Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nimshtaki Rafiki Yangu?

Je, Nimshtaki Rafiki Yangu?

Vijana Huuliza

Je, Nimshtaki Rafiki Yangu?

“Ilikuwa vigumu sana. Alikuwa rafiki yangu mkubwa.”—James. *

“Mwanzoni, mambo yalikuwa magumu kwelikweli. Wenzangu walinitenga kwa sababu niliwashtaki.”—Ann.

BIBLIA inasema: “Kuna . . . rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Je, umempata rafiki kama huyo? Ikiwa ndivyo, umepata kitu cha thamani.

Lakini vipi ikiwa rafiki anayedai kuwa Mkristo anafanya kosa? Kwa mfano, namna gani ikiwa amejihusisha na ukosefu wa maadili katika ngono, amevuta sigara, ametumia kileo kabla ya kufikia umri unaoruhusiwa, ametumia dawa za kulevya, au amefanya dhambi nyingine nzito? (1 Wakorintho 6:9, 10; 1 Timotheo 1:9, 10) Unapaswa kufanya nini? Je, umwambie unajua kosa alilofanya? Je, uwaambie wazazi wako? Uwaambie wazazi wake? Au umwambie mzee wa kutaniko? * Ukimshtaki, urafiki wenu utakuwaje? Je, ni afadhali kunyamaza tu?

Niseme au Nisiseme?

Kila mtu hukosea. Kwa kweli, Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hata hivyo, watu fulani hufanya dhambi nzito. Wengine ‘hujikwaa katika kosa’ ambalo lisiposhughulikiwa linaweza kuwatumbukiza katika kosa kubwa zaidi. (Wagalatia 6:1) Fikiria mfano halisi ufuatao.

▪ Kijana Mkristo anayeitwa Susan aligundua kwamba rafiki yake ambaye pia ni Mkristo, alikuwa na picha zenye kuamsha hamu ya ngono na muziki wenye maneno machafu katika kituo chake cha Intaneti.

Fikiria hili: Wewe ungefanya nini ikiwa ungekuwa Susan? Je, ungefanya jambo lolote? Au ungesema kwamba kile ambacho rafiki yako anaweka kwenye kituo chake cha Intaneti hakimhusu mtu mwingine yeyote isipokuwa yeye tu? Ikiwa Susan angekuja na kukuomba mawaidha, ungemwambia afanye nini?

․․․․․

Uamuzi wa Susan: Baada ya kufikiria kwa muda, Susan aliamua kuzungumza na wazazi wa rafiki yake. “Niliogopa sana,” anasema, “kwani wao pia ni rafiki zangu wakubwa. Ilikuwa vigumu sana kuwaambia hivi kwamba nikaanza kulia.”

Una maoni gani? Je, Susan alifanya uamuzi mzuri? Au ingekuwa afadhali kama angenyamaza?

Ili kukusaidia kufikia uamuzi unaofaa kuhusu hali hiyo, fikiria mambo yanayofuata:

Rafiki wa kweli angefanya nini? Methali 17:17 inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” Mtu anapochukua hatua zinazopingana na kanuni za Biblia, mtu huyo ‘ana taabu,’ iwe anajua au hajui. Ingawa ni makosa kuwa “mwadilifu kupita kiasi” kwa kufuatilia mambo madogo, rafiki wa kweli hatapuuza mwenendo usio wa Kikristo. (Mhubiri 7:16) Ni kosa kupuuza hali hiyo.—Mambo ya Walawi 5:1.

Namna gani kama ingekuwa wewe? Jiulize: ‘Ikiwa ningekuwa mzazi na mwana au binti yangu awe na kituo cha Intaneti kilicho na picha zinazoamsha hamu ya ngono, je, ningependa kujulishwa? Ningehisi namna gani ikiwa mwana au binti yangu ana rafiki ambaye alijua kinachoendelea lakini hakusema chochote?’

Namna gani kuhusu viwango vya Mungu? Huu si wakati wa kunyamaza. Badala yake, unapaswa kufuata viwango vya Mungu vilivyo katika Biblia. Ukweli ni kwamba unapofanya jambo lililo sawa, unafanya moyo wa Muumba wako ushangilie. (Methali 27:11) Isitoshe, wewe utahisi vizuri ukijua kwamba ulitenda kwa njia inayomfaidi rafiki yako.—Ezekieli 33:8.

“Wakati wa Kusema”

Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:7) Mara nyingi watoto wadogo hawajui kufanya maamuzi yanayofaa. Rafiki yao anapofanya kosa, wanafikiri hivi: ‘Sitaki rafiki yangu apatwe na matatizo’ au ‘Sitaki kuharibu urafiki wetu.’ Ikiwa hayo tu ndiyo mambo ambayo mtu anapaswa kufikiria, basi ingekuwa rahisi kufanya uamuzi, yaani, huo ungekuwa “wakati wa kukaa kimya.”

Hata hivyo unapoendelea kukua, unaanza kufanya maamuzi kwa ukomavu. Unatambua kwamba tayari rafiki yako amepatwa na matatizo na anahitaji msaada, na huenda ukamsaidia. Hata hivyo, ni mambo gani hususa unayoweza kufanya ukisikia kwamba rafiki yako amejihusisha katika mwenendo unaovunja sheria au kanuni za Biblia?

Kwanza, hakikisha kwamba yale ambayo umesikia ni kweli. Huenda ukawa ni uvumi wa uwongo. (Methali 14:15) Kijana anayeitwa Katie anakumbuka: “Rafiki yangu alianza kueneza uwongo kunihusu, na watu waliokuwa marafiki wangu wa karibu walifikiri kwamba alikuwa akisema ukweli. Niliogopa kwamba hakuna mtu ambaye angewahi kuniamini tena!” Biblia ilitabiri kwamba Yesu ‘hangekaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake’—au kama vile tafsiri ya Contemporary English Version inavyosema, ‘hatasikiliza uvumi.’ (Isaya 11:3) Tunajifunza nini? Usiamue haraka kwamba kila kitu unachosikia ni cha kweli. Jaribu kuchunguza kama ni kweli. Fikiria mfano halisi ufuatao.

James, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii alisikia kwamba rafiki yake mkubwa alitumia dawa za kulevya katika karamu.

Fikiria hili: Wewe ungefanya nini ikiwa ungekuwa James? Ungefanya nini ili ujue kwamba yale uliyosikia ni ya kweli?

․․․․․

Uamuzi wa James. Mwanzoni, James alijifanya kuwa hakuwa amesikia chochote wala hakujua lolote. “Kisha dhamiri yangu ikaanza kunisumbua,” anasema. “Nilijua kwamba ningehitaji kumwuliza rafiki yangu kuhusu jambo hilo.”

Una maoni gani? Kuna faida gani za kuzungumza kwanza na mtu ambaye inasemekana alijihusisha na mwenendo usio wa Kikristo?

․․․․․

Ukiona kwamba ni vigumu kuzungumza naye kuhusu jambo hilo, ni jambo gani lingine unaloweza kufanya?

․․․․․

Rafiki ya James alikiri kwamba alitumia dawa za kulevya katika karamu. Lakini alimsihi James asimwambie mtu yeyote. James alitaka kufanya lililo sawa. Lakini pia alitaka rafiki yake afanye jambo linalofaa. Kwa hiyo, alimwambia rafiki yake kwamba angempa juma moja ili awaeleze wazee wa kutaniko lake kuhusu jambo hilo. Ikiwa hangefanya hivyo, basi James angewaeleza.

Je, unafikiria James alitenda kwa haki? Kwa nini unafikiri hivyo?

․․․․․

Rafiki ya James hakuwaeleza wazee, kwa hiyo James akawajulisha. Hata hivyo, baadaye rafiki yake alitambua uzito wa kosa lake. Alisaidiwa na wazee kuona uhitaji wa kutubu na kufanya tena uhusiano mzuri pamoja na Yehova.

Je, Unamsaliti?

Lakini huenda bado ukajiuliza: ‘Si nitakuwa msaliti nikimshtaki rafiki yangu? Je, si ni rahisi zaidi nikitenda kana kwamba sijui jambo lolote?’ Ukijipata katika hali kama hiyo, utafanya nini?

Kwanza, tambua kwamba jambo ambalo mara nyingi ni rahisi kumfanyia rafiki yako huenda lisionyeshe kwamba unampenda, na wakati huohuo huenda isiwe rahisi kufanya jambo linaloonyesha kwamba unampenda. Unahitaji ujasiri ili kumshtaki rafiki yako anapofanya kosa. Kwa nini usisali kwa Mungu kuhusu jambo hilo? Mwombe akupe hekima na ujasiri unaohitaji. Atakusaidia.—Wafilipi 4:6.

Pili, fikiria jinsi utakavyomfaidi rafiki yako kwa kumshtaki. Kwa mfano, fikiria kwamba wewe na rafiki yako mnapanda mlima, kisha rafiki yako anajikwaa na kuanguka mahali anapoweza kuteleza kwa urahisi. Bila shaka, rafiki yako anahitaji msaada. Lakini, namna gani, kwa sababu ya aibu, rafiki yako akikuambia ni afadhali apande kutoka mahali hapo hatari bila msaada? Je, utamwacha ahatarishe uhai wake kwa njia hiyo?

Hali inakuwa vivyo hivyo rafiki anapojikwaa katika njia ya Kikristo. Huenda akahisi kwamba anaweza kupona kiroho bila msaada. Lakini huo ni upumbavu. Ni kweli kwamba huenda rafiki yako akaaibika kwa sababu ya matendo yake. Lakini huenda kilio chako cha kuomba msaada kikaokoa uhai wa rafiki yako!—Yakobo 5:15.

Kwa hiyo, usiogope kusema rafiki yako anapofanya kosa. Kwa kumtafutia msaada, unaonyesha kwamba wewe ni mshikamanifu kwa Yehova Mungu na kwa rafiki yako ambaye huenda siku moja akakushukuru kwa kumsaidia kwa upendo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 6 Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazee hutoa msaada wa kiroho kwa yeyote ambaye ametumbukia katika dhambi nzito.—Yakobo 5:14-16.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kumshtaki rafiki yako anapofanya kosa kunathibitishaje kwamba wewe ni mshikamanifu kwake?

▪ Ni watu gani unaoweza kufikiria katika Biblia ambao ushikamanifu wao kwa rafiki zao ulijaribiwa? Unaweza kujifunza nini kutoka kwao?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Unahitaji kuhakikisha kwamba rafiki yako anapata msaada anapojikwaa katika njia ya Kikristo