Hamia kwenye habari

Je, Mungu Ana Jina?

Je, Mungu Ana Jina?

Jibu la Biblia

 Wanadamu wote wana jina la kibinafsi. Je, si jambo linalopatana na akili kwa Mungu kuwa na jina? Kuwa na jina la kibinafsi na kulitumia ni jambo muhimu katika urafiki wa kibinadamu. Je, haipaswi kuwa hivyo pia kuhusu urafiki pamoja na Mungu?

 Katika Biblia, Mungu anasema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” (Isaya 42:8) Ingawa ana majina mengi ya cheo kama vile “Mungu Mweza-Yote,” “Bwana Mwenye Enzi Kuu,” na “Muumba,” anawaheshimu waabudu wake kwa kuwaalika wamwite kwa jina lake la kibinafsi.—Mwanzo 17:1; Matendo 4:24; 1 Petro 4:19.

 Tafsiri nyingi za Biblia zina jina la kibinafsi la Mungu kwenye andiko la Kutoka 6:3. Andiko hilo linasema: “Nilikuwa nikimtokea Abrahamu, Isaka na Yakobo kama Mungu Mweza-Yote, lakini kuhusu jina langu Yehova sikujifanya nijulikane kwao.”

 Yehova ni tafsiri ya jina la Mungu katika Kiswahili ambayo imekuwa ikitumiwa kwa miaka mingi. Ingawa wasomi wengi hupendelea kuliandika “Yahweh,” Yehova ndilo jina linalojulikana na watu wengi zaidi. Sehemu ya kwanza ya Biblia haikuandikwa katika Kiswahili bali Kiebrania, lugha ambayo husomwa kutoka kulia kwenda kushoto. Katika lugha hiyo, jina la Mungu liliandikwa kwa herufi hizi nne, יהוה. Herufi hizo nne za Kiebrania, ambazo hutafsiriwa YHWH, zinaitwa Tetragramatoni.