Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari

DADA wengi waseja ni kati ya idadi kubwa ya Mashahidi wenye bidii wanaotumikia katika nchi zenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Baadhi yao wametumikia katika nchi nyingine kwa miaka mingi. Ni nini kilichowachochea kuhamia kwenye nchi ya kigeni miaka mingi iliyopita? Wamejifunza nini kwa kutumikia katika nchi nyingine? Wamepata manufaa gani? Tuliwahoji baadhi ya dada hao wenye uzoefu. Ikiwa wewe ni dada mseja na unatamani kutoka moyoni kushiriki katika huduma hiyo yenye kuridhisha sana, tuna uhakika utanufaika na maelezo yao. Kwa kweli, watu wote wa Mungu wanaweza kunufaika kwa kuchunguza mfano wao.

KUSHINDA SHAKA

Anita

Je, wewe hujiuliza ikiwa kwa kweli unaweza kufanikiwa kutumikia katika nchi ya kigeni ukiwa painia mseja? Anita, mwenye umri wa miaka 75, alikuwa na shaka sana ikiwa angeweza kufanya hivyo. Alilelewa Uingereza, ambako alianza kutumikia akiwa painia alipokuwa na umri wa miaka 18. Anasema hivi: “Nilipenda kuwafundisha watu kumhusu Yehova, lakini sikuwazia ningetumikia katika nchi ya kigeni. Sikuwahi kujifunza lugha ya kigeni na nilisadiki kwamba singeweza kujifunza lugha yoyote. Kwa hiyo, nilipopata mwaliko wa kuhudhuria Shule ya Gileadi, nilishtuka. Nilishangaa kujua kwamba mtu duni kama mimi angeweza kupata mwaliko huo. Lakini niliwaza hivi: ‘Ikiwa Yehova anaona ninaweza, nitajaribu.’ Hiyo ni miaka zaidi ya 50 iliyopita. Tangu wakati huo, nimekuwa nikitumikia nikiwa mmishonari nchini Japani.” Anita anaongeza hivi: “Wakati mwingine, mimi huwaambia dada vijana hivi, huku macho yangu yakiwa yanang’aa: ‘Bebeni mifuko yenu na mwandamane nami katika safari yenye kusisimua zaidi maishani!’ Ninafurahi kusema kwamba wengi wamechukua hatua hiyo.”

KUJIPATIA UJASIRI

Mwanzoni, dada wengi ambao wametumikia katika nchi ya kigeni, walisita kuhamia kwenye nchi nyingine. Walijipa ujasiri jinsi gani?

Maureen

Maureen, mwenye umri wa miaka 64, anaeleza hivi: “Nilipokuwa nikikua, nilitamani maisha yenye kusudi ambayo yangehusisha kuwasaidia wengine.” Alipofikisha umri wa miaka 20, alihamia mkoa wa Quebec, nchini Kanada, ambako kulikuwa na uhitaji wa mapainia. “Baadaye, nilipokea mwaliko wa kuhudhuria Shule ya Gileadi, lakini nilihofia kwenda kwenye eneo jipya mbali na rafiki zangu.” Anaongeza hivi: “Nilikuwa na wasiwasi pia kuhusu kumwacha mama ambaye alikuwa akimtunza baba yangu mgonjwa. Nilisali kwa Yehova siku nyingi kuhusu mambo hayo huku nikitokwa na machozi. Nilipozungumza na wazazi wangu kuhusu mahangaiko hayo, walinihimiza nikubali mwaliko huo. Niliona pia jinsi kutaniko letu lilivyowategemeza kwa upendo. Kuona jinsi Yehova alivyowatunza kulinisaidia kuamini kwamba angenitegemeza pia. Sasa nilikuwa tayari kwenda!” Kuanzia mwaka 1979, Maureen alitumikia kwa miaka zaidi ya 30 akiwa mmishonari Afrika Magharibi. Leo, Maureen anaendelea kutumikia akiwa painia wa pekee nchini Kanada huku akimtunza mama yake. Anapofikiria miaka aliyotumikia katika nchi ya kigeni, anasema hivi: “Sikuzote Yehova aliniandalia kile nilichohitaji kwa wakati niliohitaji.”

Wendy

Wendy, mwenye umri wa miaka 65, alianza kutumikia akiwa painia nchini Australia alipokuwa tineja. Anakumbuka hivi: “Nilikuwa mwenye haya sana na ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza na watu nisiowafahamu. Lakini upainia uliniwezesha kuzungumza na watu wa namna zote, kwa hiyo nikapata ujasiri. Baadaye, niling’amua kwamba sikuwa mwenye haya tena. Upainia ulinifundisha kumtegemea Yehova, na nikaanza kuwa na tamaa ya kutumikia katika nchi ya kigeni. Pia, dada mmoja mseja aliyekuwa mmishonari nchini Japani kwa miaka zaidi ya 30, alinialika nikahubiri naye kwa miezi mitatu huko. Kutumikia pamoja naye kulichochea tamaa yangu ya kuhamia nchi ya kigeni.” Katika mwaka 1986, Wendy alihamia Vanuatu, kisiwa kilicho kilometa 1,770 hivi mashariki mwa Australia.

Bado Wendy anatumikia katika kisiwa cha Vanuatu, akifanya kazi kwenye ofisi ya kutafsiri. Anasema hivi: “Ninapata shangwe kubwa sana ninapoona vikundi na makutaniko yakianzishwa katika maeneo ya mbali. Ninahisi kwamba ni pendeleo kubwa sana kushiriki hata kwa kiasi kidogo katika kazi ya Yehova kwenye visiwa hivi.”

Kumiko (katikati)

Kumiko, ambaye sasa ana umri wa miaka 65, alikuwa painia wa kawaida nchini Japani, painia mwenzake alipopendekeza wahamie Nepal. Kumiko anasema hivi: “Painia huyo alinisihi tena na tena, lakini nikakataa. Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kujifunza lugha nyingine na kuzoea mazingira mapya. Pia, ilikuwa vigumu kupata pesa nilizohitaji ili kuhamia nchi nyingine. Nilipokuwa nikifikiria mahangaiko hayo, nilipata aksidenti ya pikipiki na nikalazwa hospitalini. Nikiwa huko, niliwaza hivi: ‘Sijui kitakachonipata baadaye. Ninaweza kupatwa na ugonjwa mbaya kisha nipoteze fursa ya kuwa painia katika nchi nyingine. Mbona nisitumikie kwenye nchi ya kigeni kwa angalau mwaka mmoja?’ Nilimwomba Yehova kwa bidii anisaidie.” Baada ya kutoka hospitalini, Kumiko alitembelea nchi ya Nepal, na baadaye yeye na painia mwenzake wakahamia huko.

Akifikiria miaka kumi aliyotumikia nchini Nepal, Kumiko anasema hivi: “Kama Bahari Nyekundu ilivyogawanyika, nilipata suluhisho la matatizo yaliyonihangaisha. Ninafurahi sana kwamba niliamua kutumikia katika eneo lenye uhitaji. Mara nyingi, ninaposhiriki ujumbe wa Biblia na familia fulani, majirani watano au sita huja kusikiliza. Hata watoto wadogo huniomba kwa heshima niwape trakti inayozungumzia Biblia. Ninafurahia sana kuhubiri katika eneo hili lenye matokeo mazuri.”

KUKABILIANA NA CHANGAMOTO

Haishangazi kujua kwamba dada waseja waliohojiwa walikabili changamoto. Walikabilianaje?

Diane

Diane, kutoka Kanada, anasema hivi: “Mwanzoni ilikuwa vigumu kwangu kuwa mbali na watu wa familia.” Sasa, akiwa na umri wa miaka 62, ametumikia akiwa mmishonari nchini Ivory Coast (sasa ni Côte d’Ivoire) kwa miaka 20. “Nilimwomba Yehova anisaidie niwapende watu katika mgawo wangu. Ndugu Jack Redford, mmoja wa walimu wangu wa Gileadi, alitueleza kwamba mwanzoni huenda tukahangaika, hata kushtuka kwa sababu ya hali katika mgawo wetu, hasa tunapojionea umaskini mwingi. Lakini akasema hivi: ‘Usiangalie umaskini. Angalia watu, nyuso zao, na macho yao. Angalia jinsi wanavyoitikia wanaposikia kweli za Biblia.’ Nilifanya hivyo, na nikapata baraka nyingi sana! Niliposhiriki ujumbe wa Ufalme wenye kufariji, niliona macho ya watu yaking’aa!” Ni nini kingine kilichomsaidia Diane kuzoea utumishi katika nchi nyingine? “Nilikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na wanafunzi wangu wa Biblia na nilifurahi sana kuona wakianza kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Nilijihisi nyumbani katika mgawo wangu. Kama Yesu alivyoahidi, nilipata mama, baba, ndugu, na dada wa kiroho.”—Marko 10:29, 30..

Anne, mwenye umri wa miaka 46, anatumikia barani Asia katika nchi ambayo kazi yetu imezuiwa. Anaeleza hivi: “Kwa miaka mingi ambayo nimetumikia maeneo mbalimbali kwenye nchi za kigeni, niliishi na dada waliokuwa na malezi na nyutu tofauti sana nami. Nyakati nyingine, hilo lilisababisha kutoelewana na kuumizana hisia. Hilo lilipotukia, nilijitahidi kuwa mwenye urafiki zaidi kuelekea dada nilioishi nao na kuelewa utamaduni wao vizuri. Nilijitahidi sana pia kuwaonyesha upendo na ufikirio. Ninafurahi kwamba jitihada hizo zilikuwa na matokeo mazuri na sasa nina marafiki wengi wa dhati wanaonisaidia kuvumilia katika mgawo wangu.”

Ute

Mnamo 1993, Ute, kutoka Ujerumani, mwenye umri wa miaka 53, alipewa mgawo wa kutumikia akiwa mmishonari nchini Madagaska. Anasema hivi: “Mwanzoni, ilikuwa vigumu kujifunza lugha ya wenyeji, kuzoea joto, na kukabiliana na ugonjwa wa malaria, amiba, na minyoo. Lakini ndugu wenyeji walinisaidia sana. Dada wenyeji, watoto wao, na wanafunzi wangu wa Biblia walinisaidia kwa subira kujifunza lugha hiyo. Mmishonari mwenzangu alinitunza kwa upendo nilipokuwa mgonjwa. Zaidi ya yote, Yehova alinisaidia. Nilimmiminia mahangaiko yangu kwa ukawaida katika sala. Halafu nikangoja kwa subira ili sala zangu zijibiwe. Nyakati nyingine nilisubiri kwa siku kadhaa au miezi mingi. Yehova alitatua matatizo yangu yote.” Kufikia sasa, Ute ametumikia nchini Madagaska kwa miaka 23.

WAMEBARIKIWA SANA

Kama wengine ambao wamejitolea katika nchi za kigeni, mara nyingi dada waseja wanaotumikia katika nchi hizo wameeleza kwamba kufanya hivyo kumewaletea thawabu nyingi. Wamepata baraka gani?

Heidi

Heidi, kutoka Ujerumani, mwenye umri wa miaka 73, amekuwa mmishonari nchini Ivory Coast (sasa ni Côte d’Ivoire) tangu 1968. Anasema hivi: “Jambo linaloniletea shangwe zaidi ni kuwaona watoto wangu wa kiroho ‘wakiendelea kutembea katika kweli.’ Baadhi ya wanafunzi wangu wa Biblia wanatumikia sasa wakiwa mapainia au wazee kwenye makutaniko. Wengi wao huniita Mama au Nyanya (Bibi). Mmoja wa wazee hao pamoja na mke na watoto wake huniona kama mmoja wa familia yao. Kwa hiyo, Yehova amenipa mwana, binti-mkwe, na wajukuu watatu.”—3 Yoh. 4.

Karen (katikati)

Karen kutoka Kanada, mwenye umri wa miaka 72, alitumikia Afrika Magharibi kwa miaka zaidi ya 20. Anasema hivi: “Umishonari ulinisaidia kujidhabihu, kuwa mwenye upendo, na subira zaidi. Pia, kufanya kazi na watu kutoka nchi mbalimbali kulinisaidia kuona mambo kwa njia tofauti-tofauti. Nilijifunza kwamba kuna njia mbalimbali za kufanya mambo. Na ni baraka kubwa sana kuwa na marafiki wapendwa ulimwenguni pote! Ingawa maisha na migawo yetu imebadilika, bado sisi ni marafiki.”

Margaret, kutoka Uingereza, mwenye umri wa miaka 79, alitumikia akiwa mmishonari nchini Laos. Anasema hivi: “Kutumikia katika nchi ya kigeni kuliniwezesha kujionea jinsi Yehova anavyowavuta watu wa rangi na malezi mbalimbali kwenye tengenezo lake. Kutumikia huko kuliimarisha sana imani yangu. Nimekuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova anaongoza tengenezo lake na kusudi lake litatimia.”

Kwa hakika, dada waseja wanaotumikia katika nchi za kigeni wameweka mfano mzuri sana katika utumishi wa Kikristo. Wanastahili kupongezwa sana. (Amu. 11:40) Jambo la kupendeza hata zaidi ni kwamba idadi yao inazidi kuongezeka. (Zab. 68:11) Je, unaweza kufanya mpango na kufuata hatua za dada wenye bidii waliohojiwa katika makala hii? Ukifanya hivyo, bila shaka ‘utaonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’—Zab. 34:8.