Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Wanashiriki Katika Ibada za Dini Nyingine?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanashiriki Katika Ibada za Dini Nyingine?

 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunafurahia kuzungumza na watu wote kuhusu mambo tunayoamini, lakini hatushiriki katika ibada za dini nyingine. Biblia inaonyesha kwamba Wakristo wa kweli ‘wameunganishwa pamoja kwa upatano,’ na sehemu muhimu ya upatano huo ni umoja wa imani. (Waefeso 4:16; 1 Wakorintho 1:10; Wafilipi 2:2) Hilo linahusisha mambo mengi zaidi ya kukubaliana tu kuhusu umuhimu wa sifa kama vile upendo, huruma, na kusamehe. Imani yetu inategemea ujuzi sahihi wa Biblia, na ikiwa hatungefanya hivyo imani hiyo ingekuwa ya bure.​—Waroma 10:2, 3.

 Biblia inasema kwamba kushiriki katika ibada pamoja na watu walio na imani tofauti ni sawa na kuwa chini ya nira isiyo sawa. Jambo hilo linaweza kuathiri imani ya Mkristo. (2 Wakorintho 6:14-17) Hivyo, Yesu hakuwaruhusu wanafunzi wake washiriki katika ibada za dini nyingine. (Mathayo 12:30; Yohana 14:6) Vivyo hivyo, Sheria ya Mungu kupitia Musa iliwakataza Waisraeli wa kale wasijiunge katika ibada na majirani wao. (Kutoka 34:11-14) Baadaye, Waisraeli waaminifu walikataa msaada ambao ungewafanya wawe na mapatano ya kidini na watu wa imani nyingine.​—Ezra 4:​1-3.

Je, Mashahidi wa Yehova wanakubali kuwa na mazungumzo na watu wa dini nyingine?

 Ndiyo. Katika mwaka wa 2023 tulitumia saa 1,791,490,713 kuzungumza na watu walio na imani tofauti na yetu. Kama mtume Paulo, tungependa kuelewa jinsi “watu . . . wengi zaidi” tunaokutana nao katika huduma wanavyofikiri na kuamini. (1 Wakorintho 9:19-22) Tunapozungumza nao, tunajaribu sana kutumia ushauri wa Biblia wa kuwaonyesha watu wengine “heshima kubwa.”​—1 Petro 3:15.