaidie kushikamana na kanuni za maadili ulizomzoeza.

KANUNI YA BIBLIA: “Iweni na dhamiri njema.”​—1 Petro 3:16.

  • Mpongeze anapofanya jambo zuri. Mtoto wako anapojiendesha vizuri, mpongeze na umweleze sababu ya kumpongeza. Kwa mfano, unaweza kumwambia: “Ulikuwa mnyoofu. Umenifurahisha sana.” Mtoto wako akifunua kosa lake kwako, mpongeze kwanza kwa unyoofu wake, kabla ya kumrekebisha.

  • Mrekebishe anapokosea. Msaidie mtoto wako kuwajibika kwa makosa yake. Watoto wanapaswa kutambua kile walichokosea na jinsi mwenendo wao ulivyo kinyume na kanuni za maadili za familia. Baadhi ya wazazi huogopa na kuhisi kwamba wataumiza hisia za watoto wakiwaeleza makosa yao, lakini kujadiliana na mtoto kuhusu makosa aliyofanya kutamsaidia kuzoeza dhamiri yake na uwezo wake wa kutofautisha jambo sahihi na lisilo sahihi.