Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anakubali Ushirikiano Kati ya Dini?

Je, Mungu Anakubali Ushirikiano Kati ya Dini?

 

“Je, dini inawaunganisha watu au inawatenganisha?” Gazeti moja linaloitwa The Sydney Morning Herald lilikuwa na swali hilo. Asilimia 89 ya waliojibu swali hilo, walisema kwamba dini hutenganisha watu.

LAKINI, watu wanaounga mkono ushirikiano kati ya dini wana maoni tofauti. Mwanzilishi wa shirika la Interfaith Youth Core, Eboo Patel, alisema: “Hakuna dini ambayo haifundishi watu kuwa na huruma . . . , au ambayo haijali mazingira . . . , au isiyokazia watu wawe wakarimu.”

Ni kweli kwamba Wabudha, Wakatoliki, Waprotestanti, Wahindu, Waislamu, na wafuasi wa dini nyingine wamewahi kushirikiana kupiga vita umaskini, kutetea haki za kibinadamu, kupinga mabomu yanayotegwa ardhini, au kujadili masuala ya mazingira. Dini mbalimbali zimehusika katika jitihada za kuungana na kutiana moyo. Wao husherehekea tofauti kati ya imani zao kupitia tamasha, nyimbo, maombi, kuwasha mishumaa, na kadhalika.

Je, ushirikiano kati ya dini ndiyo suluhisho la migogoro kati ya imani mbalimbali? Je, hiyo ndiyo njia ambayo Mungu anatumia ili kuleta ulimwengu bora?

KUTAFUTA UMOJA KWA NJIA YOYOTE ILE

Shirika moja kubwa la ushirikiano kati ya dini, linadai kwamba lina wanachama kutoka dini mbalimbali 200 na linaendesha shughuli zake katika nchi 76. Lengo lake ni “kuleta ushirikiano wa kudumu kati ya dini mbalimbali.” Kutimiza lengo hilo hakujawa rahisi. Kwa mfano, waratibu wa shirika hilo walisema mkataba wa shirika lao ulipaswa kuwa na maneno yaliyopangwa kwa uangalifu ili kuepuka kuudhi dini ambazo zilitia saini mkataba huo. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba walishindwa kukubaliana kama Mungu anapaswa kutajwa katika mkataba huo. Kwa hiyo, waliepuka kabisa kumtaja.

Ikiwa Mungu hahusishwi, basi imani yao ni ya bure. Kama ni hivyo, kuna tofauti gani kati ya shirika hilo na mashirika mengine ya kutoa misaada? Haishangazi kwamba shirika hilo linaitwa shirika la “kuleta upatano,” bali si shirika la kidini.

JE, INATOSHA KUKAZIA MEMA?

Dalai Lama, anayeunga mkono ushirikiano kati ya dini alisema: “Kimsingi, dini zote kubwa hufundisha mambo yaleyale, yaani, upendo, huruma, na kusamehe.” Na aliongezea kusema: “Tunapaswa kufanya mambo hayo kila siku.”

Ni kweli kwamba upendo, huruma, na kusamehe ni sifa muhimu sana. Hata Yesu Kristo alisema  hivi: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Lakini je, imani ya kweli inahusisha kukazia tu mambo mema?

Paulo alisema hivi kuhusu wengi waliodai kumtumikia Mungu: “Nawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” Walikuwa na tatizo gani? Paulo alisema “kwa sababu ya kukosa kujua uadilifu wa Mungu [walitafuta] kujiwekea uadilifu wao wenyewe.” (Waroma 10:2, 3) Hawakuwa na ujuzi sahihi juu ya yale ambayo Mungu alitaka wafanye, hivyo bidii na imani— yao ilikuwa bure kabisa.Mathayo 7:21-23.

MAONI YA BIBLIA KUHUSU USHIRIKIANO KATI YA DINI

Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” (Mathayo 5:9) Yesu alitenda kulingana na yale aliyofundisha kwa kuepuka jeuri na kutangaza ujumbe wa amani kwa watu wa dini mbalimbali. (Mathayo 26:52) Wale waliokubali walishirikiana pamoja kwa upendo. (Wakolosai 3:14) Lakini je, lengo la Yesu lilikuwa tu kuunganisha watu wenye imani mbalimbali ili waishi kwa amani? Je, alishirikiana na wengine katika dini zao?

Wakuu wa madhehebu ya Mafarisayo na Masadukayo walimpinga Yesu vikali, hata walijaribu kumuua. Aliitikiaje? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Waacheni. Wao ni viongozi vipofu.” (Mathayo 15:14) Yesu hakukubali kushirikiana na dini za watu kama hao.

Baada ya muda, kutaniko la Kikristo lilianzishwa huko Korintho, Ugiriki—mji uliofahamika kwa tamaduni na dini mbalimbali. Wakristo walipaswa kutendaje katika mji huo? Mtume Paulo aliwaandikia hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” Kwa nini? Paulo aliuliza: “Kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini?” Kisha akawashauri hivi: “Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge.”—2 Wakorintho 6:14, 15, 17.

Ni wazi kwamba, Biblia inapinga ushirikiano kati ya dini. Lakini huenda ukajiuliza, ‘Umoja unaweza kupatikanaje?’

KUJENGA UMOJA WA KWELI

Kituo cha Angani cha Kimataifa (The International Space Station) ni chombo cha ajabu cha kiteknolojia kinachozunguka dunia, ambacho kilitokezwa kupitia ushirikiano wa nchi 15. Je, unafikiri chombo hicho kingekuwepo ikiwa nchi hizo hazingekubaliana kuhusu muundo wake?

Hivyo ndivyo ilivyo katika jitihada za ushirikiano kati ya dini. Ingawa wanakazia ushirikiano na kuheshimiana, hawajakubaliana kuhusu mbinu ya kuunganisha imani. Matokeo ni kwamba hawapatani kuhusu viwango vya maadili na mafundisho.

Biblia ina viwango vya Mungu ambavyo ni msingi wa imani. Tunaweza kujenga imani yetu juu ya mafundisho ya Biblia. Wale ambao wamekubali mafundisho hayo wameshinda ubaguzi wa kidini na kijamii na wamejifunza kushirikiana kwa amani na umoja. Akitabiri jambo hilo, Mungu alisema: “Ndipo nitakapobadilisha lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.” Umoja unatokana na “lugha safi,” yaani, viwango vya Mungu vya ibada.—Sefania 3:9; Isaya 2:2-4.

Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu nawe, ili ujionee amani na umoja miongoni mwao.—Zaburi 133:1.