Hamia kwenye habari

Je, Kuvuta Sigara Ni Dhambi?

Je, Kuvuta Sigara Ni Dhambi?

Jibu la Biblia

 Biblia haitaji kuvuta sigara a au njia nyingine za kutumia tumbaku. Hata hivyo, ina kanuni zinazoonyesha kwamba Mungu anashutumu mazoea machafu na yanayodhuru afya, kwa hiyo, anaona kuvuta sigara kuwa dhambi.

  •   Kuheshimu uhai. “Mungu . . . huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:24, 25) Kwa kuwa uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu, hatupaswi kufanya jambo lolote linaloweza kufupisha maisha yetu, kama vile kuvuta sigara. Kuvuta sigara ni mojawapo ya sababu kuu za vifo vinavyoweza kuzuiwa ulimwenguni pote.

  •   Kupenda jirani. “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Kuvuta sigara ukiwa karibu na watu wengine kunaonyesha kwamba huwapendi. Watu ambao kwa ukawaida wanapumua moshi kutoka kwa mtu anayevuta sigara, wanaweza kuathiriwa zaidi na magonjwa yaleyale ambayo mara nyingi huwapata wavuta-sigara.

  •   Uhitaji wa kuwa mtakatifu. “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, na yenye kukubalika kwa Mungu.” (Waroma 12:1) “Acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kuvuta sigara si jambo la kiasili na halipatani na kuwa mtakatifu​—yaani, kitu safi na kilichotakata​—kwa sababu watumiaji wa tumbaku huingiza kimakusudi mwilini mwao sumu zinazoweza kuharibu mwili wao.

Je, Biblia inasema lolote kuhusu kutumia bangi au dawa nyingine?

 Biblia haitaji bangi au dawa nyingine kama hizo kwa jina. Lakini ina kanuni zinazoonyesha kwamba haifai kutumia vitu kama hivyo vinavyomfanya mtu awe mraibu. Mbali na kanuni zilizotajwa tayari, zifuatazo pia zinahusika:

  •   Uhitaji wa kudhibiti uwezo wetu wa kufikiri. “Lazima umpende Yehova Mungu wako . . . kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37, 38) “Tunzeni akili zenu kwa ukamili.” (1 Petro 1:​13) Mtu hawezi kudhibiti akili yake kikamili anapotumia dawa vibaya, na watu wengine hata wamekuwa waraibu. Akili zao hukazia fikira kutafuta na kutumia dawa za kulevya badala ya kukazia fikira mawazo yenye kujenga.​—Wafilipi 4:8.

  •   Kutii sheria za serikali. “[Wazitii] serikali na mamlaka.” (Tito 3:1) Katika nchi nyingi, sheria zinakataza kabisa matumizi ya dawa fulani. Ikiwa tunataka kumpendeza Mungu, tunapaswa kutii sheria za serikali.​—Waroma 13:1.

a Kuvuta sigara hapa kunarejelea kupumua moshi wa tumbaku kimakusudi kutoka kwenye sigara, kiko, au mirija. Hata hivyo, kanuni zinazozungumziwa hapa zinahusu kutafuna tumbaku, kutumia ugoro, sigara za kielektroni zilizo na nikotini, na bidhaa nyingine kama hizo.