Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walijitoa kwa Kujipendea Katika Ufilipino

Walijitoa kwa Kujipendea Katika Ufilipino

MIAKA karibu kumi iliyopita, Gregorio na Marilou bibi yake, walio na miaka 30 hivi, walikuwa mapainia katika muji wa Manila na wakati huohuo walikuwa na kazi ambazo ziliwachukua wakati mwingi. Haikuwa rahisi, lakini waliweza. Kisha, Marilou alipandishwa cheo kazini na kuwa mukubwa wa benki. Anasema hivi: “Kazi zetu zilitusaidia kuwa na maisha mazuri sana.” Familia hiyo ilipata feza nyingi, na kwa hiyo iliamua kujenga nyumba ambayo walitamani kujenga tangu zamani katika eneo nzuri sana linalopatikana umbali wa kilometre 19 hivi mashariki mwa muji wa Manila. Walifanya mapatano na kompanyi moja ili iwajengee nyumba na walikubaliana na kompanyi hiyo kwamba wangekuwa wanalipa kiasi fulani cha feza kila mwezi kwa muda wa miaka kumi.

“NILIJISIKIA KWAMBA NILIKUWA NIKIMUIBA YEHOVA”

Marilou anaeleza hivi: “Kazi yangu mupya ilinichukua wakati na nguvu nyingi, kwa hiyo bidii yangu kwa ajili ya mambo ya kiroho ilianza kupunguka. Nilijisikia kwamba nilikuwa nikimuiba Yehova. Singeweza tena kumutolea Yehova wakati ambao nilikuwa nimeazimia kupitisha katika kazi yake.” Gregorio na Marilou hawakufurahia hali hiyo. Kwa hiyo, siku moja walikaa pamoja na kuzungumuza kuhusu maisha yao. Gregorio anasema hivi: “Tulipenda kufanya mabadiliko lakini hatukujua tuanzie wapi kabisa. Kwa kuwa hatuna watoto, tulizungumuzia namna tunavyoweza kutumia maisha yetu ili kumutumikia Yehova zaidi. Tulimuomba Yehova atuongoze.”

Wakati huo, walisikia hotuba nyingi kuhusu kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri. Gregorio anasema hivi: “Tulitambua kwamba hotuba hizo zilikuwa jibu la Yehova kwa sala zetu.” Gregorio na Marilou walisali Yehova awape imani zaidi na ujasiri wa kuchukua uamuzi muzuri. Tatizo kubwa lilikuwa mupango wao wa kujenga nyumba uliokuwa ukiendelea. Walikuwa tayari wamelipa feza za miaka mitatu. Wangefanya nini basi? Marilou anasema hivi: “Ikiwa tungevunja mapatano tuliyofanya, tungepoteza feza zote ambazo tulikuwa tumekwisha kulipa, zilikuwa feza nyingi kabisa. Lakini tuliona kwamba tulipaswa kuchagua ikiwa tungetia pa nafasi ya kwanza mapenzi ya Yehova ao tamaa zetu wenyewe.” Walikumbuka maneno ya mutume Paulo kuhusu ‘kukubali hasara,’ kwa hiyo waliacha mupango wao wa kujenga nyumba, waliacha kazi zao, waliuzisha sehemu kubwa ya vitu vyao, na kuhamia katika kijiji cha mbali kwenye kisiwa cha Palawani, kinachopatikana umbali wa kilometre 480 hivi kusini mwa muji wa Manila.​—Flp. 3:8.

‘WALIJIFUNZA SIRI’

Mbele ya kuhama, Gregorio na Marilou walikuwa wamejaribu kuona namna gani wanaweza kuishi maisha rahisi, lakini walitambua waziwazi kwamba walipaswa kuishi maisha ya chini sana walipofika katika eneo lao. Marilou anasema hivi: “Lilikuwa jambo la kuvunja moyo kabisa. Hakukuwa na umeme, ao vitu vingine vya lazima. Kuliko kupika wali kwenye chombo cha kupikia kinachotumia umeme, tulipaswa kuvunja kuni ili kupika chakula. Nilikumbuka namna nilivyokuwa nikienda kwenye maduka, kukulia kwenye restora, na mambo mengine ambayo nilifurahia katika muji.” Lakini, waliendelea kufikiria sababu gani walihama, na kisha muda kidogo walizoea. Marilou anasema hivi: “Ninafurahia sasa kutazama uzuri wa uumbaji, kutia ndani nyota zenye kungaa usiku. Zaidi ya yote, inafurahisha sana kuona namna watu wanavyofurahi tunapowahubiria. ‘Tumejifunza siri’ ya kutosheka kwa kutumikia hapa.”​—Flp. 4:12.

“Hakuna jambo linaloshinda furaha ambayo tumepata kwa kuona watu wakifanya maendeleo ya kiroho. Tumetambua kwamba maisha yetu ni yenye maana zaidi kuliko zamani.”​—Gregorio na Marilou

Gregorio anaeleza hivi: “Tulipofika hapa, kulikuwa Mashahidi wane tu. Walifurahi sana wakati nilianza kutoa hotuba ya watu wote kila juma na kufuatana nao kwa gitari yangu wanapoimba nyimbo za Ufalme.” Kwa mwaka mumoja, Gregorio na Marilou walijionea namna kikundi hicho kidogo kiligeuka kuwa kutaniko lenye kuendelea vizuri la wahubiri 24. Gregorio anasema hivi: “Upendo ambao kutaniko hili linatuonyesha unatugusa moyo sana.” Wanapofikiria miaka zaidi ya sita ambayo wamefanya katika eneo hilo la mbali wanasema hivi: “Hakuna jambo linaloshinda furaha ambayo tumepata kwa kuona watu wakifanya maendeleo ya kiroho. Tumetambua kwamba maisha yetu ni yenye maana zaidi kuliko zamani.”

“NIMEONJA NA KUONA YA KUWA YEHOVA NI MWEMA!”

Katika inchi ya Ufilipino, ndugu na dada karibu 3 000 wamehamia katika maeneo ambako kuna lazima kubwa ya wahubiri wa Ufalme. Kati yao kuna dada 500 hivi wasioolewa. Fikiria mufano wa dada Karen.

(Picha ya kushoto) Karen

Karen, aliye sasa na miaka 20 hivi, alikomalia katika muji wa Baggao, Cagayan. Alipokuwa angali kijana, kila mara alifikiria namna angeweza kupanua utumishi wake. Anaeleza hivi: “Kwa kuwa nilijua kwamba wakati ambao umebaki ni muchache na kwamba watu wa aina yote wanahitaji kusikia ujumbe wa Ufalme, nilitaka kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa zaidi ya wahubiri.” Washiriki wachache katika familia yake walimutia moyo asome masomo ya juu kuliko kuenda kuhubiri katika maeneo ya mbali, lakini Karen aliomba Yehova amuongoze. Alizungumuza pia na wale wanaotumikia katika maeneo ya mbali. Alipokuwa na miaka 18, alihamia katika eneo lililopatikana umbali wa kilometre 64 hivi na muji wa kwao.

Kutaniko ndogo ambalo Karen alienda kutegemeza linahubiri katika eneo la mulimani pembeni ya Bahari ya Pasifiki. Karen anaeleza hivi: “Kutoka Baggao mupaka mahali ambapo kutaniko jipya lilipatikana, tulipaswa kutembea siku tatu, tukipanda milima na kushuka mabonde na kuvuka mito mara 30.” Anaongezea hivi: “Ili kufikia wanafunzi fulani wa Biblia, nilitembea saa sita, nilibaki usiku muzima katika nyumba ya mwanafunzi wa Biblia, na siku iliyofuata nilitembea saa sita ili kurudi nyumbani.” Je, alipata matokeo mazuri kwa kufanya yote hayo? Karen anasema hivi kwa furaha kubwa: “Mara nyingi, miguu yangu inauma, lakini nimeongoza mafunzo 18 ya Biblia. ‘Nimeonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema’!”​—Zab. 34:8.

“NIMEJIFUNZA KUMUTEGEMEA YEHOVA”

(Picha ya kuume) Sukhi

Ni nini iliyomuchochea Sukhi, dada asiyeolewa aliye na miaka 40 hivi, na anayeishi Amerika, kuhamia Ufilipino? Katika 2011, alihuzuria mukusanyiko wa muzunguko ambako bibi na bwana waliulizwa kuhusu utumishi wao. Walieleza namna walivyouzisha sehemu kubwa ya vitu vyao ili waende kuhubiri huko Meksiko. Dada Sukhi anasema kwamba “sehemu hiyo ya kuuliza maulizo ilimusaidia aanze kufikiria miradi ambayo alikuwa hajafikiria hapo zamani.” Sukhi, ambaye ni wa asili ya India, aliposikia kwamba kulikuwa na lazima kubwa ya kuwahubiria Wahindi wanaozungumuza Kipunjabi na ambao wanaishi huko Ufilipino, aliamua kuenda kuwasaidia. Je, alipambana na matatizo fulani?

Sukhi anasema hivi: “Sikutazamia kwamba ni vigumu sana kuamua ikiwa nitauzisha vitu gani na kubaki na vitu gani. Pia, kisha kuishi maisha mazuri kwa miaka 13 katika nyumba yangu mwenyewe, nilihamia katika familia moja na niliishi maisha ya hali ya chini. Haikuwa rahisi, lakini ilikuwa njia nzuri ya kunisaidia nijitayarishe kuishi maisha rahisi.” Ni matatizo gani ambayo alikutana nayo kisha kuhamia huko Ufilipino? Anaongezea hivi: “Matatizo makubwa ambayo nilipambana nayo ilikuwa kukumbuka nyumbani na kuogopa kunguni (vidudu vinavyojificha kwenye kitanda na vinavyonyonya damu). Nilijifunza kumutegemea zaidi Yehova kuliko hapo zamani!” Je, amepata matokeo mazuri? Sukhi anasema hivi kwa kicheko: “Yehova anatuambia, ‘Munijaribu, kama sitawamwangia baraka.’ Nilijionea ukweli wa maneno hayo wakati musikilizaji mumoja niliyekuwa nikihubiria aliniuliza, ‘Utarudi huku wakati gani? Ningali na maulizo mengi.’ Kuwasaidia watu wenye njaa ya kiroho kunaniletea furaha nyingi na kutosheka!” (Mal. 3:10) Sukhi anaongezea hivi: “Kwa kweli, haikuwa rahisi kabisa kuchukua uamuzi wa kuhama. Lakini, kisha kuhamia hapa, nilishangaa sana kuona namna Yehova alivyotosheleza mahitaji yangu.”

“NILISHINDA WOGA WANGU”

Sime, ndugu aliye na bibi na aliye na miaka 30 hivi, aliondoka Ufilipino na kuenda kufanya kazi nzuri katika inchi moja ya Mashariki ya Kati. Alipokuwa huko, kitia-moyo alichopata kutoka kwa mwangalizi wa muzunguko na katika hotuba ya mushiriki wa Baraza Linaloongoza kilimuchochea Sime kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza. Sime anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi nilipofikiria kuacha kazi yangu.” Hata hivyo, aliacha kazi yake na kurudi Ufilipino. Leo, Sime na bibi yake anayeitwa Haidee, wanatumikia huko Davao del Sur, katika sehemu ya kusini mwa inchi yao, ambako wahubiri wanahitajiwa ili kuhubiri eneo lote. Sime anasema hivi: “Ninapofikiria uamuzi niliofanya, ninafurahi sana kwa kuwa nilishinda woga wangu wa kupoteza kazi na kwamba nilitia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza. Hakuna jambo linaloleta furaha maishani kuliko kumutolea Yehova kitu kizuri zaidi!”

(Picha ya kushoto) Sime na Haidee

“TUMETOSHEKA SANA!”

Wakati Ramilo na bibi yake Juliet, ambao wana miaka 30 hivi, walisikia kwamba kutaniko moja linalopatikana umbali wa kilometre 30 hivi na nyumbani kwao lilihitaji musaada, walijitolea kuenda kulitegemeza. Kwa hiyo kila juma, katika majira ya mvua ao joto, Ramilo na Juliet walisafiri kwa pikipiki yao ili kuhuzuria mikutano na kuhubiri. Hata ikiwa haikuwa rahisi kusafiri katika barabara mbaya na vilalo vyenye kuninginia, walifurahia uamuzi wao wa kupanua utumishi wao. Ramilo anasema hivi: “Mimi na bibi yangu tunaongoza pamoja mafunzo ya Biblia 11! Inaomba kuwa na roho ya kujitoa ili kutumikia mahali ambako kuna lazima ya wahubiri, lakini kufanya hivyo kunaleta furaha nyingi!”​—1 Kor. 15:58.

(Picha ya kuume) Juliet na Ramilo

Je, ungependa kujua mengi kuhusu kutumikia mahali ambako kuna lazima kubwa ya wahubiri katika inchi yako ao katika inchi nyingine? Ikiwa ndiyo, zungumuza na mwangalizi wako wa muzunguko, na usome habari Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’? katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Mwezi wa 8, 2011.