Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sala Iliyotayarishwa Vizuri Inatufundisha Nini?

Sala Iliyotayarishwa Vizuri Inatufundisha Nini?

“Na walibariki jina lako tukufu.”​—NEH. 9:5.

1. Tutazungumuzia mukusanyiko gani wa watu wa Mungu, na hilo linatokeza maulizo gani?

 ‘MUSIMAME, mumubariki Yehova Mungu wenu milele na milele.’ Kupitia maneno hayo yenye kuchochea, Walawi waliwaalika Waisraeli wakusanyike pamoja na kusali kwa Yehova. Siku hiyo, Walawi walitoa sala ndefu kuliko sala zote zinazozungumuziwa katika Biblia. (Neh. 9:4, 5) Mukusanyiko huo ulifanywa huko Yerusalemu siku 24 ya mwezi wa saba wa Kiyahudi unaoitwa Tishri, mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Tunapochunguza sababu gani mukusanyiko huo wa pekee ulifanywa, jiulize hivi: ‘Ni jambo gani nzuri lililofanya siku hiyo iwe ya maana sana? Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na sala ya Walawi iliyotayarishwa vizuri?’​—Zab. 141:2.

MWEZI WA PEKEE

2. Waisraeli walituachia mufano gani walipokusanyika kisha kumaliza kujenga upya kuta za Yerusalemu?

2 Mwezi mumoja mbele ya mukusanyiko huo, Wayahudi walikuwa wamemaliza kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Neh. 6:15) Watu wa Mungu walimaliza kazi hiyo katika siku 52 tu, na kisha walianza kufikiria sana mahitaji yao ya kiroho. Kwa hiyo, siku ya kwanza ya mwezi uliofuata, unaoitwa Tishri, walikusanyika pamoja kwenye kiwanja cha watu wote ili kumusikiliza Ezra, na Walawi wengine, wakisoma kwa sauti na kufasiria Sheria ya Mungu. Familia nzima, kutia ndani “wote wenye akili ya kutosha kuweza kusikiliza,” walisimama na kusikiliza ‘kuanzia mapambazuko [asubuhi sana] mupaka katikati ya muchana.’ Huo ni mufano muzuri kwa wengi kati yetu leo tunaohuzuria mikutano katika Majumba mazuri ya Ufalme! Lakini, je, wakati fulani akili yetu inaanza kutangatanga na tunaanza kufikiria mambo yasiyo ya maana tunapokuwa kwenye mikutano? Ikiwa ndiyo, tufikirie tena mufano wa Waisraeli wa zamani ambao hawakusikiliza tu lakini pia waliguswa moyo na mambo waliyosikia, na hilo liliwafanya waanze kulia walipotambua kwamba taifa lao lilikuwa limeshindwa kutii Sheria ya Mungu.​—Neh. 8:1-9.

3. Waisraeli walitii muongozo gani?

3 Hata hivyo, hiyo haikuwa siku ya kuungama zambi. Kwa kuwa ilikuwa sikukuu, Waisraeli walipaswa kumwabudu Yehova kwa furaha. (Hes. 29:1) Kwa hiyo, Nehemia aliwaambia watu hivi: ‘Muende, mule vitu vinono na kunywa vitu vitamu, nanyi mumupelekee mafungu ya vitu yule ambaye hakutayarishiwa kitu; kwa maana leo ni siku takatifu kwa Bwana wetu, wala musiwe na uchungu, kwa maana shangwe ya Yehova ndiyo ngome yenu.’ Inafurahisha kwamba watu walitii, na siku hiyo ikawa siku ya “kushangilia sana.”​—Neh. 8:10-12.

4. Wanaume waliokuwa vichwa vya familia walifanya nini, na walitambua jambo gani lililokuwa sehemu ya maana sana ya Sikukuu hiyo ya Vibanda?

4 Siku iliyofuata, wanaume waliokuwa vichwa vya makabila walikusanyika ili kuona namna gani taifa linaweza kufuata kwa ukaribu zaidi Sheria ya Mungu. Walipokuwa wakijifunza Maandiko, walitambua kwamba Sikukuu ya Vibanda na mukusanyiko huo wa maana wa kumalizia sherehe hiyo vilipaswa kufanywa kuanzia siku 15 mupaka siku 22 ya mwezi wa saba, unaoitwa Tishri, kwa hiyo walianza kufanya matayarisho. Sikukuu hiyo ya Vibanda ilikuwa nzuri sana kuliko zote zilizofanywa kuanzia siku za Yoshua na ilikuwa siku ya “kushangilia sana.” Sheria ya Mungu ilisomwa mbele ya watu wote ‘siku baada ya siku, tangu siku ya kwanza mupaka siku ya mwisho.’ Jambo hilo lilikuwa sehemu ya maana sana ya Sikukuu hiyo ya Vibanda.​—Neh. 8:13-18.

SIKU YA KUUNGAMA

5. Watu wa Mungu walifanya nini mbele Walawi watoe sala kwa ajili ya taifa lote?

5 Siku mbili baadaye, wakati ulifika sasa ili Waisraeli waungame zambi zao. Hiyo haikuwa siku ya karamu. Lakini, watu wa Mungu walifunga na walivaa magunia ili kuonyesha huzuni yao. Mara hii tena, Walawi walipaswa kuwasomea watu Sheria ya Mungu kwa saa tatu hivi asubuhi. Katika kipindi cha kisha muchana, ‘waliungama na kumuinamia Yehova Mungu wao.’ Kisha, Walawi walitoa sala iliyotayarishwa vizuri kwa ajili ya taifa lote. ​—Neh. 9:1-4.

6. Ni jambo gani lililowasaidia Walawi kutoa sala yenye maana, na hilo linatufundisha nini?

6 Bila shaka, kusoma mara kwa mara Sheria ya Mungu kuliwasaidia Walawi kutayarisha sala hii yenye maana. Mistari kumi ya kwanza ya sala hiyo inakazia matendo na sifa za Yehova. Mistari mingine inazungumuzia sana “rehema nyingi” za Mungu na inaonyesha waziwazi kwamba Waisraeli hawakustahili kuonyeshwa rehema hizo. (Neh. 9:19, 27, 28, 31) Ili sala zetu ziwe pia nzuri na zenye maana kama sala ya Walawi hao, tunapaswa kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku, kwa kufanya hivyo, tunamuruhusu Yehova azungumuze nasi mbele ya kusali.​—Zab. 1:1, 2.

7. Walawi walimuomba Mungu nini, na jambo hilo linatufundisha nini?

7 Katika sala hiyo Walawi walimuomba Yehova jambo moja tu. Jambo hilo linapatikana katika sehemu ya mwisho ya Nehemia 9:32, inayosema hivi: ‘Na sasa, Ee Mungu wetu, Mungu mukubwa, mwenye nguvu na mwenye kuogopesha, anayeshika agano na fazili zenye upendo, usiache magumu yote ambayo yametupata sisi, wafalme wetu, wakubwa wetu na makuhani wetu na manabii wetu na mababu zetu na watu wako wote tangu siku za wafalme wa Ashuru mupaka leo hii, yaonekane kuwa madogo mbele zako.’ Kwa kufanya hivyo, Walawi walituachia mufano muzuri wa kumusifu na kumushukuru Yehova mbele ya kumuomba mambo fulani ya kipekee.

WALISIFU JINA TUKUFU LA MUNGU

8, 9. (a) Walawi walianza sala yao kwa maneno gani ya unyenyekevu? (b) Ni majeshi gani mawili ya mbinguni ambayo Walawi walizungumuzia?

8 Ijapokuwa sala yao ilikuwa yenye kutayarishwa vizuri, Walawi hao walikuwa wanyenyekevu na walitambua kwamba hawakuwa na maneno yanayofaa kabisa ambayo wangeweza kutumia ili kumusifu Yehova namna inavyostahili. Kwa hiyo, walianza sala yao na maneno haya ya unyenyekevu: “Na walibariki jina lako tukufu, ambalo limeinuliwa juu ya baraka na sifa zote.”​—Neh. 9:5.

9 Kisha waliongezea hivi: ‘Wewe peke yako ndiye Yehova; wewe mwenyewe umezifanya mbingu, hata mbingu za mbingu, na jeshi lao lote, dunia na vyote vilivyo juu yake, bahari na vyote vilivyomo; nawe unavihifazi vyote hai; na jeshi la mbinguni linakuinamia wewe.’ (Neh. 9:6) Bila shaka, Yehova Mungu ndiye aliyeumba ulimwengu wote muzima, unaofanyizwa na galaksi nyingi za nyota. Aliumba pia kila kitu kinachopatikana katika dunia yetu nzuri na alitolea kila kiumbe uwezo wa ajabu wa kuendelea kuzaa ao kutokeza kiumbe kingine kulingana na aina yake. Malaika watakatifu wa Mungu, wanaoweza kuitwa pia “jeshi la mbinguni,” walijionea mambo hayo. (1 Fal. 22:19; Ayu. 38:4, 7) Zaidi ya hayo, malaika wanafanya kwa unyenyekevu mapenzi ya Mungu kwa kuwatumikia wanadamu wenye zambi ‘watakaoriti wokovu.’ (Ebr. 1:14) Bila shaka, malaika wanatuwekea mufano muzuri sana tunapoendelea kumutumikia Yehova kwa umoja kama jeshi lenye kuzoezwa vizuri!​—1 Kor. 14:33, 40.

10. Tunajifunza nini kutokana na mambo ambayo Mungu alimutendea Abrahamu?

10 Kisha, Walawi walizungumuzia mambo ambayo Mungu alimutendea Abramu, ambaye kwa umri wa miaka 99 alikuwa hajazaa mutoto pamoja na Sarai bibi yake, aliyekuwa tasa. Wakati huo, Yehova alibadili jina lake kuwa Abrahamu, linalomaanisha “baba ya umati [watu wengi sana].” (Mwa. 17:1-6, 15, 16) Mungu alimuahidi pia Abrahamu kwamba uzao wake ungeriti inchi ya Kanaani. Wanadamu wanasahau kila mara ahadi wanazotoa, lakini Yehova hasahau. Kama sala ya Walawi inavyoonyesha: ‘Wewe ndiye Yehova Mungu wa kweli, uliyemuchagua Abramu na kumuleta kutoka Uru la Wakaldayo na kulifanya jina lake kuwa Abrahamu. Nawe ukaona moyo wake kuwa ni mwaminifu mbele zako; basi ukafanya lile agano pamoja na yeye ili umupe inchi ya Wakanaani, . . . kuupa uzao wake; nawe ukatimiza maneno yako, kwa maana wewe ni mwadilifu.’ (Neh. 9:7, 8) Acheni sisi pia tumuige Mungu wetu mwadilifu kwa kujikaza siku zote kutimiza ahadi tunazotoa.​—Mt. 5:37.

MATENDO YA YEHOVA

11, 12. Jina la Yehova linamaanisha nini, na namna gani aliwatendea wazao wa Abrahamu kulingana na maana ya jina hilo?

11 Jina la Yehova linamaanisha “Yeye Anafanya Kuwa,” hilo linaonyesha kwamba Mungu anaendelea kutenda ili ahadi zake zitimie. Mambo ambayo Mungu aliwatendea wazao wa Abrahamu wakati walikuwa watumwa huko Misri yanashuhudia vizuri zaidi jambo hilo. Wakati huo, ilionekana kwamba haingewezekana taifa lote likombolewe na kuingia katika Inchi ya Ahadi. Hata hivyo, Mungu alitimiza ahadi yake hatua kwa hatua, kwa kufanya hivyo alionyesha kwamba yeye ndiye anayestahili kuitwa kwa jina hilo kubwa na la pekee, Yehova.

12 Sala iliyoandikwa na Nehemia inasema hivi kumuhusu Yehova: ‘Uliona mateso ya mababu zetu huko Misri, nawe ukasikia kilio chao kwenye Bahari Nyekundu. Ndipo ukatoa ishara na miujiza juu ya Farao na watumishi wake wote na watu wote wa inchi yake, kwa maana ulijua kwamba walitenda kwa kimbelembele juu yao; nawe ukajifanyia jina kama ilivyo leo hii. Nawe ukapasua bahari mbele yao, nao wakavuka katikati ya bahari juu ya inchi kavu; na wale waliokuwa wakiwafuatilia ukawatupa ndani ya vilindi vya bahari kama jiwe katika maji yenye nguvu.’ Kisha, sala hiyo inazungumuzia mambo mengine ambayo Yehova alikuwa amewafanyia watu wake: ‘Basi wana wao wakaingia, wakaichukua inchi hiyo na kuimiliki, nawe ukatiisha mbele yao wakaaji wa inchi hiyo, Wakanaani . . . Nao wakaanza kuteka majiji yenye ngome na udongo munono na kumiliki nyumba zilizojaa vitu vyote vyema, matangi yaliyochimbwa chini, mashamba ya mizabibu na ya mizeituni na miti ya vyakula kwa wingi, nao wakaanza kula na kushiba na kunenepa na kufanikiwa katika wema wako mukubwa.’​—Neh. 9:9-11, 24, 25.

13. Namna gani Yehova aliwatimizia Waisraeli mahitaji yao ya kiroho, lakini waliitikia namna gani?

13 Kuna mambo mengine mengi ambayo Mungu aliendelea kufanya ili kutimiza kusudi lake. Kwa mufano, muda kidogo tu kisha Waisraeli kutoka Misri, Yehova aliwatimizia mahitaji yao ya kiroho. Walawi walikumbusha jambo hilo katika sala yao waliposema hivi: ‘Nawe ukashuka chini kwenye Mulima Sinai na kusema nao kutoka mbinguni na kuwapa maamuzi ya hukumu yaliyo manyoofu na sheria za kweli, masharti na amri nzuri.’ (Neh. 9:13) Yehova aliwafundisha watu wake ili wastahili kulibeba jina lake takatifu wakiwa wariti wa Inchi Iliyoahidiwa, lakini walisahau mambo mazuri waliyojifunza.​—Soma Nehemia 9:16-18.

NIZAMU NI YA LAZIMA

14, 15. (a) Namna gani Yehova aliwatendea watu wake walipofanya makosa? (b) Namna ambavyo Mungu alitendea taifa lake chaguliwa inatufundisha nini?

14 Sala ya Walawi inazungumuzia makosa mawili ambayo Waisraeli walifanya muda kidogo tu kisha kuahidi kwamba watatii Sheria ya Mungu kwenye Mulima Sinai. Kwa sababu ya makosa haya, walistahili kabisa kufa. Lakini, Walawi hao walimusifu Yehova hivi: “Katika rehema zako nyingi hukuwaacha nyikani. . . . Na kwa miaka 40 ukawapa chakula. . . . Hawakukosa chochote. Mavazi yao hayakuchakaa, wala miguu yao haikuvimba.” (Neh. 9:19, 21) Leo, Yehova anatutolea pia kila kitu tunachohitaji ili kumutumikia kwa uaminifu. Acheni tusiwe hata kidogo kama Waisraeli wengi waliokufa katika nyika kwa sababu ya kukosa utii na imani. Zaidi ya hayo, mambo hayo “yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.”​—1 Kor. 10:1-11.

15 Inasikitisha kwamba, kisha kuingia katika Inchi ya Ahadi, Waisraeli wengi walianza kuabudu miungu ya Wakanaani. Ibada hiyo ilitia ndani uasherati na kutoa watoto wao kuwa sadaka kwa miungu hiyo. Kwa hiyo, Yehova aliruhusu mataifa jirani yatese taifa lake chaguliwa. Walipotubu, Yehova aliwaonyesha rehema na aliwaokoa kutoka katika mikono ya maadui wao. Hali hiyo ilitokea “tena na tena.” (Soma Nehemia 9:26-28, 31.) Walawi walisali hivi: ‘Uliwavumilia kwa miaka mingi nawe ukaendelea kutoa ushahidi juu yao kwa roho yako kupitia manabii wako, wala hawakutega sikio. Mwishowe ukawatia mikononi mwa watu wa inchi hizo.’​—Neh. 9:30.

16, 17. (a) Matokea yalikuwa nini wakati Waisraeli waliangukia tena katika kosa la kutokutii? (b) Waisraeli walitambua nini, na waliahidi kufanya nini?

16 Hata kisha kutoka uhamishoni, Waisraeli waliangukia tena katika kosa la kutokutii. Lakini kulikuwa tofauti gani? Walawi waliendelea kusali hivi: ‘Tazama! Sisi leo ni watumwa; na tazama! sisi ni watumwa juu ya inchi ambayo uliwapa mababu zetu, ili wale matunda yake na vitu vyake vyema, na mazao yake yamejaa kwa ajili ya wafalme ambao umeweka juu yetu kwa sababu ya zambi zetu . . . nasi tumo katika taabu kubwa.’​—Neh. 9:36, 37.

17 Je, Walawi walitaka kuonyesha kwamba Mungu aliwatendea watu wake isivyo haki kwa kuruhusu wapatwe na taabu kubwa? Hapana kabisa! Walisali hivi: “Nawe ni mwadilifu kuhusu mambo yote ambayo yametupata, kwa maana umetenda kwa uaminifu, lakini sisi ndio tumetenda kwa uovu.” (Neh. 9:33) Kisha, walimalizia sala hiyo kwa kumutolea Mungu ahadi nzito, kwamba taifa litatii Sheria ya Mungu. (Soma Nehemia 9:38; 10:29) Mwishowe, waliandika ahadi hiyo na viongozi wa Wayahudi 84 walitia muhuri kwenye maandishi hayo.​—Neh. 10:1-27.

18, 19. (a) Tunahitaji kufanya nini ili tuokoke na kuingia katika ulimwengu mupya wa Mungu? (b) Tunapaswa kuendelea kusali kuhusu jambo gani, na sababu gani?

18 Tunahitaji nizamu ya Yehova ili tustahili kuingia katika ulimwengu wake mupya wenye haki. Mutume Paulo aliuliza hivi: ‘Ni mwana gani ambaye baba hamutie nizamu?’ (Ebr. 12:7) Tunaonyesha kwamba tunakubali muongozo wa Mungu katika maisha yetu kwa kuendelea kumutumikia kwa uaminifu na kukubali roho yake itufinyange. Na ikiwa tunafanya zambi nzito, tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atatusamehe ikiwa tunatubu kwelikweli na kukubali kwa unyenyekevu nizamu yake.

19 Karibuni, Yehova atalitukuza jina lake kubwa kuliko namna alivyofanya alipowakomboa Waisraeli kutoka Misri. (Eze. 38:23) Na kama vile ambavyo watu wake waliriti Inchi ya Ahadi, Wakristo wote wanaoendelea kumutumikia Mungu kwa uaminifu watapokea uzima kuwa uriti katika ulimwengu mupya wa Mungu wenye haki. (2 Pet. 3:13) Kwa kuwa tunangojea ahadi hiyo nzuri, acheni tuendelee kusali ili jina tukufu la Mungu litakaswe. Habari inayofuata itazungumuzia sala nyingine inayoweza kutusaidia kupokea baraka za Mungu kuanzia sasa na milele.