Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Usio na Kuteseka—Ahadi Ambayo Inategemeka

Ulimwengu Usio na Kuteseka—Ahadi Ambayo Inategemeka

Ulimwengu Usio na Kuteseka​—Ahadi Ambayo Inategemeka

“[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

JE, AHADI hiyo yenye kugusa moyo inaweza kutegemeka? Fikiria moja ya maonyo ya mapema zaidi ambayo mwanadamu alipewa. Mungu alimwambia Adamu kwamba asipomtii, ‘atakufa hakika.’ (Mwanzo 2:17) Na hivyo ndivyo ilivyotukia, kama tu Mungu alivyokuwa amesema. Kifo na kuteseka ambako wanadamu wamerithi kunathibitisha kwamba Mungu anaweza kutegemeka. Je, tuna sababu yoyote ya kutilia shaka ahadi ya Mungu kwamba atarudisha tena hali kamilifu duniani?

Kumbuka pia sifa za Mungu ambazo zilizungumziwa katika habari iliyotangulia. Tamaa yetu ya kukomesha kuteseka inaonyesha tuna sifa za huruma, upendo, na haki kama tu zile ambazo Mungu anazo. Isitoshe, matukio ya ulimwengu na mitazamo tunayoona leo inathibitisha kwamba wakati wa Mungu wa kuchukua hatua unakaribia sana.—Ona sanduku  “Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

Kwa nini Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi kukomesha kuteseka? Fikiria jinsi ambavyo yeye—akimtumia Mwana wake Yesu—anaweza na amepanga kuondoa visababishi vikuu vya kuteseka.

Uamuzi wa kibinafsi. Babu yetu Adamu alifanya uamuzi mbaya ambao uliwaletea wazao wake wote matatizo mabaya sana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Suluhisho ambalo Mungu atatoa ni la haki, rehema, na rahisi. Waroma 6:23 inaeleza hivi: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”

Mwanadamu mkamilifu Yesu aliishi bila kufanya dhambi. Kifo chake kwenye mti wa mateso kilikuwa msingi wa kukombolewa kwa wanadamu watiifu kutoka kwa laana ya dhambi na kifo. Sasa tuna tumaini la kuishi milele katika ulimwengu ambamo hakutakuwa na mwelekeo wenye dhambi wa kufanya maamuzi yasiyofaa. Pia, watu wanaowatesa wengine hawatakuwapo, kwa kuwa “watenda-maovu watakatiliwa mbali.”—Zaburi 37:9.

Matukio yasiyotazamiwa na kutokamilika. Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, ana uwezo wa kudhibiti nguvu za asili za dunia. Katika karne ya kwanza W.K., Yesu na mitume wake walikuwa ndani ya mashua ya uvuvi wakati ambapo kulitokea “dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi, na mawimbi yakawa yakiipiga mashua kwa nguvu, hivi kwamba karibu mashua ifunikwe na maji.” Mitume walipomwita aje kuwasaidia, Yesu “akaamka, akaukemea upepo na kuiambia bahari: ‘Nyamaza, utulie!’ Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.” Mitume wake wakaogopa. Wakasema: “Hata upepo na bahari zinamtii.”—Marko 4:37-41.

Chini ya utawala wa Yesu, wanadamu watiifu ‘watakaa salama wala hawatasumbuliwa na hofu ya msiba.’ (Methali 1:33) Hiyo inatia ndani misiba ya asili. Isitoshe, dunia haitatumiwa vibaya, hakutakuwa na mbinu zisizo salama za ujenzi, na watu hawatapuuza nguvu za asili za dunia. Hakuna mtu yeyote atakayeteseka kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.

Yesu alipokuwa hapa duniani, alionyesha njia nyingine ambayo utawala wake utaondoa kuteseka kunakosababishwa na matukio yasiyotazamiwa. Alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Naam, Yesu ana nguvu na anatamani kuwafufua mamilioni ya watu waliokufa kutokana na misiba ya asili. Je, ahadi hiyo inategemeka? Yesu alitupa sababu ya kuwa na imani yenye nguvu kwa kuwafufua wafu alipokuwa hapa duniani. Visa vitatu vya ufufuo huo vimeandikwa katika Biblia.—Marko 5:38-43; Luka 7:11-15; Yohana 11:38-44.

“Mtawala wa ulimwengu huu.” Kristo Yesu amewekwa rasmi na Mungu “apate kumwangamiza yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.” (Waebrania 2:14) Yesu alitangaza hivi: “Ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” (Yohana 12:31) Yesu ‘atazivunja kazi za Ibilisi’ kwa kuondoa uvutano wa Ibilisi katika shughuli za ulimwengu. (1 Yohana 3:8) Hebu wazia jinsi jamii ya wanadamu itakavyokuwa tofauti wakati ambapo hakutakuwa tena na roho ya Ibilisi inayochochea pupa, ufisadi, na ubinafsi!

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

 “Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

Wafuasi wa Yesu walimwuliza hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Jibu la Yesu, pamoja na maandiko mengine yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo yaliandikwa baada ya kifo cha Yesu, yanatuambia kile ambacho kitatukia wakati wa Mungu kukomesha kuteseka utakapokaribia. * Linganisha unabii mbalimbali ulio hapa chini na hali na mitazamo tunayoona leo.

● Vita ulimwengu poteMathayo 24:7; Ufunuo 6:4.

● Njaa na magonjwaLuka 21:11; Ufunuo 6:5-8.

● Kuiharibu duniaUfunuo 11:18.

● “Wenye kupenda pesa”2 Timotheo 3:2.

● “Wasiotii wazazi”2 Timotheo 3:2.

● “Wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu”2 Timotheo 3:4.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kuona kwamba ulimwengu usio na kuteseka unakaribia sana. Wasiliana na Mashahidi katika eneo lenu. Watafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe nyumbani kwako au mahali pengine panapokufaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kwa habari zaidi, ona sura ya 9 yenye kichwa “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.