Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waroma 12:12​—“Kwa Tumaini, Mkifurahi; Katika Dhiki, Mkisubiri; Katika Kusali, Mkidumu”

Waroma 12:12​—“Kwa Tumaini, Mkifurahi; Katika Dhiki, Mkisubiri; Katika Kusali, Mkidumu”

 “Shangilieni katika tumaini. Vumilieni chini ya dhiki. Dumuni katika sala.”—Waroma 12:12, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu.”—Warumi 12:12, Union Version.

Maana ya Waroma 12:12

 Katika mstari huu, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waliokuwa Roma wafanye mambo matatu ambayo yangewasaidia kubaki waaminifu ikiwa wangeteswa au kukabili matatizo mengine.

 “Shangilieni katika tumaini.” Wakristo wana tumaini zuri la kupata uzima wa milele—wachache mbinguni lakini wengi katika paradiso duniani. (Zaburi 37:29; Yohana 3:16; Ufunuo 14:1-4; 21:3, 4) Tumaini hilo linahusisha kuona Ufalme wa Mungu a ukiondoa matatizo yote yanayowakabili wanadamu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Waabudu wa Mungu wanaweza kushangilia hata wanapokabili matatizo, kwa sababu wanasadiki kwamba tumaini lao ni hakika na kwamba wakiendelea kuvumilia watapata kibali cha Mungu.​—Mathayo 5:11, 12; Waroma 5:3-5.

 “Vumilieni chini ya dhiki.” Katika Biblia kitenzi cha Kigiriki kilichotafsiriwa “vumilia” mara nyingi hutumiwa kumaanisha “kusimama badala ya kukimbia; kustahimili; na kubaki imara.” Wafuasi wa Kristo ‘si sehemu ya ulimwengu’ b hivyo wanatarajia kuteswa na wanahitaji uvumilivu. (Yohana 15:18-20; 2 Timotheo 3:12) Mkristo anapomtumikia Mungu kwa ushikamanifu hata inapohusisha kuvumilia majaribu, imani yake kwamba hatimaye Mungu atamthawabisha inaimarishwa. (Mathayo 24:13) Usadikisho huo unamsaidia kuvumilia matatizo kwa subira na shangwe.​—Wakolosai 1:11.

 “Dumuni katika sala.” Ili kubaki waaminifu kwa Mungu, Wakristo wanatiwa moyo kuendelea kusali tena na tena. (Luka 11:9; 18:1) Kila wakati wanatafuta mwongozo wa Mungu na kumtegemea katika sehemu zote za maisha. (Wakolosai 4:2; 1 Wathesalonike 5:17) Wana uhakika kwamba Mungu atajibu maombi yao kwa sababu wanafanya yote wawezayo ili kumpendeza. (1 Yohana 3:22; 5:14) Wanajua kwamba wakidumu katika sala Mungu atawapa nguvu wanazohitaji ili kuvumilia hata wakikabili majaribu ya aina gani.​—Wafilipi 4:13.

Muktadha wa Waroma 12:12

 Paulo aliwaandikia barua hii Wakristo walioishi Roma mwaka wa 56 W.K hivi. Katika sura ya 12 ya barua hii, anatoa ushauri mzuri wa jinsi ya kuonyesha sifa za Kikristo, jinsi ya kushughulika na waamini wenzetu na watu wengine, na jinsi ya kutenda kwa amani tunapoteswa. (Waroma 12:9-21) Ushauri huo ulitolewa kwa wakati unaofaa kwa Wakristo walioishi Roma kwa sababu baada ya muda mfupi tu wangekabili mateso makali.

 Miaka michache baadaye, katika mwaka wa 64 W.K. moto mkubwa uliteketeza sehemu kubwa ya jiji la Roma. Watu wengi walisema kwamba Maliki Nero ndiye aliyekuwa ameanzisha moto huo. Kulingana na Tacitus, mwanahistoria Mroma, Nero alijaribu kujilinda mwenyewe kwa kuwalaumu Wakristo. Hilo lilianzisha mateso makali dhidi ya Wakristo. Ushauri ambao Paulo aliwapa kuhusu kuvumilia mateso, uliwasaidia kuvumilia kipindi hicho kigumu wakiwa na amani na utulivu. (1 Wathesalonike 5:15; 1 Petro 3:9) Waabudu wa Mungu leo wanaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wao.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Waroma.

a Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni iliyoanzishwa na Mungu mwenyewe ili kutekeleza mapenzi yake hapa duniani. Kwa habari zaidi soma makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu ni Nini?

b Katika Biblia, neno “ulimwengu” linaweza kumaanisha jamii ya wanadamu ambayo imejitenga na Mungu.