Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ndoa?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ndoa?

Jibu la Biblia

 Baada ya kumuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Mungu aliwaunganisha katika ndoa. Alianzisha ndoa iwe muungano wa pekee kati ya mwanamume na mwanamke na hivyo kufanyiza mazingira yanayofaa ya kuwa na familia.—Mwanzo 1:27, 28; 2:18.

 Mungu anataka wenzi wa ndoa wawe na furaha. (Methali 5:18) Katika Biblia, ameandaa viwango kwa ajili ya ndoa na kanuni zinazoweza kusaidia ndoa ifanikiwe.

Katika makala hii

 Mungu ameweka viwango gani kwa ajili ya ndoa?

 Tangu mwanzo, Mungu alikusudia ndoa iwe muungano kati ya mume mmoja na mke mmoja. (Mwanzo 2:24) Mungu anachukia ndoa ya wake wengi, matendo ya ngono kati ya watu wa jinsia moja, au watu kuishi pamoja bila kufunga ndoa. (1 Wakorintho 6:9; 1 Wathesalonike 4:3) Yesu aliwafundisha wafuasi wake kutii kiwango ambacho Mungu aliweka kwa ajili ya ndoa.—Marko 10:6-8.

 Kwa maoni ya Mungu, ndoa ni muungano wa kudumu. Mwanamume na mwanamke wanapofunga ndoa wanaahidi kwamba watakuwa washikamanifu na kukaa pamoja muda wote wa maisha yao. Mungu anawatarajia watimize ahadi hiyo.—Marko 10:9.

 Mungu ana maoni gani kuhusu kutengana na kutalikiana?

 Kuna pindi ambazo huenda mwenzi mmoja akalazimika kuwa mbali na mwenzake, kama vile mmoja wao anapohitaji kusafiri ili kushughulikia dharura ya familia. Hata hivyo, Biblia haipendekezi kutengana kwa sababu ya matatizo ya ndoa. Badala yake, inawahimiza wenzi wa ndoa walio na matatizo ya ndoa wajitahidi kupatana.—1 Wakorintho 7:10.

 Uzinzi ndio msingi pekee wa kimaandiko wa kutalikiana. (Mathayo 19:9) Hivyo, mume na mke wakiamua kutengana au kutalikiana kwa sababu nyingine yoyote isipokuwa uzinzi, hakuna yeyote kati yao aliye huru Kimaandiko kumchumbia mtu mwingine au kufunga ndoa naye.—Mathayo 5:32; 1 Wakorintho 7:11.

 Je, ni lazima ndoa iandikishwe kisheria ili ikubaliwe na Mungu?

 Mungu anatarajia Wakristo watii sheria za serikali kuhusu ndoa. (Tito 3:1) Wenzi wa ndoa wanapoandikisha ndoa yao kisheria, wanaonyesha heshima kwa mamlaka za serikali na kwa kiwango cha Mungu kwamba ndoa ni muungano wa kudumu. a

 Biblia inasema mume na mke wana majukumu na wajibu gani?

  •   Majukumu ya wote wawili. Waume na wake wanapaswa kutendeana kwa upendo na heshima. (Waefeso 5:33) Kila mmoja anapaswa kushughulikia mahitaji ya ngono ya mwenzake kwa njia yenye upendo na kuepuka aina zote za ukosefu wa uaminifu. (1 Wakorintho 7:3; Waebrania 13:4) Ikiwa wana watoto, mume na mke wana jukumu la kusaidiana kuwalea.—Methali 6:20.

     Biblia haisemi kihususa jinsi wenzi wa ndoa wanavyopaswa kugawana majukumu yanayohusu kazi ya kimwili na kazi za nyumbani. Wanapaswa kuamua pamoja ni nini kitakachofaa familia yao.

  •   Jukumu la mume. Biblia inasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake.” (Waefeso 5:23) Yeye ni kichwa katika maana kwamba anapaswa kuongoza familia yake na kufanya maamuzi ambayo yatamnufaisha mke wake na watoto wake.

     Anapaswa kuhakikisha kwamba mahitaji yao ya kimwili, kihisia, na kiroho yanashughulikiwa. (1 Timotheo 5:8) Anaonyesha kwamba anathamini sifa na uwezo wa mke wake kwa kufanya kazi pamoja naye na kwa kufikiria kwa makini maoni na hisia zake anapofanya maamuzi. (Methali 31:11, 28) Biblia inasema kwamba mume anapaswa kushughulikia majukumu yake kwa upendo.—Wakolosai 3:19.

  •   Jukumu la mke. Biblia inasema kwamba “mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Mke anapoheshimu jukumu ambalo Mungu amemkabidhi mume wake, Mungu anafurahi.

     Jukumu la mke ni kuwa msaidizi wa mume wake, kumsaidia kufanya maamuzi mazuri, na kuunga mkono ukichwa wake. (Mwanzo 2:18) Biblia inamsifu mke anayetimiza jukumu lake muhimu katika ndoa.—Methali 31:10.

 Je, Mungu anatarajia kwamba lazima wenzi wa ndoa wawe na watoto?

 Hapana. Zamani Mungu aliamuru baadhi ya waabudu wake wazae watoto. (Mwanzo 1:28; 9:1) Lakini agizo hilo haliwahusu Wakristo leo. Yesu hakuamuru kamwe kwamba wafuasi wake wapate watoto. Pia, wanafunzi wake wa karne ya kwanza hawakusema kwamba lazima wenzi wa ndoa wapate watoto. Wenzi wa ndoa hujiamulia wenyewe ikiwa watazaa watoto.

 Biblia inaweza kuisaidiaje ndoa yangu?

 Biblia ina kanuni zinazoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kuanzisha ndoa yao vizuri. Pia, kanuni za Biblia zinaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kuepuka au kushinda hali ngumu.

 Kanuni za Biblia zinaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa . . .

a Ili kupata habari kuhusu maoni ya Biblia kuhusiana na ndoa za kimila au za kikabila, ona Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2006, ukurasa wa 21, fungu la 12.