Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo Wenye Nguvu Kuliko Kimbunga!

Upendo Wenye Nguvu Kuliko Kimbunga!

Upendo Wenye Nguvu Kuliko Kimbunga!

Mnamo 2005, vimbunga Katrina na Rita vilipokumba pwani ya Marekani inayopakana na Ghuba ya Mexico, vilisababisha uharibifu mkubwa na vifo vingi. Walioathiriwa walitia ndani maelfu ya Mashahidi wa Yehova.

Chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Marekani, halmashauri za kutoa misaada zilianza kuwasaidia watu mara moja. Huko Louisiana, halmashauri hizo zilianzisha vituo 13 vya kutoa misaada, mabohari 9, na vituo 4 vya petroli. Waliwasaidia watu walioishi katika eneo lililo na ukubwa wa kilomita 80,000 za mraba. Karibu Mashahidi 17,000 walijitolea kutoka sehemu mbalimbali za Marekani na nchi nyingine 13 kuandaa msaada wa dharura na kujenga. Matokeo yalionyesha kwamba upendo wa Kikristo ni wenye nguvu kuliko nguvu za asili.—1 Wakorintho 13:1-8.

Wajitoleaji hao walirekebisha zaidi ya nyumba 5,600 za waamini wenzao na Majumba ya Ufalme 90 ambapo Mashahidi wa Yehova hukutania. Hiyo ni idadi ya karibu majengo yote yaliyoharibiwa. Kupatana na andiko la Wagalatia 6:10 ambalo linawahimiza Wakristo ‘wawatendee wote mema,’ Mashahidi wa Yehova waliwasaidia pia watu kadhaa wasioamini.

KUSHIRIKI katika kazi ya kutoa misaada kulihusisha kujidhabihu, hata hivyo, wajitoleaji walipata baraka nyingi. Hebu ona maelezo ya Mashahidi saba waliosimamia sehemu mbalimbali za kazi hiyo.

“Jambo la Pekee Maishani Mwangu”

Robert: Kutumika katika halmashauri ya kutoa msaada kumekuwa jambo la pekee maishani mwangu. Nina umri wa miaka 67, nami ndiye mwenye umri mkubwa zaidi katika halmashauri hiyo. Nilitumika pamoja na kikundi kikubwa cha wajitoleaji kilichotia ndani vijana wengi wenye bidii katika mambo ya kiroho. Ni jambo lenye kutia moyo kama nini kuona vijana wakionyesha upendo wa kujidhabihu kwa Yehova na kwa Wakristo wenzao!

Mke wangu Veronica, amekuwa msaidizi mzuri sana. Ili tuweze kujitolea, aliunga mkono uamuzi wangu wa kuacha kazi niliyokuwa nimefanya kwa zaidi ya miaka 40. Sasa tunafanya kazi ya kusafisha ofisi usiku mmoja kwa juma. Tumejifunza kuishi maisha rahisi. Kufanya kazi pamoja na Mashahidi wenzetu kulifanya tuelewe zaidi kile kinachomaanishwa na kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani. (Mathayo 6:33) Tena na tena, tumeona ya kwamba Yehova huwatunza vizuri watu wake.

Frank: Ninatumika nikiwa mwangalizi wa idara ya chakula kwenye kituo cha kutoa msaada cha Baton Rouge. Mwanzoni, ili kuwalisha wajitoleaji ilibidi tufanye kazi kwa saa 10 hadi 12 kila siku ya juma. Hata hivyo, tulipata baraka nyingi kutia ndani kujionea wenyewe nguvu za upendo wa Kikristo.

Wajitoleaji wengi ambao walisaidia katika idara ya chakula kwa juma moja au zaidi waliomba kurudi tena, na wengine kati yao walituma kadi au kupiga simu ili kuonyesha shukrani zao kwa kupata pendeleo la kusaidia. Mimi na mke wangu Veronica, tumeguswa sana na roho yao ya kujidhabihu.

Alijawa na Msisimuko

Gregory: Mimi na mke wangu Kathy, tuliuza nyumba yetu huko Las Vegas, Nevada kisha tukanunua lori dogo na pia trela tunayotumia kama nyumba. Kurahisisha maisha yetu kumetuwezesha kushiriki katika kazi ya kutoa misaada huko Louisiana kwa zaidi ya miaka miwili. Sasa kuliko wakati mwingine wowote maishani mwetu, tunajionea wenyewe ukweli wa maneno yanayopatikana katika Andiko la Malaki 3:10: “‘Tafadhali, mnijaribu, . . . ’ Yehova wa majeshi amesema, ‘[na mwone] kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’”

Mara nyingi sisi hutabasamu watu wanapotuambia, “Kweli mnajidhabihu sana!” Miaka 30 iliyopita, mimi na Kathy tulitaka kutumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Marekani lakini tulikuwa na watoto. Kazi ya kutoa misaada imetosheleza tamaa yetu ya kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Mungu. Pia, tumepata pendeleo lingine la kufanya kazi kwa ukaribu na Mashahidi wenzetu, na baadhi yao wana ustadi sana. Kwa mfano, mmoja wa wapishi wetu alikuwa mpishi katika mkahawa wa kifahari na mwingine alikuwa mpishi wa marais wawili wa Marekani.

Kwa wajitoleaji wengi, kazi ya kutoa misaada imekuwa na matokeo mazuri maishani mwao. Ndugu mmoja aliye na umri wa miaka 57, alijawa na msisimuko alipoeleza jinsi alivyowasaidia walioathiriwa na vimbunga. Hata Mashahidi wengine ambao hawakuweza kuja kusaidia wametutia moyo sana. Kwa mfano, wajitoleaji wawili ambao huondoa kuvu kwenye nyumba walitupa bango kubwa lililokuwa na sahihi ya kila mtu kutia ndani na watoto kutoka makutaniko matatu ya jimbo la kwao la Nebraska.

‘Tumeona Jinsi Mungu Anavyotunza Nafsi Zilizopondeka’

Wendell: Siku moja baada ya Kimbunga Katrina kutokea, nilipokea ombi kutoka ofisi ya tawi ya Marekani nichunguze Majumba ya Ufalme na nyumba za Mashahidi wa Yehova zilizoharibiwa huko Louisiana na Mississippi. Hivi ndivyo nilivyoanza mgawo mpya na kujifunza mambo mengi. Kwa miaka 32, mimi na mke wangu Janine, tuliishi katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme, na tulijionea waziwazi jinsi Yehova anavyowatunza watu wake. Hata hivyo, sasa tumeona utunzaji wa Mungu kwa kiwango kikubwa hata zaidi.

Nina pendeleo la kutumika nikiwa mwenyekiti katika halmashauri ya kutoa msaada ya Baton Rouge. Licha ya kwamba mgawo huo ni mgumu, nimeridhika sana. Kwa kweli, mara nyingi sana tunapotoa msaada, halmashauri yetu imeona jinsi ambavyo Mungu amethibitika kuwa Baba Mweza-Yote mwenye upendo kwa kutatua matatizo, kufungua njia, na kutunza nafsi zilizopondeka.

Watu wengi wametuuliza hivi: “Wewe na mke wako mmewezaje kushiriki katika kazi ya kutoa misaada kwa zaidi ya miaka miwili?” Haijawa rahisi sikuzote. Imetubidi kufanya mabadiliko mengi katika maisha yetu. Lakini kwa upande mwingine, tumeona faida za kudumisha ‘jicho rahisi.’—Mathayo 6:22.

Tulipoanza kazi ya kuwatafuta na kuwasaidia walioathiriwa huko New Orleans, hatukupumzika vya kutosha. Kuongezea tatizo hilo, jiji lilikuwa na mvurugo na ukatili na ikabidi wanajeshi kutumwa huko. Ilikuwa rahisi kuvunjika moyo tulipoona kazi nyingi iliyotungojea.

Tulikutana na maelfu ya Mashahidi walioathiriwa. Tulisali pamoja nao na tukajaribu kuwafariji. Kisha kwa msaada wa Yehova tukaanza kazi. Kutokana na mambo ambayo nimepitia, ninahisi ni kana kwamba nimeishi maisha mawili tofauti kwa miaka miwili ambayo nimekuwa hapa.

Mara kwa mara, nilipohisi nimechoka sana kimwili na kihisia, wajitoleaji wapya waliwasili, wengine kwa miezi kadhaa, wengine kwa muda mrefu zaidi. Nimeimarishwa sana ninapoona wasaidizi wengi wenye furaha na walio tayari kufanya kazi, kutia ndani vijana wengi.

Mara nyingi, Yehova alitusaidia. Kwa mfano, tulipowasili tuligundua kwamba miti ilikuwa imeangukia zaidi ya nyumba 1,000 za ndugu zetu. Kwa sababu hatukuwa na vifaa wala watu wa kufanya kazi hatari ya kuondoa miti hiyo, halmashauri yetu ilisali kuhusu jambo hilo. Siku iliyofuata, ndugu aliyekuwa na lori na mashine tuliyohitaji alijitolea kusaidia. Pindi nyingine sala yetu ilijibiwa baada ya dakika 15 tu, na wakati mwingine, kifaa tulichohitaji kilianza kusafirishwa hata kabla ya kumaliza sala yetu! Naam, Yehova amethibitika kuwa “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.

‘Najivunia Kuwa Mmoja wa Mashahidi wa Yehova’

Matthew: Siku moja baada ya Kimbunga Katrina kutokea, nilisaidia kupanga ili tani 15 za chakula, maji, na vitu vingine vilivyohitajika vipelekwe kwenye maeneo yaliyoathiriwa. Watu wa Yehova walithibitisha kwamba wao ni wakarimu kwelikweli!

Ili jitihada zetu zifanikiwe zaidi, mimi na mke wangu Darline, tulihamia eneo lililo umbali wa saa mbili kwa mwendo wa gari kutoka eneo lililoathiriwa. Shahidi fulani wa eneo hilo alitupa kazi ya muda ili tuweze kutumia wakati wetu mwingi katika kazi ya kutoa msaada. Shahidi mwingine alitupa makao. Moyo wangu hujaa uthamini kwa kuwa sehemu ya undugu huo wenye upendo na hilo hunifanya nijivunie kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Ted: Muda mfupi baada ya Kimbunga Katrina kutokea, mimi na mke wangu Debbie, tulijitolea kusaidia. Baada ya siku chache, tulipata trela yenye urefu wa mita tisa iliyoweza kuvutwa na lori yetu. Sala yetu ilijibiwa kwani trela hiyo iliuzwa kwa nusu ya bei ya kawaida na hivyo tungeweza kuinunua. Tumeishi katika trela hiyo kwa zaidi ya miaka miwili.

Kazi ilipopungua, tuliuza nyumba yetu na vitu vyetu vingi na hivyo kuwa tayari kwa kazi zaidi huko New Orleans ambako ninatumika nikiwa mratibu wa miradi. Jambo kuu ambalo tumeona ni kwamba Yehova amethibitika kuwa “Mungu wa faraja yote” kwa waabudu wake. Wengi hawakuwa wamepoteza tu nyumba zao na Majumba ya Ufalme, bali pia kwa sababu ya kuhamishwa, walilazimika kuacha makutaniko yao na hata eneo lote walilokuwa wakihubiri habari njema.—2 Wakorintho 1:3.

‘Imani Yao Ilitugusa Moyo’

Justin: Oktoba 2005, kulikuwa na ombi la wajitoleaji wa kutoa msaada katika pwani ya Marekani inayopakana na Ghuba ya Mexico. Mara moja, mimi na mke wangu Tiffany, tulituma ombi letu na Februari (Mwezi wa 2) 2006, tuliombwa tusaidie kikundi cha kuezeka paa kilichokuwa katika kituo cha kutoa msaada cha Kenner, karibu na New Orleans.

Kila siku tulifanya kazi ya ujenzi katika nyumba fulani na kukutana na Mashahidi wa huko, ambao imani na tegemeo lao katika Mungu lilitugusa moyo. Na kila siku mambo mengi yalitukumbusha upumbavu wa kutegemea vitu vya kimwili. Ni vigumu kueleza shangwe tuliyopata kutokana na kuona kile ambacho Yehova amewawezesha watu wake kutimiza na vilevile katika kuwasaidia Wakristo wenzetu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

Siku Katika Kituo cha Kutoa Msaada

Kazi ya wafanyakazi wa jikoni katika kituo cha kutoa msaada huanza saa 10:30 hivi alfajiri. Saa 1:00 asubuhi wafanyakazi wote hukusanyika kwenye sehemu ya kulia chakula kwa ajili ya kuchunguza Andiko la siku kwa dakika kumi kabla ya kula kiamsha-kinywa. Mwenyekiti anaweza kutumia pindi hiyo kuwakaribisha wafanyakazi wapya na kueleza jambo lililoonwa la karibuni lenye kutia moyo.

Baada ya kutoa sala ya shukrani, wote hufurahia chakula kizuri na kwenda kazini. Wengine hubaki kwenye kituo ili wafanye kazi katika ofisi, dobi, au jikoni. Wapishi hutayarisha chakula cha mchana ambacho kitachukuliwa saa sita na kupelekwa na mwakilishi wa kila kikundi kwa ajili ya wajitoleaji wanaofanya kazi mbali na kituo.

Kila Jumatatu (Siku ya 1) jioni “familia” hiyo hukusanyika kwa ajili ya funzo la Biblia linalotegemea makala katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Mafunzo kama hayo huwasaidia wote wadumu wakiwa imara kiroho, na hiyo ndiyo siri ya kudumisha shangwe na kuendelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu kazi yao.—Mathayo 4:4; 5:3.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

“Niliwaelewa Vibaya”

Mwanamke mmoja huko New Orleans alikuwa amebandika tangazo hili mlangoni pake: “Mashahidi wa Yehova Msibishe Mlango Wangu.” Kisha siku moja wajitoleaji wakaanza kurekebisha nyumba ya jirani iliyokuwa imeharibiwa na kimbunga. Kila siku aliona uchangamfu na urafiki wa wafanyakazi hao. Udadisi wake ulimchochea aende kuchunguza walichokuwa wakifanya. Alipogundua kwamba wajitoleaji hao walikuwa Mashahidi wa Yehova, alisema hakuna hata mtu mmoja wa kanisa lake aliyekuwa amempigia simu tangu kimbunga hicho kilipotokea. “Ni wazi kwamba niliwaelewa vibaya,” akasema. Matokeo yakawaje? Aliondoa tangazo lake mlangoni na kuwaambia Mashahidi kwamba wanaweza kumtembelea.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Robert na Veronica

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Frank na Veronica

[Picha katika ukurasa wa 17]

Gregory na Kathy

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wendell na Janine

[Picha katika ukurasa wa 18]

Matthew na Darline

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ted na Debbie

[Picha katika ukurasa wa 18]

Justin na Tiffany