Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA

Kuwafundisha Watoto Kuhusu Ngono

Kuwafundisha Watoto Kuhusu Ngono

CHANGAMOTO

Miaka michache iliyopita, wazazi walikuwa wa kwanza kuwafundisha watoto wao kuhusu ngono. Walifundisha hatua kwa hatua kulingana na umri na mahitaji ya mtoto.

Leo mambo yamebadilika. Kitabu The Lolita Effect kinasema hivi: “Watoto wanapata habari kuhusu ngono wakiwa bado wadogo sana, na habari hizo zimeenea katika vipindi vya burudani za watoto. Je, habari hizo zinawasaidia watoto au zinawaharibu?

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Habari chafu zinapatikana kwa urahisi. Deborah Roffman, katika kitabu chake Talk to Me First, anasema “mazungumzo, matangazo ya kibiashara, sinema, vitabu, muziki, vipindi vya televisheni, jumbe, michezo, mabango ya matangazo, simu na kompyuta zimejaa picha na lugha chafu za ngono hivi kwamba [watoto na matineja] wanafikiri kwamba ngono ndilo jambo kuu maishani.”

Wafanyabiashara wamechangia tatizo. Wafanyabiashara hutangaza na kuuza nguo za watoto zinazochochea hamu ya ngono, hivyo tangu wakiwa wachanga, watoto hukazia zaidi mwonekano. Kitabu So Sexy So Soon kinasema: “Wafanyabiashara wanajua kwamba watoto hupenda kuiga na kukubaliwa na marika wao, nao hutumia vibaya tamaa hiyo. Lengo kuu la wafanyabiashara ni kuuza bidhaa.

Ujuzi pekee hautoshi. Kuna tofauti kati ya kujua jinsi gari linavyofanya kazi na mtu kuwa dereva mzuri, vivyo hivyo kuna tofauti kati ya kujua kuhusu ngono na kufanya maamuzi ya hekima kuhusu ngono.

Jambo kuu: Leo, kuliko wakati mwingine wowote, unapaswa kuwafundisha watoto watumie “nguvu zao za ufahamu” ili “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.”—Waebrania 5:14.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Wafundishe. Ingawa si rahisi kuzungumza na watoto kuhusu ngono, kumbuka kwamba hilo ni daraka lako na unapaswa kulitimiza.—Kanuni ya Biblia: Methali 22:6.

Zungumzeni kifupi. Badala ya kutumia muda mrefu kuzungumza na watoto kuhusu ngono, tumia wakati mfupi, kama vile mnaposafiri au kufanya kazi za nyumbani. Tumia maswali ya maoni ili kumsaidia mtoto wako kujieleza. Kwa mfano, badala ya kumwuliza, “Je, unapenda matangazo yanayoonyesha picha chafu?” unaweza kumuuliza hivi: “Unafikiri ni kwa nini wafanyabiashara hutumia picha kama hizi ili kuuza bidhaa?” Baada ya kujibu, unaweza kumwuliza: “Unaonaje matangazo hayo?”—Kanuni ya Biblia: Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Wafundishe kulingana na umri. Watoto ambao hawajaanza shule wanaweza kufundishwa majina ya viungo vya uzazi na jinsi ya kujilinda na wale wanaotaka kuwatendea vibaya kingono. Kadiri wanavyokua, wanaweza kufundishwa mambo ya msingi kuhusu viungo vya uzazi. Wanapobalehe, wanapaswa kuelewa kwa kina masuala yanayohusu ngono.

Wafundishe maadili. Anza kuwafundisha watoto wako umuhimu wa unyofu, heshima na maadili. Kisha, ukiwa umeweka msingi mzuri unaweza kuwafundisha kuhusu ngono. Pia, waeleze waziwazi msimamo wako. Kwa mfano, wafundishe kwamba ni vibaya kufanya ngono kabla ya ndoa. Fafanua kwa nini ni vibaya kufanya hivyo. Kitabu Beyond the Big Talk kinasema: “Vijana wengi hukataa kufanya ngono kwa sababu wanajua kwamba wazazi wao hukataza jambo hilo.”

Uwe mfano mzuri. Ishi kulingana na maadili unayofundisha. Kwa mfano, je, unachukia mizaha michafu? je, mavazi yako ni yenye kiasi? au unaepuka kuwachezea wengine kingono? Mambo hayo yanaweza kuathiri viwango vya maadili unavyowafundisha watoto wako.—Kanuni ya Biblia: Waroma 2:21.

Uwe na maoni yanayofaa. Ngono ni zawadi kutoka kwa Mungu, na inaweza kuchangia furaha kati ya mume na mke katika ndoa. (Methali 5:18, 19) Mfundishe mtoto wako kwamba baada ya kufunga ndoa atafurahia zawadi hiyo, bila kupata madhara yanayotokana na kufanya ngono kabla ya ndoa.—1 Timotheo 1:18, 19.