Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA SITA

Alimufungulia Mungu Moyo Katika Sala

Alimufungulia Mungu Moyo Katika Sala

1, 2. (a) Sababu gani Hana ni mwenye huzuni anapotayarisha safari yake? (b) Habari ya Hana inaweza kutufundisha nini?

HANA ana mambo mengi ya kufanya katika kutayarisha safari, anajaribu kufanya hivyo ili asahau matatizo yake. Huo ni wakati ambao kila mutu anapaswa kuwa na furaha; kila mwaka, Elkana, bwana yake, anaipeleka familia yake yote kwenye hema, huko Shilo, ili kuabudu. Yehova alisema kama pindi hizo zinapaswa kuwa pindi zenye kufurahisha. (Soma Kumbukumbu la Torati 16:15.) Na bila shaka, Hana alifurahia sikukuu hizo tangu utoto wake. Lakini, miaka hii ya karibuni, mambo yamemubadilikia sana.

2 Hana amebarikiwa kuwa na bwana anayemupenda. Lakini, bwana yake Elkana ana bibi wa pili, anayeitwa Penina. Na inaonekana kama Penina anakusudia kabisa kumukosesha Hana amani. Anafanya yake yote ili wakati wa sikukuu hizo, Hana asiwe na furaha hata kidogo. Namna gani? Na jambo la maana zaidi, namna gani imani ya Hana katika Yehova itamusaidia kushinda hali hiyo ambayo kwa kawaida ni nguvu sana kuvumilia? Kama una magumu yanayokukosesha furaha katika maisha, habari hii ya Hana itakutia moyo.

‘Kwa Nini Moyo Wako Una Huzuni?’

3, 4. Hana anapambana na matatizo makubwa gani mawili, na sababu gani kila tatizo si nyepesi?

3 Biblia inaeleza matatizo mawili makubwa ambayo Hana anapambana nayo. Yeye mwenyewe anaweza kumaliza tatizo la kwanza, lakini kuhusu lile la pili, hana uwezo hata kidogo. Tatizo la kwanza: Bwana ya Hana ana mwanamuke mwengine, na huyo mbanda yake anamuchukia sana. Tatizo la pili: Yeye ni tasa, ni kusema, hawezi kuzaa. Hali hiyo ni tatizo kabisa kwa mwanamuke yeyote anayetaka kuwa na watoto; na katika siku za Hana, katika maisha ya watu, hali hiyo ilihuzunisha sana. Sababu gani? Kwa sababu, kila familia ilitegemea watoto ili kuendelesha jina la familia. Kwa hiyo, mwanamuke kuwa tasa ilionekana ni mukoshi na jambo la haya sana.

4 Penina hangemusumbua Hana, labda angeweza kuvumilia tatizo hilo. Ndoa ya kuwa na mbanda si rahisi: kwa kawaida utakuta tu mambo ya kushindana, kugombana, na yenye kuhuzunisha moyo. Ni hivyo, kwa sababu ndoa hizo hazipatane na kanuni ambayo Mungu aliweka katika bustani ya Edeni kuhusu ndoa, ni kusema, bwana kuwa na bibi mumoja. (Mwa. 2:24) Hakuna andiko katika Biblia linaloonyesha kama kuoa wanawake zaidi ya mumoja ni jambo nzuri, na kwa hiyo, hali yenye kuhuzunisha inayopita katika familia ya Elkana inaonyesha wazi kwamba kuoa wanawake wengi si vizuri.

5. Sababu gani Penina anapenda kumutesa Hana, na anafanya nini ili moyo wa Hana uumie?

5 Elkana anamupenda Hana sana. Hadisi ya Wayahudi inaonyesha kwamba Hana ndiye bibi yake wa kwanza, na kisha miaka mingi baadaye ndipo anamuoa Penina. Iwe ilikuwa hivyo ao hapana, jambo la hakika ni kwamba, Penina anamusikilia Hana wivu sana, na kwa hiyo, anafanya yake yote ili kumutesa. Penina anajivuna kwa sababu yeye amezaa watoto. Kila mara anapozaa mutoto, kiburi chake kinapanda. Kuliko kumusikilia Hana huruma na kumufariji, yeye anaendelea kuingiza tena kisu katika kidonda cha Hana. Biblia inasema kwamba Penina alimusumbua Hana sana ili ‘kumufanya akasirike.’ (1 Sam. 1:6) Inaonekana kama Penina anafanya hivyo kimakusudi. Anapenda tu kumuumiza mwenzake moyoni, na anamuumiza kabisa.

Hana alihuzunika sana kwa sababu alikuwa tasa, na Penina alifanya yake yote ili kumukosesha amani

6, 7. (a) Ijapokuwa Elkana anajaribu kumufariji Hana, sababu gani Hana hapendi kumuelezea namna anavyotendewa? (b) Kwa sababu Hana alikuwa tasa, hilo linamaanisha kwamba Yehova hakuwa anapendezwa naye? Eleza. (Soma maelezo yaliyo chini.)

6 Penina anaona kwamba wakati muzuri kabisa wa kumukosesha Hana amani, ni wakati wanapatikana huko Shilo, kwenye sikukuu za kila mwaka. Penina ana watoto wengi. Elkana anapatia ‘wana na binti’ za Penina, sehemu ya zabihu ili kumutolea Yehova. Lakini, Hana hakuwa na watoto, kwa hiyo anapewa sehemu moja tu, kwa ajili yake mwenyewe. Penina anapandisha kabisa mabega na anamukumbusha Hana kwamba yeye ni tasa; basi, Hana anaanza kulia na anakosa hata hamu ya kula chakula. Elkana anaona kwamba Hana ana huzuni sana na anashindwa kula, kwa hiyo anajaribu kumufariji. Anamuuliza hivi: ‘Hana, kwa nini unalia, na kwa nini haukule chakula, na kwa nini moyo wako unahisi vibaya [ao una huzuni]? Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?’—1 Sam. 1:4-8.

7 Elkana anatambua kwamba Hana anahuzunika kwa sababu yeye ni tasa. Na bila shaka, Hana anafurahi kusikia maneno hayo yenye fazili ya Elkana, yanayomuhakikishia kwamba anamupenda. * Lakini, Elkana haseme lolote juu ya ubaya wa Penina, na Biblia haiseme kama Hana alimuelezea bwana yake namna anavyotendewa. Labda anaona kwamba kumuelezea Elkana mambo ya Penina, hilo linaweza tu kufanya mambo yachache zaidi. Je, Elkana atabadilisha kabisa jambo lolote? Je, hilo halitamuchochea Penina atende vibaya hata zaidi, na je, hilo halitafanya watoto na watumishi wa Penina wamusaidie katika kumushambulia Hana? Mambo yakiwa hivyo, basi, Hana ataendelea kujisikia kama mutu anayetupiliwa kabisa na watu wa nyumba yake.

Alipotendewa vibaya nyumbani, Hana alimwendea Yehova ili kupata faraja

8. Wakati watu wengine wanakuzarau ao wanakutendea bila haki, sababu gani ni jambo lenye kufariji kukumbuka kwamba Yehova ni Mungu wa haki?

8 Iwe Elkana alijua ao hakujua mambo yote ambayo Penina alikuwa anamutendea Hana, Yehova Mungu alikuwa anaona yote. Neno lake linasema hivyo, na yale linasema ni onyo kwa wote walio na tabia ya kuwasikilia wengine wivu na kuwachukia, iwe ni wivu kidogo ao chuki kidogo. Kwa upande mwengine, watu wasio na kosa na wenye kufanya amani kama Hana, wanaweza kufarijika kujua kwamba Mungu wa haki atatengeneza hali yao kwa namna yake na kwa wakati wake. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4.) Bila shaka, Hana anajua jambo hilo pia, kwa sababu anamuendea Yehova ili kupata musaada.

‘Uso Wake Hauna Tena Huzuni’

9. Hana alikuwa tayari kufanya safari ya Shilo ijapokuwa alijua namna mbanda yake atamutendea, mufano wake unaweza kutufundisha nini?

9 Asubuhi mapema kila mutu anajitayarisha kwa ajili ya safari, hata watoto pia. Familia itafanya safari hiyo ya kilometre 30 ili kufika Shilo, kupitia inchi ya Efraimu yenye milima​-milima. * Safari hiyo ni ya mwendo wa siku moja ao siku mbili. Hana anajua namna mbanda yake atamutendea. Hata hivyo, habaki nyumbani. Hana anaachia waabudu wote wa Mungu leo mufano muzuri sana. Si jambo la hekima kuacha kumuabudu Mungu kwa sababu ya mwenendo usiofaa wa wengine. Tukifanya hivyo, tutapoteza baraka ambazo zingetusaidia kuvumilia.

10, 11. (a) Sababu gani Hana anapopata nafasi mara moja anaenda kwenye hema la ibada? (b) Namna gani anamufungulia Baba yake wa mbinguni mahangaiko ya moyo wake katika sala?

10 Kisha kufanya safari ndefu kupitia milima iliyo na njia za lukumba​-lukumba, familia hiyo kubwa inakaribia Shilo. Muji huo uko juu ya mulima ambao unazungukwa na milima mingi mirefu. Wanapoendelea kukaribia Shilo, Hana anafikiri sana yale atakayomuelezea Yehova katika sala. Wanapofika tu, familia inakaa pamoja ili kula chakula. Wakati fulani, Hana anawaacha na anajielekeza kwenye hema ya ibada ya Yehova. Kuhani Mukubwa Eli yuko hapo, anakaa pembeni ya nguzo ya mulango wa hema. Lakini Hana hamuone kwa sababu anakazia tu Mungu wake mafikiri. Hapa kwenye hema ya ibada, iko hakika kwamba atasikiwa. Hata kama hakuna mutu anayeweza kuelewa taabu yake, Baba yake wa mbinguni anaweza kufanya hivyo. Anasikia uchungu sana moyoni na anaanza kulia.

11 Mwili wa Hana unatetemeka kwa sababu ya kulia, anazungumuza na Yehova kimoyo​-moyo. Midomo yake inatetemeka, anatafuta maneno ya kumuelezea Yehova ili kumuonyesha uchungu wake. Anasali kwa muda murefu, anamufungulia Baba yake mahangaiko ya moyo wake. Hana hamuombe tu Yehova amusaidie kuzaa, lakini zaidi ya baraka za Mungu anatamani pia kumutolea Mungu chochote ambacho angeweza. Kwa hiyo, anafanya naziri, anamuambia Yehova kwamba ikiwa anazaa mutoto mwanaume atamutolea Yehova mutoto huyo ili amutumikie.—1 Sam. 1:9-11.

12. Mufano wa Hana unatukumbusha nini kuhusu sala?

12 Kwa hiyo, Hana ni mufano muzuri sana kwa watumishi wote wa Mungu kuhusiana na sala. Yehova anawaomba wajisikie huru kuzungumuza naye, bila kusita, wamutupie mahangaiko ya moyo wao kama vile mutoto anayemutumainia baba yake. (Soma Zaburi 62:8; 1 Wathesalonike 5:17.) Mutume Petro aliongozwa na roho ya Mungu ili kuandika maneno haya yenye kufariji kuhusu sala zetu kwa Yehova: ‘Mutupe mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye [anawahangaikia] ninyi.’—1 Pet. 5:7.

13, 14. (a) Namna gani na sababu gani Eli anamuwazia Hana vibaya? (b) Namna gani jibu la Hana kwa Eli ni mufano muzuri sana wa imani?

13 Kwa kawaida, wanadamu hawawaelewe wengine na hawajitie pa nafasi ya wengine kama Yehova. Ndio sababu, Hana anaposali na kulia, sauti ya mutu fulani inamushitua. Ni sauti ya Eli, kuhani mukubwa, aliyekuwa anamutazama. Kuhani huyo anamuambia hivi: ‘Utaendelea kujiendesha kama mulevi mupaka wakati gani? Iondolee mbali divai yako.’ Eli anaona midomo ya Hana inatetemeka, ni mwenye kulia na mwenye uchungu sana. Kuliko kumuuliza magumu yake ni nini, yeye anawaza mara moja kwamba Hana ni mulevi.—1 Sam. 1:12-14.

14 Kulaumiwa bila sababu yoyote wakati huu wa taabu yake, zaidi sana na mwanaume aliye na cheo chenye kuheshimika, kunamuumiza Hana zaidi! Hata hivyo, mara hii tena, yeye anatuachia mufano muzuri wa imani. Haache kumuabudu Yehova kwa sababu ya uzaifu wa mutu fulani. Na anamujibu Eli kwa adabu na kumuelezea hali yake. Eli anatambua kwamba alikosea, kwa hiyo, labda ndio sababu anamujibu hivi kwa upole: ‘Nenda kwa amani, naye Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemuomba.’​—1 Sam. 1:15-17.

15, 16. (a) Kwa sababu Hana anamufungulia Yehova moyo, na anaendelea kumuabudu kwenye hema ya ibada, anajisikia namna gani? (b) Namna gani tunaweza kufuata mufano wa Hana tunapolemewa na magumu ao huzuni?

15 Matokeo yanakuwa namna gani wakati Hana anamufungulia Yehova moyo na anaendelea kumuabudu kwenye hema ya ibada? Biblia inasema hivi: ‘Mwanamuke huyo akaenda zake, akakula chakula, na uso wake haukuwa tena na huzuni.’ (1 Sam. 1:18, La Sainte Bible en Swahili de la R. D. Congo) Hana anajisikia mwenye kutulizwa. Tunaweza kusema kama alitia uzito wa mahangaiko yake kwenye mabega ya mutu mwenye nguvu sana kuliko yeye, ni kusema, Baba yake wa mbinguni. (Soma Zaburi 55:22.) Je, kuna tatizo lolote linaloweza kumushinda? Hakuna hata kidogo: iwe jana, iwe leo ao kesho!

16 Tunapojisikia kulemewa, magumu yanatupita ao tuna huzuni kupita kiasi, ni vizuri kufuata mufano wa Hana na kuzungumuza na Yehova ‘Musikiaji wa sala’ bila kusita. (Zab. 65:2) Tukifanya hivyo kwa imani, kuliko kuwa na huzuni, tutakuwa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Flp. 4:6, 7.

“Hakuna Mwamba Ulio Kama Mungu Wetu”

17, 18. (a) Ni nini inaonyesha kama Elkana anaunga mukono naziri ya Hana? (b) Penina hana tena uwezo gani juu ya Hana?

17 Asubuhi inayofuata, Hana anarudi tena kwenye hema pamoja na Elkana. Hakukosa kumuelezea bwana yake kuhusu ombi na naziri aliyofanya, kwa kuwa Sheria ya Musa inasema kwamba bwana ana haki ya kuvunja naziri ambayo bibi yake alifanya bila kumuuliza bwana yake maoni yake. (Hes. 30:10-15) Lakini, mwanaume huyo mwaminifu havunje naziri hiyo. Kuliko kufanya hivyo, yeye na Hana wanamuabudu Yehova pamoja kwenye hema mbele ya kushika njia yao na kurudi nyumbani.

18 Ni wakati gani kabisa Penina alitambua kuwa uchokozi wake haumuhuzunishe tena Hana? Biblia haizungumuzie jambo hilo, lakini maneno ‘uso wake haukuwa tena na huzuni,’ yanaonyesha kama kuanzia wakati huo Hana alirudiliwa na furaha yake. Kwa vyovyote, Penina aliona kama mazarau yake hayakuwa na matokeo juu ya Hana. Na Biblia haitaje tena jina la Penina.

19. Ni baraka gani ambayo Hana anapata, na namna gani anaonyesha kama alijua yule aliyemupatia baraka hiyo?

19 Miezi inapita, amani ya Hana inaongezeka na anakuwa mwenye furaha sana. Ni mwenye kuwa na mimba! Hana anafurahi sana, lakini hasahau hata kidogo ni nani amemubariki hivyo. Mutoto anapozaliwa, anamupatia jina la Samweli, linalomaanisha “Jina la Mungu,” na kwa kweli jina hilo linaonyesha tendo la kuitia jina la Mungu kama Hana alivyofanya. Mwaka huo Hana haende Shilo pamoja na Elkana na jamaa yote. Anabaki nyumbani pamoja na mutoto kwa miaka mitatu mupaka wakati mutoto anaachishwa kunyonya. Sasa anajitayarisha kwa ajili ya siku ambayo ataachana na mwana wake mupendwa.

20. Namna gani Hana na Elkana wanatimiza mambo waliyomuahidia Yehova?

20 Si jambo rahisi kwa Hana kuachana na mutoto wake. Bila shaka, Hana anajua kama Samweli atatunzwa vizuri huko Shilo; inaonekana ni wanawake fulani wanaotumika katika hema ya ibada ndio watamutunza. Hata hivyo, kijana Samweli angali bado mutoto sana na tunajua kwamba si vyepesi kwa mama kuachana na mutoto ambaye angali muchanga. Lakini, Hana na Elkana wanamupeleka mutoto huko kwenye nyumba ya Mungu, hawafanye hivyo wakiwa na kinyongo, lakini wanafanya hivyo kwa furaha. Wanatoa zabihu na kisha wanamuacha Samweli katika mikono ya Eli, wanamukumbusha Eli naziri ambayo Hana alifanya hapo miaka fulani iliyopita.

Hana alikuwa baraka kabisa kwa Samweli

21. Namna gani sala ya Hana inaonyesha kwamba alikuwa na imani yenye nguvu? (Soma pia kisanduku “Sala Mbili Zisizo za Kawaida.”)

21 Kisha Hana anatoa sala ambayo Mungu aliona kama inastahili kutiwa katika Neno lake lililoongozwa na roho. Unaposoma maneno ya Hana katika 1 Samweli 2:1-10, utaona kama kila mustari unaonyesha imani yenye nguvu ya mwanamuke huyo. Anamusifu Yehova namna anavyotumia kwa ajabu nguvu zake na uwezo wake usiolinganishwa ili kuwashusha wenye kujivuna, kuwabariki wanaoonewa, na namna alivyo na uwezo wa kuua na hata wa kuokoa kutoka katika kifo. Anamusifu Baba yake wa mbinguni kwa kuwa ni mutakatifu zaidi, ni mwenye haki, na ni mwaminifu. Hana ana haki ya kusema hivi: “Hakuna mwamba ulio kama Mungu wetu.” Yehova anastahili kabisa kutumainiwa, yeye habadilike, ni kimbilio kabisa kwa wote wanaoonewa na kugandamizwa na ambao wanamuomba musaada.

22, 23. (a) Sababu gani tuko hakika kwamba Samweli anaendelea kukomaa akiwa mwenye kujua kwamba wazazi wake wanamupenda? (b) Namna gani Yehova anaendelea kumubariki Hana?

22 Bila shaka, kijana Samweli ana pendeleo kabisa la kuwa na mama aliye na imani kama hiyo kwa Yehova. Hata ikiwa anakomalia mbali naye, hajisikie hata kidogo kuwa anasahauliwa. Kila mwaka, Hana anakuja Shilo; anamuletea koti lisilo na mikono ambalo Samweli atavaa anapomutumikia Yehova katika hema. Kumushonea yeye mwenyewe koti hilo kunaonyesha kama anamupenda na kumuhangaikia mwana wake. (Soma 1 Samweli 2:19.) Funga macho kidogo: unamuona Hana akimuvalisha kijana wake koti hilo, akilinyoosha, na kumutazama kwa upendo anapomutia moyo na kuzungumuza naye kwa fazili? Samweli ni mwenye kubarikiwa kabisa kuwa na mama kama huyo, naye anapoendelea kukomaa, anakuwa baraka kubwa kwa wazazi wake na kwa Waisraeli wote.

23 Yehova pia hamusahau Hana. Anafungua tumbo lake la uzazi kabisa, na anamuzalia Elkana watoto wengine watano. (1 Sam. 2:21) Hata hivyo, labda baraka kubwa ambayo Hana anapata ni uhusiano wa karibu sana alio nao pamoja na Baba yake Yehova, ambao unaendelea kuwa nguvu kadiri miaka inavyopita. Acha iwe hivyo pia kwako, wakati unapoendelea kuiga imani ya Hana.

^ fu. 7 Hata ikiwa Biblia inasema kama Yehova ‘alifunga tumbo la uzazi la Hana,’ hakuna jambo lolote linaloonyesha kama Mungu hakuwa anapendezwa na mwanamuke huyo munyenyekevu na mwaminifu. (1 Sam. 1:5) Wakati mwingine Biblia inaonyesha kwamba Mungu anaweza kuruhusu mambo fulani yatokee kwa muda fulani.

^ fu. 9 Wamekadiria umbali huo kutokana na wazo la kwamba muji wa Rama ndio uliokuwa muji wa Elkana, na muji huo ndio uliitwa Arimatea katika siku za Yesu.