Hamia kwenye habari

Kuhitimu kwa Darasa la 138 la Shule ya Gileadi

Kuhitimu kwa Darasa la 138 la Shule ya Gileadi

Machi 14, 2015, darasa la 138 la Shule ya Gileadi lilihitimu katika kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova cha Patterson, New York. Zaidi ya watu 14,000 walisikiliza programu hiyo, kutia ndani waliounganishwa kupitia Intaneti katika maeneo mengine. Programu ilianza kwa kipindi cha muziki chenye nyimbo nne mpya za Ufalme, ambazo ziliimbwa baadaye na wote waliohudhuria. *

Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mwenyekiti wa programu. Katika utangulizi wake, aliwatia moyo wanafunzi wasiwanyime wengine ujuzi waliopata bali watumie mazoezi waliyopata kuwanufaisha wengine.​—2 Timotheo 2:2.

Ndugu Jackson alizungumzia kielelezo cha Musa. Kwa kipindi fulani, hema la Musa lilitumika kama mahali pa ibada kwa taifa la Israeli. Hata hivyo, maskani ilipokamilika, ilitumiwa kwa ajili ya ibada. Inaonekana kwamba Musa hakuruhusiwa kuingia mahali Patakatifu Zaidi pa maskani; pendeleo hilo lilikuwa la kuhani mkuu. Hata hivyo, hakuna lolote linaloonyesha kwamba Musa alinung’unika kwa sababu ya mabadiliko hayo. Badala yake, alimuunga mkono kwa ushikamanifu Haruni katika mgawo wake mpya akiwa kuhani mkuu. (Kutoka 33:​7-​11; 40:34, 35) Tunajifunza nini? Ndugu Jackson alisema, “Thamini mapendeleo, lakini usiwazuie wengine kuyapata.”

“Je, Utaogopeshwa na Sauti ya Jani?” Hicho ndicho kichwa cha hotuba iliyotolewa na Kenneth Flodin, msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza. Alisema kwamba ni kweli wanafunzi wanaweza kukabili hali zinazoweza kuwaogopesha, kama vile kuteswa au kupewa mgawo mgumu. Kwa kutumia andiko la Mambo ya Walawi 26:36, aliwahimiza wanafunzi kwamba watakapokabili hali ngumu wazione kuwa kama jani lililokauka na si kama tatizo lisiloweza kushindwa. Kisha Ndugu Flodin alikazia mfano wa mtume Paulo, ambaye alivumilia magumu mengi kwa sababu alimtumaini Yehova.​—2 Wakorintho 1:​8, 10.

“Mnatafuta Nini?” Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba iliyofuata katika programu. Alizungumzia kanuni iliyo katika Methali 13:12, inayosema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Inahuzunisha kwamba watu wengi huishi maisha yao yote wakiwa wamekata tamaa kwa sababu walijiwekea miradi ambayo hawawezi kamwe kufikia, kama vile utajiri au umaarufu.

Katika siku za Yesu, baadhi ya watu walikuwa na matazamio yasiyofaa kuhusu Yohana Mbatizaji. (Luka 7:​24-​28) Kwa mfano, huenda walitazamia kwamba angekuwa mwanafalsafa ambaye angewafurahisha kwa nadharia zisizo na msingi. Ikiwa ndivyo, walikatishwa tamaa kwa kuwa Yohana alifundisha kweli zilizo na msingi imara. Huenda wengine walitazamia angekuwa mtu mwenye kuvutia. Lakini Yohana alivaa mavazi ya watu maskini. Hata hivyo, wale waliotazamia nabii hawakukatishwa tamaa, kwa kuwa Yohana hakuwa nabii tu bali pia mtangulizi wa Masihi!​—Yohana 1:​29.

Akitumia shauri hilo, Ndugu Sanderson aliwahimiza wanafunzi kutafuta mambo yanayofaa. Badala ya kutafuta umaarufu au kutazamia kutendewa kwa njia ya pekee katika mgawo wao, wanapaswa kutumia mazoezi yao kuwanufaisha wengine. Wanaweza kufanya hivyo kwa kushiriki na wengine mambo waliyojifunza katika Gileadi, kwa kuimarisha imani ya ndugu na dada zao, na kwa kuwapenda. Ndugu Sanderson alisema, “Watumikie kwa unyenyekevu ndugu na dada zako na ufanye yote uwezayo kutimiza mapenzi ya Yehova, nawe hutakata tamaa.”

“Walishe Wenye Njaa.” Hicho ndicho kichwa kilichozungumziwa na James Cauthon, mwalimu katika Idara ya Shule za Kitheokrasi. Ndugu Cauthon alisema kwamba kila mtu ana njaa ya kupendwa, kuthaminiwa, na kutambuliwa. Hata Yesu alikuwa na uhitaji huo, na Yehova aliutimiza kwa kusema maneno yenye kugusa moyo wakati wa ubatizo wa Yesu.​—Mathayo 3:​16, 17.

Yehova ametupa uwezo wa kuwatia moyo na kuwaimarisha wengine kwa maneno yetu, na anatarajia tutumie uwezo huo. (Methali 3:​27) Ndugu Cauthon aliwahimiza hivi: “Jizoeze kuona mambo mazuri ya watu wengine na uwe tayari kuwapongeza.” Pongezi za kutoka moyoni huwasaidia waamini wenzetu watambue kwamba jitihada zao zinathaminiwa.

“Kujitoa Mpaka Tone la Mwisho.” Mark Noumair, msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji, alitoa hotuba iliyofuata katika programu. Kwa kutumia mfano wa mtume Paulo, Ndugu Noumair aliwatia moyo wanafunzi wasiridhike na kufanya mambo ya msingi tu. Badala yake, kama Paulo, watapata shangwe ya kweli wakijitoa kabisa kwa ajili ya wengine.​—Wafilipi 2:​17, 18.

Paulo hakukata tamaa hata alipokabili magumu. Kwa sababu alijitoa hadi kifo chake, ni kana kwamba alijimimina mpaka tone la mwisho. Hivyo alisema hivi kwa uhakika: “Nimekimbia mwendo mpaka mwisho.” (2 Timotheo 4:​6, 7) Ndugu Noumair aliwatia moyo wanafunzi wamwige Paulo kwa kuunga mkono kazi ya Ufalme katika migawo yao.

Mambo Yaliyoonwa. Mwalimu mwingine wa Gileadi, Michael Burnett, aliongoza sehemu iliyofuata kwenye programu, ambapo baadhi ya wanafunzi waliigiza mambo yaliyoonwa ambayo walifurahia katika huduma ya shambani walipokuwa Patterson.

Tena na tena, wanafunzi walipata matokeo mazuri kwa kutafuta fursa za kutoa ushahidi na kwa kujitahidi kushiriki na wengine kweli katika “lugha ya moyoni”​—yaani, katika lugha yao ya kwanza. Kwa mfano, mwanafunzi mmoja aliambiwa kwamba kuna watu wengi waliozungumza Kihispania katika eneo alilopanga kuhubiri. Hivyo siku hiyo kabla ya kwenda kuhubiri, alijifunza maneno machache ya Kihispania kwa kutumia programu ya JW Lugha. Siku hiyohiyo, alikutana na mwanamume mmoja barabarani aliyezungumza Kihispania. Kwa kutumia maneno machache aliyojifunza, mwanafunzi huyo alianzisha mazungumzo ambayo yaliongoza kwenye funzo la Biblia pamoja na mtu huyo na watu wanne wa familia yake.

Mahojiano. William Turner, Jr., msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza, aliwahoji wanafunzi wanne kuhusu mambo waliyopitia kabla ya kuja Gileadi na kuhusu mazoezi waliyopokea kwenye shule.

Wanafunzi walisimulia mambo waliyojifunza shuleni ambayo yaliwatia moyo kibinafsi. Kwa mfano, mwanafunzi mmoja alieleza kile ambacho alijifunza kutokana na simulizi la Luka sura ya 10. Wanafunzi 70 waliotumwa na Yesu walishangilia walipopata matokeo mazuri katika huduma. Ingawa Yesu pia alishangilia, aliwafundisha wanafunzi wake wasitegemeze shangwe yao juu ya matokeo waliyopata tu lakini hasa katika kujua kwamba Yehova anafurahishwa na jitihada zao. Hilo linatukumbusha kwamba shangwe ya kweli, haitegemei hali tulizo nazo, bali kuwa na kibali cha Yehova.

Ndugu Turner aliwaonyesha wanafunzi jinsi andiko la Wafilipi 1:6 linavyowahusu, na kuwahakikishia kwamba Yehova alikuwa ‘ameanza kazi njema’ ndani yao na kwamba Yehova ataendelea kuwa pamoja nao.

“Mkazieni Macho Yehova.” Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi katika programu. Alisema ni kweli kwamba hatuwezi kumwona Yehova. Hivyo, inawezekanaje kumkazia macho?

Njia moja tunayoweza kumwona Yehova ni kwa kuchunguza uumbaji wake, ambao hutufundisha kumhusu. Pia, ‘macho ya moyo wetu . . . yametiwa nuru’ na Yehova. (Waefeso 1:​18) Kadiri tunavyoendelea kusoma Biblia, ndivyo tunavyozidi kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova. Na kadiri tunavyojifunza kumhusu Yehova, ndivyo tunavyomkaribia zaidi.

Tunapaswa kukazia uangalifu vitabu vya Injili, kwa kuwa vinatupa picha kamili ya Yehova kupitia maneno na matendo ya Mwana wake. Yesu alikuwa na utu kama wa Yehova hivi kwamba angesema: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”​—Yohana 14:9.

Ndugu Herd aliwatia moyo wahudhuriaji wamkazie macho Yehova kupitia mfano wa Yesu na waige mambo wanayoona. Kwa mfano, kama Yesu alivyojitahidi kuwalisha wengine, sisi pia tunahitaji kufanya kazi kwa bidii ili kushiriki na wengine chakula cha kiroho ambacho tumepokea.

Tunapata matokeo gani kwa kumkazia macho Yehova? Tunaweza kuwa na uhakika kama wa mtunga zaburi aliyeandika: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.”​—Zaburi 16:8.

Umalizio. Baada ya wanafunzi kupokea vyeti vyao, mmoja wa wanafunzi alisoma barua ya shukrani kutoka kwa wanafunzi. Kisha Ndugu Jackson alimalizia kwa kuwaambia wanafunzi kwamba hawahitaji kufikiri kwamba kila kitu watakachofundisha lazima kiwe kipya au chenye kusisismua. Kwa sehemu kubwa, watakuwa wakiwakumbusha ndugu na dada zao mambo ambayo tayari wanayafahamu. Ndugu Jackson alikazia pia umuhimu wa unyenyekevu. Badala ya kuelekeza fikira kwa mazoezi waliyopokea Gileadi au kujielekea, wahitimu wanapaswa kuelekeza fikira kwenye Biblia na kwenye machapisho yanayotegemea Biblia. Hivyo, badala ya kuwavunja moyo wale ambao huenda hawatapata nafasi ya kuhudhuria shule ya Gileadi, wahitimu watawatia moyo waamini wenzao kwa kuwasaidia kunufaika kutokana na maandalizi ya kiroho ambayo wanaweza kupata. Wote waliohudhuria waliondoka wakiwa wamejengwa na wakiwa wameazimia kuwatumikia ndugu na dada zao.

^ fu. 2 Wote ambao walialikwa kuhudhuria programu hiyo walipewa nyimbo hizo mpya juma moja kabla ya programu.

^ fu. 32 Si nchi zote zinazoonekana kwenye ramani.

^ fu. 34 Wahitimu wote hawajaorodheshwa