Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Nafsi

Nafsi

Dini mbalimbali hutoa ufafanuzi unaotofautiana kuhusu nafsi na kinachoipata baada ya kifo. Hata hivyo, Biblia inatoa ufafanuzi ulio wazi kabisa.

Je, nafsi inaweza kufa?

WATU HUSEMA NINI?

Watu wengi wanaamini kwamba nafsi haiwezi kufa. Baadhi huamini kwamba baada ya kifo nafsi huzaliwa upya katika mwili mwingine. Wengine huamini kwamba hatimaye nafsi itaenda sehemu nyingine, iwe ni mbinguni au katika moto wa mateso.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haisemi kwamba nafsi haiwezi kufa. Badala yake, inaeleza mara kadhaa kwamba nafsi hufa. Nabii Ezekieli, ambaye alitumiwa na Mungu kuandika kitabu kimoja cha Biblia, aliandika kwamba nafsi inaweza kuhukumiwa kifo. Biblia pia inatumia maneno ‘nafsi iliyokufa’ kurejelea maiti. (Mambo ya Walawi 21:11) Ni wazi Biblia haifundishi kwamba nafsi haiwezi kufa.

“Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.”Ezekieli 18:20.

Je, nafsi na mwili ni vitu viwili tofauti?

WATU HUSEMA NINI?

Nafsi hufanya mwili uwe hai lakini mtu anapokufa nafsi hiyo hutoka.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inaeleza kuwa mama mmoja alizaa “nafsi”—yaani, watu walio hai. (Mwanzo 46:18) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa katika Biblia kuwa “nafsi” linaweza kutafsiriwa pia “anayepumua.” Nyakati nyingine neno hilo hurejelea hata wanyama. Mbali na hilo, Biblia husema kwamba nafsi inahitaji chakula. (Kumbukumbu la Torati 12:20) Ikiwa nafsi ni kitu kinachoweza kutenganishwa na mwili, je, kingehitaji kupumua au kula? Mara nyingi katika Biblia neno “nafsi” linarejelea mtu aliye hai, yaani mwili, hisia, na utu wake.

‘Akamzalia nafsi 16.’Mwanzo 46:18.

Nafsi hupatwa na nini wakati wa kifo?

BIBLIA INASEMA NINI?

Tunajua kwamba miili yetu huharibika baada ya kifo, vivyo hivyo pia “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi.” (Mhubiri 9:10) Maandiko yanaonyesha wazi kwamba mtu anapokufa yeye “hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:4) Nafsi iliyokufa haiwezi kutenda lolote, na hivyo kwa njia ya mfano Maandiko husema kwamba mtu aliyekufa ‘amelala usingizi.’—Mathayo 9:24.

KWA NINI JAMBO HILI NI MUHIMU?

Unapopoteza wapendwa wako katika kifo, unataka kupata majibu ya maswali kama: Wako wapi? Wako katika hali gani? Je, wanateseka? Kwa kuwa Biblia inatuambia kwamba wafu hawafahamu lolote, tunafarijika kujua wapendwa wetu waliokufa hawateseki. Na tunafarijika hata zaidi kujua kwamba Yehova anaahidi kwamba wakati ujao atafufua nafsi zilizokufa.—Isaya 26:19.

Wafu, hawajui lolote kamwe.”Mhubiri 9:5.