Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Mapendezi Yanapotofautiana

Mapendezi Yanapotofautiana

CHANGAMOTO

Wewe unafurahia michezo; mwenzi wako anapenda zaidi kuketi na kusoma. Wewe unafuata utaratibu na hupendi kupoteza muda; mwenzi wako anafanya mambo shaghalabaghala. Wewe unapenda kuchangamana na wengine; mwenzi wako anapenda faragha.

Huenda ukajiambia, ‘Hatupatani kabisa! Kwa nini hatukugundua hilo tulipokuwa tukichumbiana?’

Kuna uwezekano mkubwa uligundua jambo hilo. Lakini wakati huo ulikuwa tayari kukubali tofauti hizo—jambo ambalo unapaswa kuanza kufanya tena, kwa kuwa sasa mmeoana. Makala hii itakusaidia kufanya hivyo. Lakini kwanza, kuna mambo unayopaswa kuzingatia kuhusu tofauti hizo.

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Tofauti nyingine si za kupuuza. Kusudi muhimu la uchumba ni kuchunguza ikiwa mtafaana. Hivyo, watu wengi wanapogundua kwamba wana tofauti kubwa, kwa hekima wao huamua kukatisha uhusiano badala ya kuingia katika ndoa yenye migawanyiko. Lakini vipi ikiwa tofauti zilizopo ni ndogo na ni za kawaida katika ndoa zote?

Hakuna watu wanaofanana kabisa. Huenda wenzi wa ndoa wasipatane katika mambo yafuatayo:

Mapendezi. Anna * anasema hivi: “Tangu utotoni mume wangu amekuwa akifurahia kupanda milima yenye theluji na kutembea nyikani, lakini sijawahi kupendezwa na mambo ya aina hiyo.”

Mazoea. “Mke wangu anaweza kulala usiku sana na bado aamke saa 11:00 alfajiri, lakini mimi ninahitaji kulala kwa saa saba au nane la sivyo siku inayofuata mimi hukasirika-kasirika upesi,” anasema Brian.

Utu. Huenda wewe ni mnyamavu, ilhali mwenzi wako ni mwongeaji. David anasema, “Tangu utotoni sijazoea kuzungumzia matatizo yangu, lakini mke wangu alilelewa katika familia iliyozoea kujadili mambo yote waziwazi.”

Tofauti zina faida. “Huenda njia yangu ya kufanya jambo ni sahihi, lakini hilo halimaanishi kwamba ndiyo njia pekee ya kulifanya,” anasema mwanamke mmoja anayeitwa Helena.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mwunge mkono. Adam anasema hivi: “Mke wangu Karen hapendezwi hata kidogo na michezo. Lakini yeye huandamana nami kunapokuwa na mechi na hata yeye hushangilia pamoja nami. Kwa upande mwingine, Karen anapenda kutembelea majumba ya maonyesho ya sanaa, hivyo ninaandamana naye, na tunafanya hivyo mpaka anaporidhika. Nimelazimika kupendezwa na sanaa kwa sababu hilo ni jambo muhimu kwake.”—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 10:24.

Uwe na akili iliyofunguka. Kwa sababu tu mtazamo wa mwenzi wako unatofautiana na wako haimaanishi kwamba si sahihi. Alex amejifunza jambo hilo. Alisema hivi: “Siku zote maoni yangu yalikuwa kwamba kuna njia moja tu sahihi ya kufanya jambo. Lakini kuoa kumenisaidia kutambua kwamba kuna njia nyingi za kufanya jambo, na kila moja ina faida yake.”—Kanuni ya Biblia: 1 Petro 5:5.

Uwe na usawaziko. Kufaana hakumaanishi kufanana. Hivyo usifikiri kwamba ulikosea kufunga ndoa kwa sababu tu umegundua mnatofautiana kwa njia fulani. Kitabu The Case Against Divorce kinasema hivi: “Watu wengi wanajitetea kwamba ‘Walipumbazwa na mahaba.’” Hata hivyo, kitabu hicho kinaendelea kusema “kila siku mliyoifurahia pamoja, inaonyesha kwamba hata ingawa mnatofautiana kwa njia fulani, mnaweza kupendana.” Jitahidini ‘kuendelea kuvumiliana ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika.’—Wakolosai 3:13.

Jaribu kufanya hivi: Andika mambo ambayo unapenda kuhusu mwenzi wako na unayoona kuwa mnapatana. Halafu andika mambo unayoona kuwa mnatofautiana. Huenda ukagundua kwamba tofauti zenu si kubwa kama ulivyofikiri. Orodha hiyo itakusaidia kugundua maeneo ambayo huenda ukahitaji kuonyesha uvumilivu zaidi au kumwunga mkono mwenzi wako. Kenneth anasema hivi: “Ninathamini sana mke wangu anapotanguliza mapendezi yangu, na ninajua anathamini ninapotanguliza yake. Hata ikiwa lazima nijidhabihu, maadamu yeye anafurahi, mimi pia ninafurahi.”—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:5.

^ fu. 10 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.