Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA TATU

Makosa Yake Mwenyewe Yalimufundisha

Makosa Yake Mwenyewe Yalimufundisha

1, 2. (a) Kwa sababu ya makosa ya Yona, wafanyakazi wa mashua na Yona mwenyewe wanajikuta katika hali gani? (b) Maisha ya Yona yanaweza kutufundisha nini?

YONA anapenda kabisa kufunga masikio yake ili asisikie makelele yenye kusumbua sana. Si makelele ya ule upepo mukali tu unaoipiga ile mashua; wala si makelele ya mawimbi makubwa tu yanayoipiga mashua na kufanya mbao zake zisikiwe kama zinataka kuvunjika. Lakini, makelele yanayomusumbua sana ni yale ya kapiteni na wafanyakazi wa mashua wanaojikaza kufanya mashua isikumbwe ao kupelekwa na upepo. Yona iko hakika kwamba wanaume hao watakufa hivi karibuni, na ni kwa sababu yake!

2 Ni nini inayomufanya Yona apatikane katika hali hiyo mbaya? Amefanya kosa nzito kabisa, amekosa kumutii Mungu wake, Yehova. Kwa kweli, amefanya nini? Je, uhusiano wake na Yehova umeharibika kabisa? Majibu ya maulizo hayo yanaweza kutufundisha mambo mengi. Kwa mufano, maisha ya Yona yanaweza kutusaidia kujua kwamba hata wale walio na imani wanaweza kufanya makosa, hata hivyo, wanaweza kutengeneza mambo.

Nabii wa Galilaya

3-5. (a) Mara nyingi, watu wanapofikiri juu ya Yona wanaona zaidi nini? (b) Ni mambo gani machache ambayo Biblia inazungumuzia kuhusu Yona? (Soma maelezo yaliyo chini.) (c) Sababu gani kazi ya Yona ya kuwa nabii haikuwa kazi nyepesi na yenye kufurahisha?

3 Mara nyingi, watu wanapofikiri juu ya Yona, wanaona zaidi sana mambo mabaya aliyofanya; kama vile kukosa utii ao mutu mwenye kichwa kigumu. Lakini, Yona alifanya pia mambo mengi mazuri. Tusisahau kwamba Yehova Mungu alimuchagua Yona kuwa nabii wake. Ikiwa Yona hakuwa mutu mwaminifu ao mwenye haki, Yehova hangemuchagua na kumupa pendeleo hilo kubwa.

Ni kweli kwamba Yona alifanya mambo mabaya, lakini alifanya pia mambo mengi mazuri

4 Biblia inazungumuzia mambo machache tu kuhusu malezi ya Yona. (Soma 2 Wafalme 14:25.) Inasema yeye ni mutu wa Gath-heferi, muji uliopatikana kwenye kilometre ine tu kutoka Nazareti, muji ambako Yesu alikomalia miaka 800 hivi baadaye. * Yona alifanya kazi yake ya nabii wakati wa utawala wa Mufalme Yeroboamu wa Pili, aliyekuwa mufalme wa makabila kumi ya ufalme wa Israeli. Siku za Eliya zilikuwa zimekwisha kupita zamani; Elisha aliyemugomboa Eliya, alikuwa amekwisha kufa, wakati wa utawala wa baba ya Yeroboamu. Hata ikiwa Yehova alitumia wanaume hao ili kuangamiza ibada ya Baali, Waisraeli walikuwa tena wameanza kupotoka kimakusudi. Inchi ilikuwa yenye kutawaliwa sasa na mufalme ‘aliyeendelea kutenda yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’ (2 Fal. 14:24) Kwa hiyo, kazi ya nabii Yona haingekuwa nyepesi ao yenye kufurahisha. Hata hivyo, alifanya kazi hiyo kwa uaminifu.

5 Siku fulani, maisha ya Yona yanabadilika kwa gafula. Yehova anamupatia mugao ambao Yona anaona kuwa mugao mugumu sana. Yehova anamuomba Yona kufanya nini?

Simama, Uende Ninawi

6. Yehova anamupa Yona mugao gani, na sababu gani inaonekana kuwa ni mugao wenye kuogopesha?

6 Yehova anamuambia Yona: Simama, uende Ninawi ule muji mukubwa, ‘uutangazie kwamba ubaya wake umefika mbele zangu.’ (Yona 1:2) Ni vyepesi kuona sababu gani mugao huo ni wenye kuogopesha. Muji wa Ninawi unapatikana kwenye kilometre 800 hivi upande wa mashariki, mutu anaweza kutembea kwa miguu safari ya mwezi mumoja hivi. Si safari hiyo ndefu na ngumu ndio inayomuogopesha Yona, lakini kazi. Huko Ninawi, Yona anapaswa kuwatangazia Waasiria hukumu ya Yehova; watu hao wanajulikana sana kuwa wajeuri na hata wenye kutesa watu kinyama. Ikiwa kati ya watu wa Mungu ni wachache tu ndio waliomusikiliza, je, kuna tumaini lolote kwamba wapagani hao watamusikiliza? Atafanya nini sasa, kwa sababu ni yeye peke ndiye atakuwa mutumishi wa Yehova katika muji mukubwa huo wa Ninawi, ambao baadaye ulikuja kujulikana kuwa ni ‘muji wa umwangaji wa damu?’—Nah. 3:1, 7.

7, 8. (a) Sababu gani tunaweza kusema kwamba Yona aliazimia kabisa kukimbia mugao ambao Yehova alikuwa amemupatia? (b) Sababu gani hatupaswe kumuhukumu Yona haraka na kusema kwamba alikuwa mwoga?

7 Hatujue kabisa ikiwa mawazo hayo yalimupitia Yona katika akili. Lakini jambo tunalojua ni kwamba alikimbia mugao wake. Yehova alimuambia aende upande wa mashariki, lakini Yona anaenda upande wa mangaribi, na anajaribu kuenda mbali kadiri anavyoweza. Anashuka kwenye bandari ya Yopa, mahali anapopata mashua inayoenda Tarshishi. Watu fulani wenye elimu ya mambo ya Biblia wanasema kwamba muji wa Tarshishi ao Tarsisi ulikuwa huko Espanye. Ikiwa ni hivyo, basi mahali ambapo nabii Yona alikuwa anaenda ni kilometre 3 500 hivi kutoka Ninawi. Katika siku hizo, safari kama hiyo ya kuenda mupaka ule upande mwengine wa Bahari Kubwa (Mediteranea) ilikuwa inachukua karibu mwaka mumoja. Kwa hiyo, inaonekana kwamba Yona alikuwa kabisa mwenye kuazimia kukimbia mugao ambao Yehova alikuwa amemupatia!—Soma Yona 1:3.

8 Je, hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kumuona Yona kuwa mutu mwoga? Hatupaswe kumuhukumu hivyo haraka. Kama tutakavyoona, kuna mambo mengi Yona alifanya ambayo iliomba mutu kuwa na ujasiri ili ayafanye. Lakini, kama vile sisi wote, Yona alikuwa mutu asiye mukamilifu, alikuwa na uzaifu wake pia. (Zab. 51:5) Ni nani kati yetu ambaye hajawahi hata siku moja kuwa na woga?

9. Nyakati nyingine, sisi pia tunaweza kujisikia namna gani kuhusu mugao ambao Mungu ametupatia, na ni ukweli gani hatupaswe kusahau katika hali kama hizo?

9 Nyakati nyingine tunaweza kufikiri kwamba jambo ambalo Mungu anatuomba tufanye ni ngumu, ao hata ni jambo lisilowezekana. Kwa mufano, sisi Wakristo tunaombwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, lakini wakati mwengine tunaweza hata kuogopa kuenda kuhubiri. (Mt. 24:14) Tunaweza pia kusahau kwa urahisi ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Mk. 10:27) Ikiwa sisi pia wakati mwengine tunasahau ukweli huo, labda tunaweza kuelewa magumu ya Yona. Sasa, Yona anapokimbia anapatwa na nini?

Yehova Anamufundisha Nabii Wake

10, 11. (a) Inawezekana Yona anafikiri nini anapoona mashua inaanza safari? (b) Ni hatari gani inayoifikia mashua na wafanyakazi wa mashua?

10 Wazia namna Yona anavyokaa katika mashua akingojea safari, labda mashua hiyo ilikuwa mashua ya Wafoinike ya kubeba mizigo. Anaangalia namna kapiteni na wafanyakazi wa mashua wanavyofanya ili mashua iondoke katika bandari na kuanza safari. Yona anapoona kwamba wameacha inchi kavu na wamekuwa mbali, anafikiri kwamba ameponyoka hatari aliyokuwa anaogopa. Lakini, kwa gafula hali ya hewa inachafuka.

11 Upepo wenye nguvu sana unafanya bahari itomboke kabisa na mawimbi yanapiga sana, mawimbi ambayo yangeweza kufanya hata zile mashua kubwa za wakati wetu zionekane kuwa si kitu. Itachukua muda gani kwa mashua hiyo ndogo ya mbao, isiyo na nguvu, kutupwa huku na huku na mawimbi hayo? Kufikia wakati huo, je, Yona anajua yale aliyoandika baadaye kwamba ‘Yehova mwenyewe ndiye aliyevumisha upepo mukubwa baharini’? Hatujue. Hata hivyo, Yona anaona namna wafanyakazi wa mashua wanavyoanza kuililia miungu yao mbalimbali, na anajua vizuri kwamba miungu hiyo haiwezi kuwasaidia. (Law. 19:4) Yona aliandika hivi: “Nayo [mashua] ikawa karibu kuvunjika.” (Yona 1:4) Naye Yona angesali namna gani kwa Mungu ambaye yeye alikuwa anakimbia?

12. (a) Sababu gani hatupaswe kumuhukumu Yona harakaharaka kwa kuwa analala wakati zoruba ni yenye kutomboka? (Soma maelezo yaliyo chini.) (b) Namna gani Yehova anafunua sababu ya zoruba hiyo?

12 Kwa kuwa Yona anaona kwamba hana lolote la kufanya ili kusaidia, anashuka katika sehemu za ndani kabisa za mashua na anajipatia nafasi ya kulala. Na huko analala fofofo. * Kapiteni anamukuta Yona analala humo, anamuamusha, na anamuambia yeye pia amuombe mungu wake, kama vile kila mutu anavyofanya. Kwa sababu wanaamini kwamba hiyo si zoruba ya kawaida, wafanyakazi wa mashua wanapiga kura ili kujua ni nani anayewaletea taabu hiyo. Bila shaka, Yona anaogopa tena zaidi anapoona namna kila mumoja anavyopita bila kukamatwa na kura hiyo. Bila kukawia, ukweli unajulikana. Yehova anafanya kura imuangukie Yona ili kuonyesha sababu gani kuna zoruba hiyo.—Soma Yona 1:5-7.

13. (a) Yona anawaambia wafanyakazi wa mashua nini waziwazi? (b) Anawaomba wafanye nini, na sababu gani?

13 Yona anawafunulia wafanyakazi wa mashua kila jambo. Anawaambia kwamba yeye ni mutumishi wa Mungu Mweza Yote, Yehova. Kwamba amemukosea Mungu huyo na kumukimbia, na ni kwa sababu hiyo wako katika hatari. Watu hao wanashituka sana; woga unaonekana kwenye nyuso zao. Sasa wanamuuliza jambo wanalopaswa kufanya ili kuokoa mashua hiyo na uzima wao. Yona atawaambia nini? Labda Yona anaogopa sana anapofikiria namna atazama katika bahari hiyo yenye kuchafuka na yenye maji baridi. Lakini, je, inawezekana kabisa Yona awaache wanaume wote hao wakufe wakati yeye anajua kwamba anaweza kuwaokoa? Hapana! Kwa hiyo anawaambia hivi: ‘Muninyanyue na kunitupa baharini, nayo bahari itatulia kwa ajili yenu; kwa maana najua kwamba ni kwa sababu yangu tufani [ao upepo mukali] hii kubwa imewajia.’—Yona 1:12.

14, 15. (a) Namna gani tunaweza kuiga imani ya Yona? (b) Je, wafanyakazi wa mashua walikubali mara moja yale Yona aliwaambia wamufanyie?

14 Je, mutu mwenye woga anaweza kweli kusema hivyo? Hakika Yehova alifurahi sana alipoona ujasiri na kujitoa kwa nabii wake katika wakati huo mugumu. Hapa tunaona kweli kwamba Yona anaonyesha imani yenye nguvu. Leo tunaweza kuiga imani ya Yona kwa kutanguliza faida za wengine. (Yoh. 13:34, 35) Tunapoona mutu mwengine ana lazima ya kusaidiwa kwa sababu anakosewa, ana lazima ya kufarijiwa kwa sababu ya huzuni, ao ana lazima ya kujifunza kweli ao kutiwa moyo, je, tuna roho ya kujitoa kabisa ili kumusaidia? Tukisaidia mutu kama huyo, Yehova atapendezwa sana!

15 Labda wafanyakazi wa mashua walimusikilia Yona huruma, kwa sababu mwanzoni walikataa kufanya kama alivyowaambia! Kwa hiyo, walifanya yao yote ili wapenye zoruba hiyo, lakini haikuwezekana. Bahari ilizidi tu kuchafuka. Mwishowe, waliona kama hawana jambo lingine la kufanya. Walimuomba Yehova, Mungu wa Yona, awahurumie, basi wakamunyanyua Yona na kumutupa katika bahari.—Yona 1:13-15.

Yona anawaomba wafanyakazi wa mashua wamunyanyue na kumutupa katika bahari

Mungu Anamuonyesha Yona Rehema na Anamuokoa

16, 17. Fasiria namna Yona alivyojisikia wakati alipatikana katika bahari. (Ona pia picha, hapa chini.)

16 Yona anatumbukia ndani ya bahari iliyo na mawimbi yenye kutomboka. Labda anajaribu kuogelea, lakini anaona namna mashua inavyokumbwa haraka na mawimbi hayo makubwa yenye pofu. Mawimbi hayo yanamuzamisha; anazidi kuzama chini kabisa na anajisikia kuwa hana tena tumaini lolote.

17 Baadaye Yona alieleza namna alivyojisikia wakati huo. Anafikiria mambo fulani katika maisha yake. Anafikiri kwa huzuni yote kwamba hataliona tena hekalu nzuri la Yehova lililo Yerusalemu. Anajisikia kuwa anashuka katika vilindi vya bahari kubwa, mupaka sehemu za chini kabisa za milima, mahali ambako magugu yanamuzunguka. Huko inaonekana kuwa ndilo shimo lake, ao kaburi lake.​—Soma Yona 2:2-6.

18,19. Ni nini inamufikia Yona katika vilindi vya bahari kubwa, ni kiumbe gani kinatumwa na ni nani aliyekuwa akifanya mambo hayo? (Soma maelezo yaliyo chini.)

18 Lakini, tazama, anaona kitu kikubwa, cheusi kinachotembea na kinamukaribia. Kinamukaribia zaidi na kinafungua kinywa kabisa na kumumeza!

Yehova alitayarisha ‘samaki mukubwa amumeze Yona’

19 Basi, Yona anaona huo kuwa mwisho wake. Lakini, anashangazwa na jambo fulani. Bado yeye iko muzima! Hasagwe-sagwe wala kupondwa​-pondwa, wala hata kusongwa pumuzi. Ni mwenye kupumua, hata ikiwa iko katika kaburi lake. Polepole, Yona anaanza kuingiwa na woga. Hakuna shaka, ni Mungu wake, Yehova ndiye ametayarisha ‘samaki mukubwa amumeze Yona.’ *Yona 1:17.

20. Sala ambayo Yona alitoa alipokuwa katika tumbo la samaki mukubwa inatufundisha nini?

20 Dakika zinapita, saa zinapita. Yona iko sasa katika giza kubwa zaidi ambalo hajawahi kuona, na humo anaanza tena kufikiri sana na kisha anasali kwa Yehova Mungu. Sala ya Yona tunayosoma katika Sura ya pili ya kitabu chake inaweza kutufundisha mambo mengi kuhusu nabii huyo. Inaonyesha kwamba Yona alikuwa na ujuzi mwingi wa Maandiko, kwa sababu sala hiyo inataja mara nyingi maneno yaliyo katika Zaburi. Pia, inaonyesha sifa fulani nzuri ya Yona: alikuwa mutu mwenye shukrani. Nabii huyo anamalizia sala yake hivi: ‘Lakini mimi, kwa sauti ya kutoa shukrani nitakutolea zabihu. Nilichoweka naziri, nitakitimiza. Wokovu ni wa Yehova.’—Yona 2:9.

21. Yona anajifunza nini kuhusu wokovu, na ni somo gani la lazima ambalo tunapaswa kukumbuka?

21 Yona anajifunza kwamba ikiwa Yehova anaweza kusikia sala zake na kumusaidia hata “ndani ya tumbo la samaki,” basi, anaweza kusaidia watumishi wake mahali popote walipo, katika hali yoyote na wakati wowote. Ndiyo, hata humo, Yehova alimuona na kumusaidia mutumishi wake aliyekuwa katika taabu. (Yona 1:17) Ni Yehova tu ndiye anayeweza kumulinda mutu muzima katika tumbo la samaki mukubwa siku tatu muchana na usiku. Ni vizuri kila mara kukumbuka kwamba ‘pumuzi yetu imo mikononi’ mwa Yehova Mungu. (Dan. 5:23) Tunapopumua, hata kidogo tu, na tunapoishi ni kwa sababu ya mapenzi yake. Je, sisi ni wenye shukrani? Kwa hiyo, hauone kwamba inatuomba tumutii kabisa Yehova?

22, 23. (a) Namna gani sifa ya Yona ya kuonyesha shukrani ilijaribiwa? (b) Tunapofanya makosa, namna gani tunaweza kumuiga Yona?

22 Yona alifanya nini? Je, alijifunza kumuonyesha Yehova shukrani kwa kumutii? Ndiyo. Kisha siku tatu, muchana na usiku katika tumbo la samaki, samaki huyo alimupeleka Yona na ‘akamutapika inchi kavu.’ (Yona 2:10) Fikiria jambo hili: baada ya mambo hayo yote, haikuwa lazima Yona aogelee mupaka inchi kavu! Bila shaka, ilimuomba sasa ajue mahali ataenda, ili atoke mahali hapo ambako samaki alimutapika. Sifa yake ya kuonyesha shukrani ilijaribiwa. Andiko la Yona 3:1, 2 linasema hivi: ‘Ndipo neno la Yehova likamujia Yona mara ya pili, na kusema: Ondoka, uende Ninawi ule muji mukubwa, ukautangazie neno ninalokuambia.’ Yona atafanya nini sasa?

23 Yona hakusita. Tunasoma hivi: ‘Basi Yona akasimama na kuenda Ninawi kulingana na neno la Yehova.’ (Yona 3:3) Ndiyo, anatii. Ni wazi kwamba makosa yake mwenyewe yalimufundisha. Katika jambo hilo pia tunapaswa kuiga imani ya Yona. Sisi wote tunafanya zambi, sisi wote tunafanya makosa. (Rom. 3:23) Je, tutavunjika moyo ao tutaacha pia makosa yetu yatufundishe na kuwa sasa watumishi watiifu wa Mungu?

24, 25. (a) Yona alipata zawadi gani wakati huo? (b) Ni zawadi gani inamungojea wakati ujao?

24 Je, Yehova alimupa Yona zawadi kwa sababu ya utii wake? Ndiyo. Kwanza, inaonekana kwamba baadaye Yona alipata habari kwamba wafanyakazi wa ile mashua hawakufa. Zoruba ilitulia mara moja kisha Yona kujitoa, na wafanyakazi hao ‘wakaanza kumuogopa sana Yehova’ na wakamutolea zabihu kuliko kuitolea miungu yao ya uongo.—Yona 1:15, 16.

25 Zawadi kubwa zaidi ilikuja baadaye. Yesu alifananisha kwa njia ya kiunabii wakati ambao Yona alikuwa ndani ya tumbo la samaki huyo mukubwa na muda ambao angepitisha katika kaburi, ao Sheoli. (Soma Mathayo 12:38-40.) Wakati Yona atafufuliwa ili kuishi duniani, atafurahi sana kujua jambo hilo! (Yoh. 5:28, 29) Yehova ana nia ya kukubariki wewe pia. Kama Yona, je, wewe pia utajiacha ufunzwe na makosa yako na kisha uwe mutiifu kwa Mungu na uonyeshe roho ya kujitoa?

^ fu. 4 Kujua kwamba Yona alikuwa mutu wa Galilaya ni jambo la lazima kabisa, kwa sababu Mafarisayo walisema hivi kwa kiburi kumuhusu Yesu: “Chunguza na uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.” (Yoh. 7:52) Watafsiri na wachunguzi wengi wanasema kwamba Mafarisayo walikuwa wakizungumuza kwa ujumla na kwa kupitisha kiasi kwa kusema kwamba Galilaya, muji wa hali ya chini, haujawahi kutosha nabii ao hakuna nabii atakayetoka huko. Ikiwa ndivyo walivyomaanisha, basi Mafarisayo walipuuza historia na pia unabii.—Isa. 9:1, 2.

^ fu. 12 Tafsiri ya Biblia ya Septante inasema Yona alikuwa anakoroma ili kuonyesha kwamba alikuwa mwenye kulala fofofo. Hata hivyo, hatupaswe kuwaza mara moja kwamba alifanya hivyo kwa sababu hakuwa mwenye kuhangaikia wengine; tunapaswa kukumbuka kwamba wakati mwengine watu wanaovunjika moyo wanapatwa na usingizi muzito. Wakati Yesu alikuwa na uchungu mwingi katika bustani ya Gethsemane, Petro, Yakobo, na Yohana walikuwa wenye ‘kusinzia kwa huzuni.’—Lu. 22:45.

^ fu. 19 Neno lililotafsiriwa “samaki” linamaanisha “munyama mukubwa wa baharini” katika Kiebrania, ao “samaki mukubwa” katika Kigiriki. Ingawa hakuna njia ya kuhakikisha ni kiumbe gani wa baharini anayetajwa, imevumbuliwa kwamba katika Bahari ya Mediteranea kuna papa (requins) wakubwa wanaoweza kumumeza mutu muzima. Kuna papa wakubwa zaidi katika maeneo mengine. Kwa mufano, kuna papa-nyangumi (baleine-requin) anayeweza kufikia urefu wa metre 15, na hata zaidi!