Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kuchagua Wakati Ujao Wenye Mafanikio?

Unawezaje Kuchagua Wakati Ujao Wenye Mafanikio?

Unawezaje Kuchagua Wakati Ujao Wenye Mafanikio?

UNAWEZAJE kuwa na maisha yenye mafanikio ya kweli? Njia moja ni kwa kutumia uwezo mkubwa ulio nao wa kuchunguza matokeo ya muda mrefu ya maamuzi unayofanya sasa.

Ni kweli kwamba huenda ikawa vigumu kwako kufanya maamuzi ambayo yatakufaidi katika maisha yako yote. Kwa nini? Kwa sababu watu wengi leo wangependa kupata mara moja vitu wanavyotaka. Kwa mfano, huenda umetambua kwamba kufuata mashauri ya Biblia kunaweza kukusaidia usitawishe mahusiano yenye nguvu katika familia. (Waefeso 5:22–6:4) Lakini ili upate matokeo hayo, ni lazima utumie muda mwingi pamoja na familia yako, huku ukiepuka kutumia wakati mwingi kufanya kazi, kujiburudisha, au kuwa na tafrija. Kama ilivyo na sehemu nyingi za maisha, ni lazima uchague kati ya kujifurahisha kwa muda mfupi au kupata mafanikio ya muda mrefu. Unawezaje kusitawisha uwezo wa kuchagua maisha yanayofaa? Ni kwa kufuata hatua nne zifuatazo.

1 Fikiria Matokeo ya Maamuzi Yako

Kabla ya kufanya uamuzi wowote, fikiria kwa makini matokeo ya uamuzi wako. Biblia inatushauri hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Ukichunguza kihalisi matokeo ya uamuzi fulani, inaelekea kwamba utaepuka kuchukua hatua ambazo zinaweza kusababisha matatizo. Kwa upande mwingine, ukifikiria faida za muda mrefu za kufanya uamuzi wenye hekima, unaweza kuimarisha azimio lako la kuchukua hatua.

Jiulize hivi: ‘Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani baada ya mwaka mmoja, au hata miaka 10 au 20 ijayo? Uamuzi huo utakuwa na matokeo gani juu ya hisia zangu na afya yangu? Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani juu ya familia yangu na wengine ninaowajali?’ Jambo muhimu zaidi, jiulize: ‘Je, uamuzi wangu utampendeza Mungu? Uamuzi huo utakuwa na matokeo gani juu ya urafiki wangu naye?’ Kwa kuwa Biblia imeandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, inaweza kukusaidia utambue mambo yanayompendeza na kukusaidia utambue hatari ambazo huenda ungepuuza.—Methali 14:12; 2 Timotheo 3:16.

2 Chunguza Maamuzi Unayohitaji Kufanya

Badala ya kujifanyia maamuzi, wengi huamua tu kuiga watu wanaowazunguka. Lakini uamuzi fulani hautakuletea mafanikio eti kwa sababu unapendwa na watu wengi. Jichunguzie maamuzi unayopaswa kufanya. Kwa mfano, mfikirie Natalie. * Anasema hivi: “Nilitamani kuwa na maisha mazuri ya ndoa. Lakini nilidhani singefaulu kwa sababu ya jinsi nilivyokuwa nikiishi. Chuoni, rafiki zangu wote walikuwa vijana werevu sana. Hata hivyo, kila wakati walifanya maamuzi mabaya maishani. Walibadili wapenzi kila mara. Kama wao, nilikuwa na wapenzi kadhaa wa kiume. Maisha hayo yaliniletea uchungu mwingi moyoni.”

Natalie alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Miongoni mwa Mashahidi niliona vijana wenye furaha na pia watu wenye uhusiano imara katika ndoa. Ingawa haikuwa rahisi kwangu, nilibadili viwango na maisha yangu hatua kwa hatua.” Matokeo yalikuwa nini? “Sikuzote nilitamani kuolewa na mtu ambaye nilivutiwa naye kabisa,” anasema Natalie. “Baada ya muda, niliolewa na mwanamume ambaye tulikuwa na imani moja ya kidini. Ninahisi kwamba Mungu amenipa maisha bora ya familia kuliko jinsi nilivyowazia.”

3 Fikiria Matokeo ya Muda Mrefu

Ili kuepuka kuangalia tu matokeo ya muda mfupi, unahitaji pia kufikiria waziwazi maisha ya wakati ujao ambayo ungependa na upange jinsi ya kufikia lengo hilo. (Methali 21:5) Usifikirie tu miaka 70 au 80 ambayo mwanadamu wa kawaida huishi. Badala yake, jiwazie ukifurahia uzima wa milele ambao unazungumziwa katika Biblia.

Biblia inaeleza kwamba kupitia dhabihu ya ukombozi ya Kristo Yesu, Mungu amefanya mpango ili wanadamu wapate uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Waroma 6:23) Mungu anaahidi kwamba hivi karibuni kusudi lake la mwanzoni kwa wanadamu na dunia litatimia. Wale wanaompenda Mungu watapata nafasi ya kuishi milele kwa furaha katika dunia maridadi. (Zaburi 37:11; Ufunuo 21:3-5) Unaweza kuwa na wakati ujao kama huo ikiwa utafikiria matokeo ya muda mrefu.

4 Jitahidi Kufikia Miradi Yako

Unaweza kufanya nini ili ufurahie maisha yaliyoahidiwa wakati ujao? Anza kwa kupata ujuzi kumhusu Mungu. (Yohana 17:3) Ujuzi sahihi wa kweli za Biblia utakusaidia uwe na hakika kwamba ahadi za Mungu kuhusu wakati ujao zitatimia. Imani kama hiyo inaweza kukuimarisha ufanye mabadiliko yoyote yanayohitajiwa ili upate kibali cha Mungu.

Fikiria mambo ambayo Michael alijionea. Anasimulia hivi: “Nilianza kunywa pombe kupita kiasi na kutumia dawa za kulevya nilipokuwa na umri wa miaka 12. Nilishirikiana na genge fulani na nilitarajia kufa kabla ya kufikia umri wa miaka 30. Kwa sababu ya hasira na kukata tamaa nilijaribu kujiua mara kadhaa. Nilitumaini kwamba maisha yalikuwa na kusudi fulani, lakini sikulipata.” Michael alipokuwa katika shule ya sekondari, mshiriki fulani wa genge aliloshirikiana nalo alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Michael aliamua kujifunza pia.

Mambo ambayo Michael alijifunza katika Biblia yalibadili maoni yake kuhusu wakati ujao. “Nilijifunza kwamba wakati ujao dunia itafanywa kuwa paradiso tena na kwamba watu wataishi kwa amani, bila mahangaiko. Nilianza kuona huo kuwa wakati wangu ujao. Nilijiwekea mradi wa kusitawisha urafiki pamoja na Yehova. Hata hivyo nyakati fulani nilishindwa kumpendeza Yehova. Hata baada ya kuanza kujifunza Biblia, nililewa mara kadhaa. Na nikawa na uhusiano na msichana fulani.”

Michael alifauluje kushinda vizuizi na kufanikiwa kubadili maisha yake? Anasema hivi: “Mwalimu wangu wa Biblia alinitia moyo nisome Biblia kila siku na kushirikiana na watu waliotaka kumpendeza Mungu. Nilitambua kwamba washiriki wa genge nililoshirikiana nalo bado waliniathiri. Ingawa walikuwa kama familia yangu, nilivunja uhusiano huo.”

Michael alijiwekea miradi ya muda mfupi na mambo ya kutanguliza ambayo yalimsaidia kufikia mradi wake mkubwa wa kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Unaweza kufanya hivyo pia. Andika mradi wako wa muda mrefu na hatua ambazo unapaswa kuchukua sasa ili kuufikia. Zungumzia miradi yako na watu wanaoweza kukusaidia, na uwaombe wakusaidie kuchunguza maendeleo yako.

Usiahirishe kujifunza kumhusu Mungu na kufuata mwongozo wake katika maisha yako. Chukua hatua sasa za kuimarisha upendo wako kwa Mungu na Neno lake, Biblia. Neno la Mungu linamfafanua hivi mtu ambaye anafuata kanuni za Biblia: “Kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zaburi 1:1-3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Majina katika makala hii yamebadilishwa.