Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Je, Tuishi Pamoja Kabla ya Ndoa?

Je, Tuishi Pamoja Kabla ya Ndoa?

 Wenzi wengi wa ndoa wanaishi pamoja kabla ya kufunga ndoa. Baadhi yao hufanya hivyo kwa sababu wangependa kuona ikiwa wanapatana na wanatumaini kwamba kufanya hivyo kutasaidia ndoa yao ifanikiwe. Je, ni jambo la hekima kuishi pamoja kabla ya ndoa?

Katika makala hii

 Biblia inasema nini?

  •   Biblia inashutumu kufanya ngono nje ya ndoa. Kwa mfano, inasema hivi: “Mjiepushe na uasherati.” (1 Wathesalonike 4:3; 1 Wakorintho 6:18) Hiyo inatia ndani ngono kati ya mwanamume na mwanamke wanaoishi pamoja, hata ikiwa wanakusudia kufunga ndoa baadaye. a Viwango vya Biblia vinawasaidia wasipate ujauzito bila kufunga ndoa na matokeo mengine mabaya yanayoweza kusababishwa na kuishi pamoja kabla ya ndoa.

  •   Mpango wa ndoa unatoka kwa Mungu. Alipouanzisha, alisema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Mwanamume na mwanamke wanapowajibika katika ndoa, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba familia yao itakuwa imara na yenye upendo.

 Je, kuishi pamoja kutakusaidia kujitayarisha kwa ajili ya ndoa?

 Baadhi ya watu husema ndiyo. Wanahisi kwamba mwanamume na mwanamke wanapata uzoefu unaofaa wanaposhirikiana kufanya kazi za nyumbani na kuchunguzana tabia kila siku. Hata hivyo, jambo muhimu sana ili kuwa na ndoa yenye furaha ni kuwajibika.

 Mwanamume na mwanamke wanawezaje kujifunza kushikamana katika nyakati nzuri na mbaya? Si kwa kuingia katika muungano wa “majaribio” wakati wote wawili wanaona uhusiano wao kama kitu kinachoweza kukomeshwa na kila mtu kwenda zake. Badala yake, mahusiano hufanikiwa kila mmoja anapowajibika kabisa kwa mwenzake na kushirikiana kutatua matatizo.

 Jambo kuu: Badala ya kujitayarisha kwa ajili ya ndoa, mwanamume na mwanamke wanaoamua kuishi pamoja kabla ya ndoa wanajitayarisha kutengana.

 Kanuni ya Biblia: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”​—Wagalatia 6:7.

 Je, kuishi pamoja kutakunufaisha kiuchumi?

 Baadhi ya watu wanasema ndiyo. Uchunguzi uliofanywa na Kituo cha Utafiti cha Pew ulisema kwamba nchini Marekani, watu wazima wanne kati ya kumi walianza kuishi pamoja kwa sababu za kiuchumi. Hata hivyo, baada ya kuishi pamoja kwa muda, idadi fulani ya watu bado walisema matatizo ya kiuchumi ndiyo sababu kubwa iliyowafanya wasifunge ndoa.

 Kuishi pamoja kabla ya ndoa kunaweza kuwa na madhara mengine, hasa kwa wanawake. Kwa mfano, baada ya uhusiano kwisha, mara nyingi wanawake ndio wanaoachiwa jukumu la kulea watoto.

 Jambo kuu: Madhara ya kuishi pamoja kabla ya ndoa ni makubwa zaidi kuliko manufaa yoyote ambayo huenda mtu akafikiri atapata.

 Kanuni ya Biblia: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”​—Isaya 48:17.

 Je, kuishi pamoja kutakusaidia kuepuka kufunga ndoa na mtu asiyefaa?

 Baadhi ya watu wanasema ndiyo. Hata hivyo, “mara nyingi watu wanaoanza kuishi pamoja kabla ya ndoa hawatambui kwamba kufanya hivyo kunafanya iwe vigumu zaidi kukomesha uhusiano wao,” kinasema kitabu Fighting for Your Marriage. Kwa nini? Kwa sababu wenzi fulani wanaoishi pamoja wanaweza kugundua kwamba kuna mambo mengi yanayowafanya wasipatane. Lakini kwa sababu ya majukumu kama vile kuwa na mnyama-kipenzi, nyumba wanayolipia pamoja, au ujauzito ambao haukutarajiwa, watafiti wanasema wenzi hao wanazoea au wanalazimika kuishi pamoja kwa sababu hawawezi kufanya mabadiliko yatakayowafaa. b Kitabu Fighting for Your Marriage kinaendelea kusema kwamba “watu fulani ambao wangetengana kabla ya ndoa, wanalazimika kufunga ndoa kwa sababu ni rahisi zaidi kuendelea kuishi pamoja.”

 Jambo kuu: Badala ya kukusaidia kufanya uamuzi mzuri, kuishi pamoja kunaweza kufanya iwe vigumu zaidi kukomesha uhusiano mbaya.

 Kanuni ya Biblia: “Mtu mwerevu huona hatari na kujificha, lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.”​—Methali 22:3.

 Je, kuna njia inayofaa?

 Unaweza kuepuka hatari zinazotokana na kuishi pamoja kabla ya ndoa na kuongeza nafasi za kuwa na ndoa yenye mafanikio. Jinsi gani? Kwa kushikamana na viwango vya Biblia kuhusu ndoa. Chukua muda wa kutosha kumfahamu mtu unayefikiria kufunga ndoa naye kabla ya kuanza kuishi pamoja kama mume na mke. Inafaa zaidi kumchagua mwenzi wa ndoa kwa sababu nyote wawili mna viwango na imani zinazopatana, badala ya kufunga ndoa kwa sababu unavutiwa naye kingono.

 Biblia ina mashauri yanayoweza kukusaidia kuweka msingi wa kuwa na ndoa imara na yenye furaha. c Kwa mfano, Biblia ina kanuni zinazoweza kukusaidia . . .

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu habari hizo, ona sehemu ya “Ndoa na Familia” kwenye jw.org.

 Kanuni ya Biblia: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha.”​—2 Timotheo 3:16.

b Kutoka kwenye makala “Kuteleza Ama Kuamua: Matokeo ya Kuzoeana kwa Lazima na Kuishi Pamoja Kabla ya Ndoa,” imeandikwa na Scott M. Stanley, Galena Kline Rhoades, na Howard J. Markman, ikachapishwa katika jarida Family Relations.

c Katika tamaduni fulani, wazazi wanahusika sana katika kuamua ni nani atakayekuwa mwenzi wa ndoa wa mwana au binti yao. Ikiwa ndivyo ilivyo, Biblia inaweza kuwasaidia wazazi kutambua sifa za kutafuta.