Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Ufilipino

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Ufilipino

MIAKA kumi hivi iliyopita, Gregorio na Marilou, wenzi wa ndoa waliokuwa na umri wa miaka zaidi ya 30 walifanya upainia huko Manila na wakati huohuo walikuwa wakifanya kazi ya wakati wote. Ijapokuwa haikuwa rahisi, walifanikiwa. Baadaye, Marilou alipandishwa cheo na kuwa meneja wa benki. Anasema hivi: “Tuliishi maisha ya starehe kwa sababu tulikuwa na kazi nzuri.” Waliamua kujenga nyumba ya kifahari katika eneo zuri kilomita 19 hivi upande wa mashariki wa jiji la Manila. Kwa hiyo, walifanya mkataba na kampuni moja ya ujenzi ili iwajengee nyumba hiyo kwa mkopo nao wangelipa deni hilo kila mwezi kwa miaka kumi.

“NILIHISI NINAMWIBIA YEHOVA”

Marilou anasema hivi: “Nikiwa meneja, nilitumia wakati na nguvu nyingi kazini hivi kwamba bidii yangu katika utendaji wa kiroho ikapungua. Nilihisi ninamwibia Yehova.” Kisha anasema hivi: “Sikuweza tena kutumia wakati nilioahidi kutumia katika utumishi wa Yehova.” Gregorio na Marilou hawakufurahia hali hiyo, hivyo, siku moja waliamua kuzungumzia jinsi walivyokuwa wakitumia maisha yao. Gregorio anasema hivi: “Tulitaka kufanya  mabadiliko lakini hatukujua tungefanyaje mabadiliko hayo. Tulizungumzia jinsi tunavyoweza kutumia kikamili maisha yetu kumtumikia Yehova, hasa kwa sababu hatukuwa na watoto. Tukasali ili Yehova atuongoze.”

Wakati huo, walisikia hotuba kadhaa kuhusu kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Gregorio anasema: “Tulihisi kwamba Yehova alijibu sala zetu kupitia hotuba hizo.” Wenzi hao walimwomba Yehova awape imani zaidi ili wawe na ujasiri wa kufanya uamuzi unaofaa. Jambo jambo lililowazuia hasa kufanya uamuzi huo ni ujenzi wa nyumba yao uliokuwa ukiendelea. Tayari walikuwa wamelipa pesa za ujenzi kwa miaka mitatu. Wangefanya nini? Marilou anasema hivi: “Tungepoteza pesa zote tulizokuwa tumelipa ikiwa tungevunja mkataba huo. Lakini tulihitaji kuamua ama kutanguliza mapenzi ya Yehova au tamaa zetu.” Walipokumbuka maneno ya mtume Paulo kuhusu ‘kukubali hasara,’ wakaamua kuacha ujenzi, wakaacha kazi zao za kimwili, wakauza baadhi ya vitu vyao, na kuhamia kijiji fulani cha mbali kilicho katika kisiwa cha Palawan, kilomita 480 upande wa kusini wa jiji la Manila.Flp. 3:8.

‘WALIJIFUNZA SIRI’

Kabla ya kuhama, Gregorio na Marilou walianza kuishi maisha rahisi, lakini hawakujua maisha yao mapya yangekuwaje hadi walipofika katika eneo hilo. Marilou anasema hivi: “Tulishtuka sana. Hakukuwa na umeme au vitu vingine tulivyozoea. Tulipika wali kwa kutumia moto wa kuni. Hakukuwa na maduka makubwa, mikahawa, na vitu vingine vinavyopatikana jijini.” Hata hivyo, walijikumbusha tena na tena kilichowafanya wahamie eneo hilo, na baada ya muda mfupi walizoea maisha hayo mapya. Marilou anasema: “Sasa ninafurahia uzuri wa uumbaji, kama vile nyota zinazong’aa usiku. Zaidi ya yote, ni shangwe kuona watu wakifurahi tunapowahubiria. Kutumikia hapa kumetusaidia ‘kujifunza siri’ ya kuridhika.”Flp. 4:12.

“Shangwe tunayopata tunapoona ongezeko la kiroho haina kifani. Sasa tunahisi kwamba maisha yetu yana kusudi.”—Gregorio na Marilou

Gregorio anasema: “Tulipofika, kulikuwa na Mashahidi wanne tu. Walifurahi sana nilipoanza kutoa hotuba ya watu wote kila juma na kupiga gitaa huku tukiimba nyimbo za Ufalme.” Katika kipindi cha mwaka mmoja, wenzi hao walijionea kikundi hicho kikiongezeka na kuwa kutaniko lenye wahubiri 24. Gregorio anasema hivi: “Upendo tunaoonyeshwa na kutaniko hili unatugusa moyo sana.” Wanapofikiria miaka sita waliyotumikia katika eneo hilo la mbali, wanasema hivi: “Shangwe tunayopata tunapoona ongezeko la kiroho haina kifani. Sasa tunahisi kwamba maisha yetu yana kusudi.”

 ‘NIMEONJA NA KUONA KWAMBA YEHOVA NI MWEMA!’

Nchini Ufilipino, ndugu na dada 3,000 hivi wamehamia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Dada waseja 500 hivi ni miongoni mwa wajitoleaji hao. Mfikirie Karen.

Karen

Karen, aliye na umri wa miaka 20 hivi, alilelewa katika jiji la Baggao, Cagayan. Alipokuwa tineja alifikiria kupanua huduma yake. Anasema hivi: “Kujua kwamba wakati uliobaki umepungua na watu wa namna zote wanahitaji kusikia ujumbe wa Ufalme, kulinichochea nitamani kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri.” Ingawa baadhi ya washiriki wa familia yake walimsihi afuatilie elimu ya juu zaidi badala ya kuhamia eneo la mbali kuhubiri, Karen alimwomba Yehova amwongoze. Alizungumza pia na ndugu wanaotumikia eneo la mbali. Alipokuwa na umri wa miaka 18, alihamia eneo lililo umbali wa kilomita 64 kutoka mji wao.

Kutaniko dogo alilohamia lilikuwa likihubiri eneo lenye milima kwenye Pwani ya Pasifiki. Karen anakumbuka hivi: “Ili kufika kwenye kutaniko hilo jipya, tulitembea kwa siku tatu kutoka Baggao, tukipanda na kushuka milima na kuvuka mito mara zaidi ya 30.” Anaongezea hivi: “Ili kuwafikia wanafunzi fulani wa Biblia, ninatembea kwa muda wa saa sita, kisha ninalala katika nyumba ya mwanafunzi, na kesho yake ninatembea kwa saa sita kurudi nyumbani.” Je, jitihada hizo zina faida yoyote? Karen anasema hivi huku akitabasamu: “Pindi nyingine ninaumwa na miguu, hata hivyo, ninaongoza mafunzo ya Biblia 18 hivi. ‘Nimeonja na kuona kwamba Yehova ni mwema’!”Zab. 34:8.

“NILIJIFUNZA KUMTEGEMEA YEHOVA”

Sukhi

Ni nini kilichomchochea Sukhi, dada mseja mwenye umri wa miaka zaidi ya 40 aliyeishi Marekani, kuhamia Ufilipino? Alihudhuria kusanyiko la mzunguko mwaka wa 2011 na wenzi fulani wa ndoa walihojiwa katika kusanyiko hilo. Walisimulia jinsi walivyouza baadhi ya vitu vyao na kuhamia Mexico ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri. Sukhi anasema hivi: “Mahojiano hayo yalinifanya nianze kufikiria miradi ambayo sikuwa nayo mwanzoni.” Sukhi, aliye na asili ya Kihindi, alipogundua kwamba wahubiri zaidi walihitajiwa ili kuwahubiria Wapunjabi nchini Ufilipino, aliamua kwenda kusaidia. Je, alikabili hali ngumu?

Sukhi anasema hivi: “Haikuwa rahisi kuamua ni vitu gani ambavyo ningeuza. Pia, baada ya kufurahia kuishi peke yangu kwa miaka 13 nilianza kuishi na familia moja. Haikuwa rahisi lakini nilijifunza kuishi maisha rahisi.” Ni changamoto gani  alizokabili alipohamia Ufilipino? Sukhi anasema hivi: “Ninaogopa sana wadudu na nilitamani sana kurudi nyumbani. Hata hivyo, nilijifunza kumtegemea Yehova hata zaidi!” Je, amepata faida yoyote kwa kufanya hivyo? Sukhi anasema hivi huku akitabasamu: “Yehova anatuambia, ‘Mnijaribu kama sitawamwagia baraka.’ Ninaona ukweli wa maneno hayo mwenye nyumba anaponiuliza, ‘Utarudi lini? Nina maswali mengi.’ Ninapata shangwe na uradhi ninapowasaidia watu wenye njaa ya kiroho!” (Mal. 3:10) Sukhi anaongezea hivi: “Kwa kweli haikuwa rahisi kufanya uamuzi wa kuhama. Lakini baada ya kuhama, nilistaajabu sana kuona jinsi Yehova alivyonitegemeza.”

‘NILISHINDA HOFU YANGU’

Sime, ndugu aliyeoa mwenye umri wa miaka karibu 40, kutoka Ufilipino, alipata kazi yenye mshahara mnono na kuhamia nchi fulani huko Mashariki ya Kati. Alipokuwa huko, alichochewa kumtanguliza Yehova maishani alipozungumza na mwangalizi wa mzunguko na kusikiliza hotuba iliyotolewa na mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Sime anasema hivi: “Niliogopa sana kuacha kazi.” Hata hivyo, Sime aliacha kazi hiyo na kurudi Ufilipino. Sime na mke wake, Haidee, wanatumikia huko Davao del Sur, kusini mwa Ufilipino, katika eneo kubwa lenye uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Sime anasema hivi: “Mimi hushukuru sana kwa sababu nilishinda hofu ya kupoteza kazi na kuamua kumtanguliza Yehova. Hakuna jambo linaloleta uradhi maishani kuliko kumpa Yehova kilicho bora zaidi!”

Sime and Haidee

“TUNARIDHIKA SANA!”

Ramilo na Juliet, wenzi wa ndoa mapainia walio na umri wa miaka 30 hivi, walijitolea kusaidia kutaniko lililohitaji msaada lililo umbali wa kilomita 30 hivi kutoka nyumbani kwao. Bila kujali hali ya hewa, Ramilo na Juliet huenda mara kadhaa kila juma katika eneo hilo kwa pikipiki yao ili kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Ijapokuwa si rahisi kusafiri katika barabara mbovu na madaraja yanayoning’inia, wanafurahi kwamba wamepanua huduma yao. Ramilo anasema hivi: “Mimi na mke wangu tunaongoza kwa ujumla mafunzo 11 ya Biblia! Ni kweli kwamba tunahitaji kujidhabihu ili kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa, hata hivyo tunaridhika sana!”1 Kor. 15:58.

Juliet and Ramilo

Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme nchini kwenu au katika nchi nyingine? Zungumza na mwangalizi wenu wa mzunguko, na usome makala yenye kichwa “Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 2011.