Hamia kwenye habari

Biblia Ni Nini?

Biblia Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Biblia ni mkusanyiko wa vitabu 66 vitakatifu. Iliandikwa katika kipindi cha miaka 1,600 hivi. Biblia ina ujumbe kutoka kwa Mungu—“neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

Katika makala hii

 Mambo hakika kuhusu Biblia

  •   Ni nani aliyeandika Biblia? Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia, lakini alitumia wanaume 40 tofauti kuiandika. Baadhi ya wanaume hao ni Musa, Mfalme Daudi, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. a Mungu aliingiza mawazo yake katika akili za waandikaji ili waweze kuandika ujumbe wake.—2 Timotheo 3:16.

     Kwa mfano: Mfanyabiashara akimwagiza karani wake aandike ujumbe kwa niaba yake, na labda hata akimpa mapendekezo fulani, bado mfanyabiashara huyo ndiye mtungaji wa ujumbe wenyewe. Vivyo hivyo, hata ingawa Mungu aliwatumia wanaume kuandika ujumbe wake, yeye ndiye Mtungaji halisi wa Biblia.

  •   Neno “Biblia” linamaanisha nini? “Biblia” linatokana na neno la Kigiriki biblia, linalomaanisha “vitabu vidogo.” Kadiri muda ulivyopita, neno biblia likaja kurejelea mkusanyo wote wa vitabu vidogo vinavyofanyiza Biblia.

  •   Biblia iliandikwa lini? Biblia ilianza kuandikwa mwaka wa 1513 K.W.K. na ilikamilishwa baada ya zaidi ya miaka 1,600, katika mwaka wa 98 W.K. hivi.

  •   Biblia ya awali iko wapi? Hakuna maandishi ya awali ambayo yanajulikana kuwa yaliokoka. Sababu ni kwamba waandikaji wa Biblia walitumia vifaa vilivyopatikana wakati huo ambavyo vingeweza kuharibika, kama vile mafunjo na hati za ngozi. Hata hivyo, kwa karne nyingi wanakili stadi walinakili tena na tena maandishi ya Biblia, na hivyo kuhifadhi maneno yake kwa ajili ya wasomaji wa wakati ujao.

  •   “Agano la Kale” na “Agano Jipya” ni nini? Kinachojulikana sana kama Agano la Kale ni ufafanuzi unaotumiwa kurejelea sehemu ya Biblia iliyoandikwa hasa kwa Kiebrania, b ambayo pia inajulikana kama Maandiko ya Kiebrania. Kinachojulikana kuwa Agano Jipya ni ufafanuzi unaorejelea sehemu iliyoandikwa kwa Kigiriki, inayojulikana kama Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Sehemu hizo mbili zikiwa pamoja zinafanyiza kitabu kimoja kamili, ambacho pia kinaitwa Maandiko Matakatifu. c

  •   Ni mambo gani yaliyomo katika Biblia? Sehemu mbalimbali za Biblia zina historia, sheria, unabii, mashairi, methali, nyimbo, na barua.—Ona “ Orodha ya Vitabu vya Biblia.”

 Biblia ina ujumbe gani?

 Biblia inaanza kwa kutoa muhtasari wa jinsi Mungu Mweza-Yote alivyoumba mbingu na dunia. Kupitia Biblia, Mungu anajitambulisha kwa jina lake, Yehova, na hivyo kuwakaribisha wanadamu wamjue.—Zaburi 83:18.

 Biblia inaeleza kwamba jina la Mungu limechafuliwa, na inaonyesha jinsi atakavyosafisha jina lake.

 Biblia inafunua kusudi la Mungu kwa wanadamu na dunia. Inaonyesha jinsi wakati ujao Mungu atakavyoondoa mambo yanayowafanya wanadamu wateseke.

 Biblia inatoa mashauri yanayofaa kwa ajili ya maisha ya kila siku. Ifuatayo ni mifano michache:

  •   Kudumisha uhusiano mzuri. “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

     Maana: Tunapaswa kuwatendea wengine kama ambavyo sisi tungependa kutendewa.

  •   Kukabiliana na mkazo. “Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.”—Mathayo 6:34.

     Maana: Badala ya kuhangaika kupita kiasi kuhusu mambo yatakayotokea wakati ujao, ni muhimu zaidi kukazia fikira hali zetu za sasa.

  •   Kufurahia ndoa yenye furaha. “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Waefeso 5:33.

     Maana: Upendo na heshima ni muhimu ili kuwa na ndoa yenye mafanikio.

 Je, Biblia imebadilishwa?

 Hapana. Wasomi wamelinganisha kwa makini hati za kale za Biblia na Biblia iliyopo leo na wamegundua kwamba ujumbe wa awali wa Biblia haujabadilika. Hilo linapatana na akili kwa sababu, ikiwa Mungu anataka ujumbe wake usomwe na kueleweka, je, haipatani na akili kwamba atahakikisha ujumbe huo haubadilishwi? dIsaya 40:8.

 Kwa nini kuna tafsiri nyingi tofauti za Biblia?

 Wasomaji wengi leo hawawezi kuelewa lugha zilizotumiwa zamani kuandika Biblia. Hata hivyo, Biblia ina “habari njema” kwa ajili ya “kila taifa na kabila na lugha.” (Ufunuo 14:6) Kwa sababu hiyo, watu wanahitaji tafsiri ya Biblia katika lugha wanayoweza kuelewa ili wasome na kuelewa vizuri ujumbe wa Mungu.

 Kuna aina tatu za tafsiri za Biblia:

  •   Tafsiri ya neno kwa neno ambayo ni ambayo ni tafsiri sisisi kadiri iwezekanavyo.

  •   Tafsiri ya wazo kwa wazo inayotumia maneno yanayowakilisha maana ya maandishi ya lugha ya awali.

  •   Tafsiri ya ufafanuzi inayobadili maandishi kwa uhuru, lengo likiwa kumfanya msomaji afurahie usomaji wake. Hata hivyo, nyakati nyingine uhuru uliopo katika tafsiri ya ufafanuzi huficha maana ya kweli ya simulizi.

 Tafsiri nzuri ya Biblia ni ile inayosawazisha tafsiri sisisi kwa kutumia lugha ya kisasa inayoeleweka ili kuwapitishia wanadamu ujumbe wa Mungu kwa usahihi. e

 Ni nani aliyeamua mambo yanayopaswa kuwa katika Biblia?

 Mungu akiwa Mtungaji wa Biblia ndiye aliyeamua mambo yanayopaswa kuwa katika Biblia. Alichagua kwanza taifa la kale la Israeli nao “walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu,” na hivyo wakatenda kama wahifadhi wa Maandiko ya Kiebrania.—Waroma 3:2.

 Je, kuna vitabu vya Biblia vilivyopotea?

 Hapana. Biblia ni kamili; hakuna vitabu “vilivyopotea.” Watu fulani hudai kwamba vitabu fulani vya kale vilivyofichwa zamani vinapaswa kuwa sehemu ya Biblia. f Hata hivyo, Biblia ina njia yake ya kuthibitisha uasilia. (2 Timotheo 1:13) Kupitia kiwango hicho, vitabu vya Biblia vilivyoongozwa na roho ya Mungu vina upatano kamili. Hilo haliwezi kusemwa kuhusu maandishi mengine yote ya kale ambayo watu fulani wangependa kudai kuwa ni sehemu ya Biblia. g

 Jinsi ya kupata mistari ya Biblia

  Orodha ya vitabu vya Biblia

a Ili upate orodha kamili ya vitabu vya Biblia, majina ya waandikaji, na wakati vilipoandikwa, tafadhali ona “Orodha ya Vitabu vya Biblia.”

b Sehemu ndogo za Biblia ziliandikwa katika Kiaramu, lugha inayohusiana kwa ukaribu na Kiebrania.

c Wasomaji wengi wa Biblia wanapenda kutumia maneno “Maandiko ya Kiebrania” na “Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.” Maneno hayo husaidia kuondoa wazo la kwamba “Agano la Kale” limepitwa na wakati na mahali pake kuchukuliwa na “Agano Jipya.”

d Ona makala yenye kichwa “Je, Biblia Imebadilishwa au Kupotoshwa?

e Watu wengi hufurahia kusoma Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu ya usahihi wake na ni rahisi kuelewa. Ona makala yenye kichwa “Je, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Ni Sahihi?

f Maandishi hayo kwa pamoja yanaitwa Apokrifa. Kulingana na Encyclopædia Britannica, “katika maandishi yanayohusiana na Biblia, [maneno hayo yanarejelea] vitabu ambavyo havijatiwa ndani ya maandiko yanayokubalika”—yaani, hayajatiwa ndani ya orodha rasmi inayokubalika ya vitabu vya Biblia.

g Ili kujifunza mengi zaidi, ona makala yenye kichwa “Injili za Apokrifa—Je, Zina Ukweli Uliofichwa Kumhusu Yesu?