Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii Ambao Umetimia

Unabii Ambao Umetimia

Awali tulisimulia jinsi Croesus alivyopotoshwa na mwaguzi kutoka Delphi, na kusababisha ashindwe na mfalme wa Uajemi. Kwa upande mwingine, Biblia ina unabii wenye kustaajabisha kumhusu mfalme huyo wa Uajemi ambao ulitimia kikamili.

Nabii Mwebrania aliyeitwa Isaya alitabiri kwamba mfalme huyo angeitwa Koreshi na akaelezea jinsi ambavyo atalishinda jiji lenye nguvu la Babiloni. Unabii huo ulitolewa miaka 200 hivi mapema, muda mrefu kabla Koreshi hajazaliwa.

Isaya 44:24, 27, 28: “Yehova . . . anasema hivi, . . . ‘[Ninaviambia] vilindi vya maji, “Kauka, Nami nitaikausha mito yako yote”; Ninayesema kumhusu Koreshi, “Yeye ni mchungaji wangu, naye atatimiza kikamili mapenzi yangu yote”; Ninayesema kuhusu Yerusalemu, “Litajengwa upya,” na kuhusu hekalu, “Msingi wako utawekwa.”’”

Kulingana na mwanahistoria Mgiriki Herodoto, jeshi la Koreshi liligeuza mkondo wa Mto Efrati ambao ulipita katikati ya jiji la Babiloni. Mbinu ya Koreshi iliwawezesha wanajeshi wake kuingia Babiloni wakipitia kwenye Mto Efrati ambao maji yake yalikuwa yamepungua. Baada ya kulishinda jiji hilo, Koreshi aliwaachilia huru Wayahudi waliokuwa mateka Babiloni, na akawaruhusu warudi na kujenga upya jiji la Yerusalemu ambalo lilikuwa limeharibiwa miaka 70 mapema.

Isaya 45:1: “Hivi ndivyo Yehova anavyomwambia mtiwa-mafuta wake, Koreshi, ambaye nimeushika mkono wake wa kulia ili kuyatiisha mataifa mbele yake, kuwanyang’anya silaha wafalme, kufungua mbele yake milango yenye pande mbili, hivi kwamba malango hayatafungwa.”

Waajemi waliingia jijini kupitia malango makubwa yenye pande mbili ambayo kwa sababu ya uzembe, yalikuwa yameachwa wazi. Iwapo Wababiloni wangejua mipango ya Koreshi, wangefunga malango yote yaliyokuwa karibu na Mto Efrati. Lakini hawakujua, hivyo jiji halikuwa na ulinzi wowote.

Unabii huo wenye kustaajabisha, ni sehemu ya unabii mwingi ulioandikwa kwenye Biblia ambao ulitimia kikamili. * Tofauti na utabiri mwingi wa wanadamu unaotegemea miungu ya uwongo, unabii wa Biblia unatoka kwa Yule aliyesema: “Tangu mwanzo ninatabiri matokeo, na tangu zamani za kale mambo ambayo bado hayajafanywa.”—Isaya 46:10.

Ni Mungu wa kweli pekee, ambaye jina lake ni Yehova, anayeweza kusema maneno hayo. Inaeleweka kwamba maana ya jina hilo ni, “Yeye Husababisha Kuwa.” Linaonyesha uwezo wake wa kujua na kuelekeza matukio ya wakati ujao ili yapatane na mapenzi yake. Linatuhakikishia kwamba atatimiza kila kitu ambacho ameahidi kufanya.

UNABII UNAOTIMIA NYAKATI ZETU

Je, ungependa kujua unabii wa Biblia unasema nini kuhusu nyakati tunazoishi? Miaka 2,000 hivi iliyopita, Biblia ilitabiri kwamba “katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Siku za mwisho wa nini? Sio wa dunia au wanadamu, bali ni mwisho wa migogoro, ukandamizaji, na mateso ambayo wanadamu wamekabili kwa maelfu ya miaka. Acheni tuchunguze baadhi ya unabii unaotaja ishara za “siku za mwisho.”

2 Timotheo 3:1-5: “Katika siku za mwisho. . . , watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu, wakionekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake.”

Je, si ni kweli kwamba watu wengi zaidi katika siku zetu wana tabia za aina hiyo? Je, umetambua kwamba tumezungukwa na watu wanaojipenda sana, wanaopenda pesa, na wanaoongozwa na kiburi? Watu pia wanataka watimiziwe mengi na hawataki makubaliano na wengine, sivyo? Na bila shaka umegundua kwamba watoto wengi si watiifu kwa wazazi wao na watu kwa ujumla wanapenda raha kuliko wanavyompenda Mungu. Na mambo yanazidi kuzorota kila kunapokucha.

Mathayo 24:6, 7: “Mtasikia kuhusu vita na habari za vita. . . . Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.”

Inakadiriwa kwamba zaidi ya watu milioni 100 wameuawa kwenye vita na mapigano tangu mwaka wa 1914. Hicho ni kiwango kinachozidi idadi ya watu katika nchi nyingi. Hebu wazia majonzi, huzuni, na mateso yaliyosababishwa na vifo vyote hivyo! Je, mataifa yamejifunza chochote kutokana na vita hivyo na kuacha kupigana?

Mathayo 24:7: “Kutakuwa na upungufu wa chakula.”

Shirika la Chakula Ulimwenguni lilisema hivi: “Ingawa chakula kinachozalishwa duniani kinatosha kuwalisha wanadamu wote, bado watu milioni 815, yaani mtu mmoja kati ya watu tisa, hulala njaa kila siku. Na zaidi ya hayo, mtu mmoja kati ya watatu ana utapiamlo.” Inakadiriwa kwamba watoto milioni tatu hivi hufa kila mwaka kutokana na njaa.

Luka 21:11: “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi.”

Kila mwaka, matetemeko ya ardhi yapatayo 50,000 ambayo ni makubwa kiasi cha wanadamu kuhisi mtikisiko wake, hutokea. Matetemeko 100 hivi kati ya hayo yana uwezo wa kuharibu majengo kwa kiasi kikubwa, na angalau tetemeko moja kubwa sana hutokea kila mwaka. Inakadiriwa kwamba kati ya mwaka wa 1975 na 2000, matetemeko ya ardhi yalisababisha vifo vya watu 471,000.

Mathayo 24:14: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”

Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni nane, wamekuwa wakihubiri na kutoa ushahidi kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu duniani kote katika nchi 240 hivi. Wanahubiri habari njema kwenye majiji makubwa na vijijini, na mahali pengine popote ambapo watu wanapatikana iwe ni kwenye misitu au milimani. Unabii unasema kwamba kazi hiyo itakapokamilika na Mungu awe ameridhika nayo ‘ule mwisho utakuja.’ Mwisho wa nini? Mwisho wa utawala wa wanadamu na mwanzo wa utawala mwingine, Ufalme wa Mungu. Ufalme wa Mungu utatimiza ahadi zipi? Tafadhali soma makala inayofuata ili upate jibu.