Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kuepuka Wivu Katika Ndoa

Jinsi ya Kuepuka Wivu Katika Ndoa

 Ndoa haiwezi kuwa na furaha ikiwa mume na mke hawaaminiani au ikiwa mmoja anamshuku mwenzake. Hivyo, unaweza kuepukaje wivu usio na msingi?

Katika makala hii

 Wivu ni nini?

 Neno “wivu” lina maana kubwa. Katika makala hii, neno hilo linarejelea hisia tunayopata tunapoamini kwamba mtu anavutiwa kimahaba na mwenzi wetu wa ndoa au tunapoamini mwenzi wetu anavutiwa kimahaba na mtu mwingine. Huenda tukahisi kwamba ndoa yetu iko hatarini. Ikiwa kihalisi hali iko hivyo, basi wivu huo unafaa na ni kawaida kuhisi hivyo. Ukweli ni kwamba ndoa ni urafiki wa karibu zaidi kati ya watu wawili na wenzi wa ndoa wanapaswa kufanya yote wawezayo ili kuilinda ndoa yao.

 Kanuni ya Biblia: “Basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. . . . Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”​—Mathayo 19:6.

 “Ikiwa ndoa yako inakabili hatari, wivu ni kama moshi unaokuonya kwamba moto unaweza kuwaka na kwamba unahitaji kuchukua hatua.”​—Benjamin.

 Hata hivyo, wivu usiofaa unatokana na shaka na woga usio na msingi. Upendo wa kweli unatusaidia kuepuka wivu huo wenye madhara. (1 Wakorintho 13:4, 7) Dakt. Robert L. Leahy aliandika hivi: “Unapokuwa na wivu usio na msingi unaweza kufanya mambo ambayo yanaweza kuharibu uhusiano uleule unaojaribu kulinda.” a

 Ni nini husababisha wivu usiofaa?

 Huenda ukawa na wivu usiofaa ikiwa umewahi kusalitiwa na mwenzi wa ndoa wa zamani. Au huenda ndoa ya wazazi wako ilivunjika kwa sababu mzazi mmoja hakuwa mwaminifu na una hofu kwamba ndoa yako itapatwa na hali hiyohiyo.

 “Baba yangu hakuwa mwaminifu kwa mama yangu, kwa hiyo, ni vigumu kwangu kuamini wengine hata ingawa jambo hilo lilitokea nilipokuwa mtoto. Hilo liliniumiza kihisia na wakati mwingine inakuwa vigumu kwangu kumwamini mume wangu.”​—Melissa.

 Mambo mengine yanayochangia: Ikiwa unahisi huna thamani au hufai, ni rahisi kufikiria kwamba wengine wanajaribu kuvunja ndoa yako. Hata unaweza kujisadikishia kwamba mwenzi wako akipata tu nafasi, atakuacha na kuchukua mtu mwingine.

 “Rafiki ya mume wangu alimwomba asimamie kwenye harusi yake na hilo lilimaanisha kwamba angepangwa na mwanamke mwingine. Jambo hilo halikunifurahisha kabisa. Ilibidi akatae.”​—Naomi.

 Katika nchi mbalimbali kuna tamaduni tofauti-tofauti za harusi lakini Wakristo wanapaswa kuongozwa na kanuni za Biblia. Je, Naomi alionyesha usawaziko katika kisa hicho? Anapofikiria kisa hicho sasa, anahisi kwamba hakuwa na sababu za kuwa na wivu. Anasema: “Nilihisi kana kwamba wanawake wengine ni bora kuliko mimi kwa kuwa nilifikiri kwamba mume wangu alinilinganisha na wanawake wengine, lakini hilo lilikuwa akilini mwangu tu.”

 Kwa vyovyote vile, wivu usiofaa unaweza kukufanya umshuku mwenzi wako na kumlaumu ukidhani kwamba yeye si mwaminifu. Matokeo ni kwamba kuwa na hisia hizo kunaweza kuharibu ndoa yako na hata afya yako.

 Kanuni ya Biblia: “Wivu ni kama ugonjwa wa ubovu mifupani.”​—Mithali 14:30, Swahili Roehl Bible 1937.

 Unawezaje kudhibiti wivu wako?

 Jitahidi kumwamini zaidi mwenzi wako. Badala ya kutafuta dalili za kwamba mwenzi wako anakosa uaminifu, kumbuka mambo aliyofanya yanayoweza kukufanya umwamini zaidi.

 “Mimi hufikiria sifa nzuri za mume wangu. Anapomsikiliza mtu kwa makini, anafanya hivyo kwa sababu yeye ni mwenye kujali na si kwa sababu ana nia mbaya. Mara nyingi ninahitaji kujikumbusha kwamba ingawa ndoa ya wazazi wangu haikuwa nzuri hilo halimaanishi kwamba ndoa yangu haitakuwa nzuri.”​—Melissa.

 Kanuni ya Biblia: “Upendo . . . huamini mambo yote.”​—1 Wakorintho 13:4, 7.

 Angalia upya sababu zinazokufanya umshuku. Dakt. Leahy, aliyenukuliwa hapo juu aliandika hivi: “Mara nyingi tunafikiri kwamba mambo tunayofikiria ni sahihi. Kwa kuwa tunaamini kwamba jambo tunalofikiria ni la kweli, basi tunahisi huo ni uthibitisho tosha. Hata hivyo, kuamini au kuhisi kwamba jambo fulani ni kweli hakulifanyi liwe kweli, na huo si uthibitisho halisi.” b

 “Kuwa na shaka kuhusu kila jambo ambalo tunamwona mwenzi wetu akifanya, kunazusha tu matatizo katika ndoa.”​—Nadine.

 Kanuni ya Biblia: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.”​—Wafilipi 4:5.

 Mweleze mwenzi wako mahangaiko yako. Hata iwe wivu wako unasababishwa na nini, zungumza na mwenzi wako kuhusu mahangaiko yako ili nyote wawili mkubaliane kuhusu mipaka yenye usawaziko mnayoweza kujiwekea kuhusu tabia.

 “Mnapokuwa na mazungumzo ya aina hiyo uwe na uhakika kwamba mwenzi wako hangependa kukuumiza na kwamba yeye pia anajitahidi kufanya maamuzi mazuri. Usihisi kwamba mwenzi wako ana nia mbaya. Huenda ni mambo madogo tu yanayokuhangaisha na una matarajio makubwa kupita kiasi. Au huenda mwenzi wako asitambue kwamba unahitaji kuonyeshwa upendo zaidi.”​—Ciara.

 Kanuni ya Biblia: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”​—1 Wakorintho 10:24.

a b Kitabu The Jealousy Cure.