Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA

Maoni Yanapotofautiana

Maoni Yanapotofautiana

 Wenzi wa ndoa wanaweza kukabili changamoto kwa sababu ya kuwa na mapendezi, mazoea, na nyutu zinazotofautiana. Hata hivyo, mambo mengine yanaweza kutokeza hali ngumu zaidi. Kwa mfano:

  •   Tutashirikiana kwa muda mrefu kadiri gani na watu wa ukoo?

  •   Tutashughulikiaje pesa?

  •   Je, tutapata watoto?

 Unaweza kufanya nini ikiwa wewe na mwenzi wako mna maoni yanayotofautiana?

 Unachopaswa kujua

 Kupatana hakumaanishi kufanana. Hata mume na mke wanaopatana sana hawawezi kuwa na maoni yaleyale sikuzote, hata katika mambo mazito.

 “Nililelewa katika familia yenye uhusiano wa karibu sana. Mwisho-juma tulikuwa tukiwatembelea babu na nyanya (bibi), wajomba, shangazi, na binamu zetu. Lakini familia ya mume wangu hawakuwa na zoea la kufanya mambo pamoja. Kwa hiyo, tuna maoni yanayotofautiana kuhusu muda tunaotumia pamoja na watu wa ukoo au wa kuwasiliana nao ikiwa wanaishi mbali.”—Tamara.

 “Kwa sababu ya malezi yetu, mimi na mke wangu tuna maoni tofauti kuhusu kutumia pesa. Katika miezi michache ya kwanza baada ya kufunga ndoa tulibishana mara kadhaa kuhusu hilo. Tulikubaliana baada tu ya kuzungumzia jambo hilo mara kadhaa.”—Tyler.

Watu wawili wanaweza kutazama tukio lilelile lakini wawe na maoni tofauti kulihusu. Ni hivyo pia kuhusu jambo ambalo wenzi wa ndoa hawakubaliani

 Matatizo fulani hayawezi kutatuliwa kwa kukubaliana tu kuacha jambo. Kwa mfano, vipi ikiwa mkwe wako anakuwa mgonjwa na anahitaji kutunzwa? Au vipi ikiwa mwenzi mmoja anataka kupata watoto lakini yule mwingine hataki? a

 “Mimi na mke wangu tumezungumza mara kadhaa kuhusu kupata watoto. Yeye ameanza kutaka kupata watoto na hisia hiyo inazidi kuongezeka, lakini maoni yetu yanazidi kutofautiana. Sioni jinsi tutakavyokubaliana.”—Alex.

 Kwa kuwa tu maoni yenu yanatofautiana haimaanishi ndoa yenu itavunjika. Wataalamu fulani wanasema kwamba ikiwa wewe na mwenzi wako hamwezi kukubaliana kuhusu jambo zito, unapaswa kufanya chochote unachoweza ili kupata unachotaka—hata ikiwa utahitaji kuvunja ndoa yako. Lakini “suluhisho” hilo linalenga hasa kutosheleza hisia zako na linapuuza nadhiri uliyoweka mbele ya Mungu kwamba lolote na liwe, utashikamana na mwenzi wako.

 Unachoweza kufanya

 Azimia kuheshimu nadhiri yako ya ndoa. Mkiwa na msingi huo, mtaweza kushughulikia hali hiyo kwa pamoja badala ya kama watu wanaopingana.

 Kanuni ya Biblia: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.

 Hesabu gharama. Kwa mfano, tuseme mwenzi mmoja anataka kupata watoto lakini mwenzake hataki. Kuna mambo kadhaa ya kufikiria, kutia ndani:

  •   Uhusiano wenu ni imara kadiri gani?

     Je, ndoa yenu itaweza kustahimili mkazo wa kulea mtoto?

  •   Madaraka ya kuwa mzazi.

     Mengi zaidi yanahusika mbali na kuandaa chakula, mavazi, na makao.

  •   Hali yenu ya kifedha.

     Je, mnaweza kusawazisha kazi, familia, na majukumu mengine?

 Kanuni ya Biblia: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama?”—Luka 14:28.

 Fikiria sehemu zote za jambo hilo. Huenda mkafaulu kutatua mambo fulani ambayo hamkubaliani. Kwa mfano, ikiwa tatizo ni kuhusu kupata watoto, mwenzi ambaye anasita kupata watoto anaweza kujiuliza hivi:

  •   ‘Ninaposema kwamba sitaki kupata watoto, je, ninamaanisha kwamba sitaki kabisa au ni kwa sasa tu?’

  •   ‘Je, ninaogopa kwa sababu sidhani nitakuwa mzazi mzuri?’

  •   ‘Je, ninaogopa kwa sababu ninafikiri mwenzi wangu ataanza kunipuuza?’

 Kwa upande mwingine, mwenzi anayetaka kupata watoto anapaswa kufikiria maswali kama vile:

  •   ‘Je, tuko tayari kushughulikia majukumu ya kuwa wazazi?’

  •   ‘Je, tuna uwezo wa kifedha wa kumlea mtoto?’

 Kanuni ya Biblia: “Hekima inayotoka juu . . . ni . . . yenye usawaziko.”—Yakobo 3:17.

 Tambua faida ya maoni ya mwenzi wako. Watu wawili wanaweza kutazama tukio lilelile lakini wawe na maoni tofauti kulihusu. Vivyo hivyo, wenzi wa ndoa wanaweza kutaka kushughulikia jambo lakini kila mmoja awe na maoni yake kuhusu jinsi ya kulishughulikia—kwa mfano, jinsi ya kushughulikia pesa. Ili kuzungumzia hali yoyote ambayo mna maoni yanayotofautiana, anzeni na mambo mnayopatana.

  •   Mnakubaliana kuhusu malengo gani?

  •   Maoni ya kila mmoja wenu yana uzito gani?

  •   Ili kudumisha ndoa yenu ikiwa imara, je, mmoja wenu anaweza kubadili maoni yake au hata nyote wawili mbadili maoni yenu kwa kadiri fulani?

 Kanuni ya Biblia: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

a Mambo mazito yanapaswa kuzungumziwa kabla ya ndoa. Hata hivyo, hali zisizotarajiwa zinaweza kutokea, au hisia za mwenzi mmoja zinaweza kubadilika baada ya muda.—Mhubiri 9:11.