Hamia kwenye habari

Je, Ni Sawa Kusali kwa Watakatifu?

Je, Ni Sawa Kusali kwa Watakatifu?

Jibu la Biblia

 Hapana. Biblia inaonyesha kwamba tunapaswa kusali kwa Mungu peke yake, kupitia jina la Yesu. Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kusali: Baba yetu uliye mbinguni: Jina lako litukuzwe.” (Mathayo 6:9, Biblia Habari Njema) Hakuwahi kuwaagiza wanafunzi wake wasali kwa watakatifu, malaika, au mtu mwingine yeyote isipokuwa kwa Mungu.

 Yesu pia aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mimi ni njia, na ukweli na uhai. Hakuna awezaye kwenda kwa Baba ila kwa kupitia kwangu.” (Yohana 14:6, BHN) Yesu tu ndiye amepewa mamlaka na Mungu ya kuomba kwa niaba yetu.—Waebrania 7:25.

Vipi nikisali kwa Mungu na kusali pia kwa watakatifu?

 Mungu alisema hivi katika mojawapo wa zile Amri Kumi: “Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.” (Kutoka 20:5, BHN) Mungu ni “mwenye wivu” katika njia gani? Mungu anataka tuwe washikamanifu au tumwabudu—kutia ndani sala—yeye peke yake.—Isaya 48:11.

 Tunamchukiza Mungu tunaposali kwa mtu yeyote yule, iwe watakatifu au malaika. Mtume Yohana alipotaka kumwabudu malaika fulani, malaika huyo alimkataza na kumwambia: “Acha! Mimi ni mtumishi tu kama wewe na ndugu zako; sote tunamshuhudia Yesu. Mwabudu Mungu!”—Ufunuo 19:10, BHN