Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova, tafadhali niruhusu nikutumikie”

“Yehova, tafadhali niruhusu nikutumikie”

“Yehova, tafadhali niruhusu nikutumikie”

Imesimuliwa na Danielle Hall

Nilipokuwa msichana mdogo, nilipenda kumtembelea Nyanya, ambaye aliishi karibu nasi. Kila alasiri alikuwa akipumzika. Ikiwa ningemtembelea wakati huo, tungeketi kitandani na angenisomea hadithi za Biblia. Mara nyingi angeniambia: “Usisahau kamwe kwamba Yehova anakupenda. Ukimpenda, atakutunza sikuzote.” Maneno hayo yalikaziwa sana akilini na moyoni mwangu.

NYANYA alikufa mnamo 1977, nilipokuwa na miaka minne. Kama wengi wa familia ya Baba walioishi mji wa Moe, Australia, nyanya pia alikuwa Shahidi wa Yehova. Wazazi wangu hawakuwa Mashahidi wa Yehova, lakini Baba aliwapenda. Baadaye, familia yetu ilihamia mji mdogo wa Tintenbar, karibu na pwani ya New South Wales. Mimi, Baba, na kaka yangu, Jamie, tulihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova.

Nilipokuwa na miaka minane, wazazi wangu walitengana. Baba alirudi Moe, lakini mimi na Jamie tulibaki na Mama. Mama hakupendezwa na Biblia na hakutaka tuhudhurie mikutano ya Mashahidi. Jambo hilo lilinihuzunisha sana. Nilifikiria maneno ya Nyanya ambayo yalinigusa sana moyo. Nilijua kwamba ninampenda Yehova! Nilitaka kumtumikia. Nilisali na kumwomba Yehova niwe mmoja wa Mashahidi wake. Naye Jamie alihisi vivyo hivyo.

Majaribu Shuleni

Baada ya muda fulani, mwalimu aliwauliza watoto wote wataje dini zao ili aziandike kwenye kitabu. Jamie alipoulizwa, alisema kwa sauti kubwa, “Mimi ni Shahidi wa Yehova.” Mwalimu alitua na kumwomba arudie jibu lake, naye akafanya hivyo. Mwalimu akasema, “Sidhani hiyo ni kweli, lakini nitazungumza nawe baadaye.” Nilipoulizwa, mimi pia nilisema, “Mimi ni Shahidi wa Yehova.” Akiwa amekata tamaa, mwalimu alimwita mwalimu mkuu.

Mwalimu mkuu alisema hivi kwa uthabiti: “Hizi ndizo fomu zenu za kuandikishwa shule, na wazazi wenu hawakuwaandikisha ninyi kama Mashahidi wa Yehova.” Tulijibu hivi kwa heshima: “Lakini hiyo ndiyo dini yetu.” Hakuna yeyote kati yao aliyeuliza jambo hilo tena.

Nilipokuwa shuleni, niliwaeleza wenzangu mambo niliyokuwa nimejifunza katika Biblia. Mara kwa mara nilibeba nakala ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na mara kwa mara niliweza kumsomea hadithi msichana mmoja ambaye alimwamini Mungu. * Lakini kwa kuwa nilijitahidi kuishi kulingana na viwango vya Kikristo, sikuwa na marafiki wengi na nyakati nyingine nilijihisi mpweke.

Nilisali kwa Yehova mara nyingi sana na kwa bidii hivi kwamba akawa rafiki yangu wa karibu. Kila siku baada ya shule, niliketi kitandani na kumweleza Yehova mambo yote yaliyotukia siku hiyo, bila kuacha hata mambo madogo. Nililia mara nyingi. Nilimsihi Yehova huku machozi yakitiririka kwenye mashavu yangu, “Yehova tafadhali, niruhusu nikutumikie pamoja na watu wako.” Kila mara baada ya kusali, nilihisi nafuu zaidi.

Barua Yenye Kutia Moyo

Nilipokuwa na miaka kumi, Jamie alirudi Moe ili aishi na Baba. Sasa nilijihisi mpweke kiroho hata zaidi. Kisha nilipokuwa nikimtembelea jirani mmoja, nilipata magazeti ya Mashahidi wa Yehova. Kwa msisimko nilikariri anwani ya ofisi ya tawi ya kwetu, kisha nikakimbia nyumbani kuiandika. Niliandikia ofisi ya tawi barua ya kutoka moyoni nikiwaeleza hali yangu na kuwaomba msaada wa kiroho. Macho yangu yalijawa na machozi niliposoma jibu lao lenye kugusa moyo lililoandikwa kwenye kurasa mbili hasa kwa ajili yangu. Huu ulikuwa uthibitisho kwamba Yehova ananithamini!

Barua hiyo ilinisihi niige imani ya msichana Mwisraeli ambaye alikuwa mtumishi wa Naamani, mwanajeshi Msiria wa nyakati za Biblia. Ingawa alikuwa mfungwa na aliishi mbali sana na nyumbani kwao, alikaa karibu na Mungu wake Yehova. Kwa kuzungumza kwa ujasiri kuhusu imani yake, alijionyesha kuwa shahidi wa kweli wa Yehova.—2 Wafalme 5:1-4.

Barua hiyo iliendelea kusema: “Kwa kuwa wewe ni msichana mdogo, unapaswa kumtumikia Yehova kwa kuwatii wazazi wako na kufanya bidii shuleni. Pia unahitaji kumkaribia Yehova kwa sala na kwa kujifunza.” Kwa kumalizia barua hiyo ilisema: “Danielle kumbuka kwamba hata tuwe wapi, Yehova yuko karibu nasi. Tunajua unaamini hilo.” (Waroma 8:35-39) Ingawa barua hiyo imezeeka na kuchakaa, nimeiweka ndani ya Biblia yangu. Nimeisoma mara nyingi, lakini kila mara ninapoisoma machozi yananitoka.

Muda mfupi baada ya hapo, nilipata barua nyingine. Ilisema kwamba baba yangu alikuwa amepanga niwe nikipokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kupitia posta. Nilifurahi kama nini! Sasa ningeweza kupata chakula cha kiroho kwa ukawaida. Nilisoma kila gazeti lilipofika, kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa mwisho. Bado nina magazeti hayo yenye thamani niliyotumiwa kwanza. Wakati huohuo, mzee Mkristo kwenye kutaniko la eneo hilo, alianza kunitembelea. Ingawa alinitembelea kwa muda mfupi, ziara zake zilinitia moyo sana.

Mabadiliko Yatokeza Maendeleo

Licha ya kwamba hali yangu ya kiroho ilikuwa afadhali kuliko mwanzoni, bado nilitamani kumwabudu Yehova kwa uhuru. Kwa hiyo nilipofikia umri wa miaka 13, nilimwomba Mama aniruhusu nikaishi na Baba. Nilimpenda sana Mama, naye alinipenda sana, lakini nilikuwa nimeazimia kumtumikia Mungu. Alipokubali, nilirudi Moe na nikaanza kujifunza Biblia. Baba aliniruhusu mimi na Jamie tuhudhurie mikutano. Mashahidi walijitolea kutusaidia kwa hali na mali. Mimi na Jamie tulifanya maendeleo ya kiroho na tukabatizwa kukiwa na tofauti ya miezi michache tu kati yetu. Naam, sala niliyotoa nilipokuwa mtoto ilijibiwa. Nilikuwa nikimtumikia Yehova pamoja na watu wake!

Wakati huohuo, nilianzisha urafiki wa karibu na mjomba Philip na shangazi, Lorraine Taylor, ambao pia walikuwa kwenye kutaniko hilohilo la Moe. Walinitendea kama binti yao. Waliponikaribisha niende nao kwenye kisiwa cha Bougainville, huko Papua New Guinea, walikokuwa wanaenda kutumikia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, nilikubali mara moja mwaliko wao. Nilikuwa na umri wa miaka 15 tu lakini Baba na Mama waliniruhusu niende.

Huko Bougainville niliendelea na masomo yangu kwa njia ya posta. Lakini niliutumia muda wangu mwingi kuhubiri. Jinsi nilivyofurahia kuhubiri na wamishonari na mapainia! Watu tuliokutana nao walikuwa wanyenyekevu sana na wengi wao walitaka kujifunza Biblia.

Mwishoni mwa mwaka huohuo, kukawa na msukosuko wa kisiasa na hali ikawa mbaya sana, hivyo singeweza kukaa huko tena. Ilinivunja moyo kuondoka kisiwa hicho kidogo na kuacha watu wake wenye kupendeza. Ndege yetu ndogo ilipoanza kupaa, nilimwona Mjomba Philip akinipungia mkono. Huku nikilia sana, nilimwomba Yehova aniruhusu nimtumikie kama mmishonari katika nchi ya kigeni.

Sala Zaidi Zajibiwa

Huko Australia, baada ya kumaliza masomo ya sekondari, nilianza kujifunza kazi kwenye shirika fulani la sheria. Wakati huohuo, Baba alikuwa ameoa tena na alikuwa akitunza familia kubwa ya mama wa kambo. Naye Jamie alikuwa akiishi na Mama. Kwa muda fulani, nilitanga-tanga kati ya wazazi hao wawili na jambo hilo lilifanya maisha yangu yawe magumu sana. Nilihitaji kufanya maisha yangu yawe sahili ili nikazie fikira miradi ya kiroho. Kwa hiyo mwaka wa 1994, nilianza utumishi wa wakati wote huko Moe kama painia.

Nilikuwa na furaha tena. Rafiki zangu walikuwa vijana wa kiroho katika kutaniko, nao walinitegemeza sana. Naam, mnamo 1996 nilipata baraka kutoka kwa Yehova ya kuolewa na mmoja wao ambaye aliitwa Will. Ndugu huyo alikuwa mtu mpole, mwenye fadhili, na mnyenyekevu.

Tulianza maisha yetu ya ndoa, nasi tulikuwa na furaha nyingi. Siku moja, Will alirudi nyumbani baada ya kwenda shambani na mwangalizi anayesafiri ambaye alikuwa anazungukia makutaniko katika eneo letu. Aliniketisha chini na kuniuliza, “Je, ungependa kuhama ukasaidie kutaniko lingine?” Moyoni mwangu nilisema ndiyo mara moja. Lakini nilimwuliza kwa utani, “Wapi? Vanuatu? Au Fiji?” Will alijibu: “Morwell,” nami nikasema, “Lakini hilo si ni kutaniko jirani!” Sote tulicheka na kukubaliana kwamba tungependa kuhamia kutaniko hilo jirani na kutumika tukiwa mapainia.

Miaka mitatu iliyofuata tukiwa Morwell ilikuwa mizuri na yenye matokeo. Kisha jambo lingine la kushangaza likatokea. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia ilitualika tutumikie kama mapainia wa pekee. Mgawo wetu ungekuwa wapi? Timor Mashariki, nchi ndogo upande wa mashariki wa visiwa vya Indonesia. * Macho yangu yalifurikwa na machozi. Nilimshukuru Yehova kwa kujibu sala zangu zote. Zaidi ya kuniruhusu niwe mtumishi wake, aliniruhusu mimi pamoja na mume wangu tutumikie katika nchi ya kigeni.

Kutumika Katika Nchi ya Ng’ambo

Mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2003, tuliwasili huko Dili, ambao ni mji mkuu. Kutaniko la Dili, ambalo ndilo kutaniko pekee nchini humo, lilikuwa na mapainia wa pekee 13 kutoka Australia na mashahidi wengine wachache wa eneo hilo. Ndugu na dada Watimori ni maskini sana, wengi wao walikuwa wamepoteza vitu vyao vya kimwili na pia watu wa familia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe, vilivyochukua miaka 24 na kuisha mnamo 1999. Wengi pia wamevumilia upinzani wa familia kwa sababu ya imani yao mpya. Licha ya matatizo yao na umaskini, wao ni matajiri kiroho na wana furaha.—Ufunuo 2:8, 9.

Tuligundua kwamba Watimori wengi walimwogopa Mungu na kuiheshimu Biblia. Muda si muda, tukawa na mafunzo ya Biblia mengi kuliko yale tuliyoweza kuyashughulikia! Baada ya muda, wanafunzi wetu wa kwanza walijiunga nasi wakiwa ndugu na dada waliobatizwa. Kuona maendeleo yao ya kiroho kulituletea furaha kubwa sana.

Mnamo 2006, kukawa na msukosuko tena katika jiji la Dili. Migogoro kati ya makabila mbalimbali ilitokeza vita. Watu walipora na kuchoma nyumba nyingi, nao Mashahidi wenyeji wakakimbilia usalama katika nyumba za mapainia wa pekee. Nyumba yetu na kiwanja chake iligeuzwa kuwa kambi ya muda ya wakimbizi, na wakati mmoja karibu watu 100 waliishi pamoja nasi! Gereji yetu ilitumiwa kama jiko, chumba cha kulia chakula, na Jumba la Ufalme la muda.

Ingawa tulisikia milipuko ya risasi na gruneti, nyumba yetu ilikuwa na amani. Sote tulihisi kwamba Yehova anatulinda. Kila siku tulianza kwa kuzungumzia Andiko fulani. Tulifanya mikutano kama kawaida. Pia tuliongoza mafunzo ya Biblia na watu waliopendezwa.

Baada ya majuma kadhaa, tuligundua kwamba ilikuwa hatari kwa akina ndugu waliozaliwa sehemu ya mashariki ya nchi hiyo kuendelea kuishi katika jiji la Dili. Kwa hiyo, akina ndugu wanaoongoza waliamua kuanzisha kikundi kipya huko Baucau, jiji kubwa la pili, mwendo wa saa tatu mashariki ya Dili. Na hiyo ndiyo sababu mimi na Will, tulipata mgawo mpya.

Mnamo Julai 2006, miaka mitatu hivi baada ya sisi kuingia Timor Mashariki, tuliwasili Baucau. Kikundi chetu kipya kilikuwa na mapainia wa pekee wanne na Mashahidi sita Watimori. Ingawa ndugu na dada hao wenyeji walikuwa wameacha kila kitu huko Dili, bado waliweza kutabasamu. Kwa kweli tulipendezwa na roho yao ya uaminifu na kujidhabihu!

Bado mimi na Will tunatumika mjini Baucau. Tunafurahia mgawo wetu na kuuona kama baraka nyingine kutoka kwa Yehova. Ninapokumbuka yaliyopita ninaona Nyanya hakuwa amekosea. Yehova amenitunza miaka hiyo yote. Kila mara ninamshukuru kwa kuniruhusu niwe na pendeleo la kumtumikia pamoja na watu wake. Pia ninatamani sana kumwona Nyanya kwenye ufufuo. Kisha ninaweza kumshukuru kwa kunionyesha njia ya kupata maisha yenye furaha na yenye kuthawabisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 25 Ingawa katika Kiswahili nchi hiyo inaitwa Timor Mashariki, inaitwa pia Timor-Leste.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Nyanya

[Picha katika ukurasa wa28, 29]

Nikiwa na mume wangu, Will